ASKOFU GWAJIMA KASHINDWA KUFIKA MAHAKAMANI LEO KUSIKILIZA HUKUMU YA KESI YAKE


Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu Agosti 30, 2017 itatoa hukumu katika kesi ya kushindwa kuhifadhi silaha na risasi inayomkabili Askofu wa Kanisa la ufufuo na uzima, Josephat Gwajima na wenzake watatu.

Hukumu hiyo ilipaswa kutolewa leo Jumatatu, Julai 31 kwa Hakimu Mfawidhi, Cyprian Mkeha lakini ilishindikana kwa sababu hakimu huyo alikuwa na udhuru.

Hata hivyo, Wakili Peter Kibatala amemueleza Hakimu Mkazi Mkuu, Godfrey Mwambapa wakati kesi ilipoitwa mbele yake kuwa Askofu Gwajima ni mgonjwa na mahakamani hapo amewakilishwa na mdhamini wake.

Hayo yametokea baada wakili wa Serikali, Shedrack Kimaro kuiambia mahakama kuwa washtakiwa George Mzava, Msaidizi wa Askofu Gwajima, Yekonia Bihagaze (39) na Georgey Milulu wapo mahakamani lakini Askofu Gwajima hayupo.

Pia, amedai kesi ilipangwa kwa ajili ya washtakiwa hao kusomewa hukumu lakini wamepata taarifa Hakimu Mfawidhi, Mkeha anayeisikiliza kesi hiyo anaudhuru.

Baada ya kutolewa kwa maelezo hayo kesi imeahirishwa hadi Agosti 30, 2017 ambapo watasomewa hukumu.

Mzava, Bihagaze na Milulu wao wanakabiliwa na mashtaka mawili ya kukutwa wakimiliki bastola aina ya berretta pamoja na risasi 20 kinyume cha sheria.

Hukumu hiyo inatarajiwa kutolewa siku hiyo na Hakimu Mfawidhi wa mahakama hiyo, Cyprian Mkeha mara baada ya mashahidi wa upande wa mashtaka na utetezi kutoa ushahidi wao na kuufunga.

Katika kesi hiyo, upande wa mashtaka uliwakilishwa na Mawakili wa Serikali, Shedrack Kimaro na Joseph Maugo.

Huku upande wa utetezi uliwakilishwa na Wakili Peter Kibatala ambapo washtakiwa walijitetea pamoja na mashahidi wao wawili akiwamo Nesi wa hospitali ya TMJ, Devotha Bayona na Mchungaji wa Kanisa la Ufufuo na Uzima George Kiwia.

Katika ushahidi wa upande wa utetezi wa shahidi, Devotha alidai kuwa yeye ni afisa muugizi daraja la pili katika Hospitali ya TMJ na yupo kitengo cha ICU.

Machi 29, 2015 aliingia zamu usiku akipokea zamu toka kwa Nesi Rebecca ambaye aliacha kazi 2016 wakati huo Askofu alikuwa amelazwa katika hospitali hiyo kwa siku ya tatu.

Anakumbuka siku hiyo walikwenda askari wawili na mtu mwingine Bihagaze wakagonga mlango wa ICU wakahitaji begi la mgonjwa, walivyojitambulisha alitaka kuhakikisha ni kweli akamfuata Gwajima na kumuuliza. Alieleza ushahidi.

Amedai Gwajima alimueleza ni kweli Bihagaze ni msaidizi wake na kwamba Bihagaze alimwambia yupo pamoja na askari hao wanataka begi la mgonjwa.

Muuguzi huyo amesema Gwajima alisema hawezi kutoa begi hadi wapewe maelezo maalumu na kwamba begi hilo lilikuwepo pembeni ya kitanda cha Gwajima.

Baada ya kupewa majibu hayo na Gwajima, aliwaambia polisi amesema hawezi kulitoa hadi polisi waandike maelezo, wakamueleza wanachohitaji ni begi na maelezo wataandika kesho.

Wakati wanajibizana Gwajima alisikia na akamwambia nesi atawapa hilo begi kwa sababu ndani Lina silaha yake.

“Polisi walitaka kuingia kinguvu nikawaambia hapa ni ICU hamuwezi kuingia kinguvu, " alieleza nesi huyo na kwamba Gwajima alimwambia kama wanalihitaji kinguvu chukua begi mpe Bihagaze awape polisi.

Amedai kabla hajampatia begi hilo Bihagaze polisi walimpokonya, akafunga mlango akaendelea na mgonjwa wake lakini alimuona mgonjwa anamawazo.

Washtakiwa wengine mbali na Gwajima wao wanadaiwa kuwa Machi 29, 2015 katika Hospitali ya TMJ iliyopo Mikocheni A walikutwa wakimiliki Bastola aina ya Berretta yenye namba ya siri CAT 5802 bila ya kuwa na kibali toka kwa mamlaka inayohusika na silaha na milipuko.

Imeendelea kudaiwa kuwa washtakiwa hao walifanya kosa hilo kinyume na kifungu cha 32 (1) na cha 34 (1) (2) na(3) cha sheria ya Silaha na Milipuko sura ya 223 iliyofanyiwa marekebisho mwaka 2010.

Pia, wanadaiwa kuwa siku hiyo ya tukio washtakiwa hao pia walikutwa wakimiliki isivyo halali risasi tatu za bastola pamoja na risasi 17 za bunduki aina ya Shotgun.

Washtakiwa hao wapo nje kwa dhamana baada ya kukamilisha masharti waliyopewa ya kuwa kila mshtakiwa awe na mdhamini mmoja anayeaminika ambaye alisaini hati ya maneno ya dhamana yenye thamani ya Sh1 milioni.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527