MWENDESHA BODABODA AFARIKI BAADA YA KUKAMATWA NA ASKARI POLISI SHINYANGA,VURUGU YATOKEA



Wananchi wakiwa eneo la tukio


Kamanda wa polisi mkoa wa Shinyanga ACP Muliro Jumanne Muliro akiwa eneo la tukio-Picha na Marco Maduhu 

***
Mwendesha bodaboda aliyejukana kwa jina la Joel Gabriel Mamla amefariki dunia baada ya kupasuka kichwa kwa kuanguka kwenye pikipiki aliyokuwa amembeba na askari polisi aliyemkamata kwa makosa ya usalama barabarani .


Kwa Mujibu wa mashuhuda wa tukio hilo wanasema mwendesha bodaboda huyo amepoteza maisha kwa kuanguka kwenye pikipiki aliyokuwa amembeba askari polisi aliyekuwa amevaa kiraia.


Kufuatia kifo hicho wananchi waliamua kumshushia kichapo askari polisi huyo na jeshi la polisi kulazimika kutumia mabomu ya machozi kuwatawanya wananchi waliokuwa wanamtuhumu kusababisha kifo hicho.

"Tulishuhudia mwendesha bodaboda akivutana na askari polisi baada ya kumkaba shingoni bila kuelewa sababu na baadae ajali ikatokea"

"Wamekuja wanavutana kwenye pikipiki,walikuwa wanakabana juu ya pikipiki,walipofika eneo ambako yanatokea mabasi,askari akawa anaburuza miguu chini,mara akamkaba mwendesha bodaboda ili pikipiki isimame,askari akamkaba roba dereva,ikabidi aachie usukani,alivyotaka kurudi akakuta pikipiki imeshahama barabarani ndiyo akakutana na alama ya barabarani akaibamiza,akaangukia jiwe ndivyo kifo chake kilivyotokea,sisi tulijua huyo askari pengine ni raia maana hakuvaa kiraia",mashuhuda wa tukio hilo wanasimulia hali ilivyokuwa.


Mganga Mfawidhi wa hospitali ya rufaa ya mkoa wa Shinyanga,Dkt. Herbert Masigati amethibitisha kutokea kwa kifo cha mwendesha bodaboda huyo na kuongeza kuwa alipasuka kichwa baada ya ajali kutokea.


Taarifa ya jeshi la polisi mkoa wa Shinyanga kwa vyombo vya habari kuhusiana na ajali ya pikipiki kuanguka na kusababisha majeruhi kwa askari na mwendesha pukipiki (bodaboda) 


Tarehe 6/6/17 majira ya saa 1245 eneo la Soko kuu Manispaa ya Shinyanga, askari mmoja mwenye cheo cha CPL wa kikosi cha usalama barabarani akiwa na askari wenzake wawili wakiwa katika utekelezaji wa majukumu yao ya kisheria ya ukamataji wa kawaida wa waendesha pikipiki zisizotii sheria za barabarani,waliikamata pikipiki na MC 700 AWH SANLG iliyokuwa ikiendeshwa na Joel Gabriel Mamla, 26yrs kwa kosa la kutovaa helmet.


Mtuhumiwa huyo aliwakuta askari hao eneo la Soko Kuu na baada ya kushusha abiria ndipo alipoambiwa kosa lake na kuamriwa kwenda kituo cha polisi kwa hatua zaidi za kisheria.


Dereva huyo wa bodaboda alidai yeye ndiye atakayeendesha pikipiki yake na hivyo akampakia kwa nyuma askari polisi aliyekuwa amevaa kiraia aliyepewa jukumu na kiongozi wake ampeleke mtuhumiwa kituoni. 


Badala yake dereva huyo wa bodaboda alibadilisha uelekeo wa barabara baada ya kutoka pale sokoni na kuanza kuendesha kwa speed kubwa kuelekea barabara ya Tabora- Tinde huku akimweleza askari yule kuwa watakufa wote.


Alipofika eneo la Buhangija aliielekeza pikipiki kwenye nguzo ya alama ya usalama wa barabarani na akafanikiwa kuitumbukiza kwenye shimo kwa maksudi ambapo wote walianguka na hivyo kupata majeraha na wakakimbizwa hospitali ya mkoa kwa matibabu.

Uchunguzi wa kina kuhusiana na tukio hili unafanywa.

Hali zao ni mbaya.

Imetolewa na Muliro J Muliro RPC - Shinyanga.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post