KUWAIT YATOA BILIONI 110 KWA AJILI YA UJENZI WA BARABARA YA TABORA


RAIS John Magufuli ameishukuru Serikali ya Kuwait kwa kutoa mkopo wa Dola za Marekani milioni 51 (sawa na takribani Sh bilioni 110), kwa ajili ya kujenga barabara ya Chaya - Nyahua mkoani Tabora yenye urefu wa kilometa 85.

Barabara hiyo itaunganisha mawasiliano ya barabara kati ya mkoa wa Singida na Tabora. Rais Magufuli alitoa shukrani hiyo jana Ikulu Jijini Dar es Salaam, alipofanya mazungumzo na Balozi wa Kuwait hapa nchini, Jasem Ibrahim Al Najem na kupokea msaada wa magari mawili ya kusombea taka ngumu yenye thamani ya Dola za Marekani 200,000.

Magari hayo yametolewa na Serikali ya Kuwait kwa lengo la kuunga mkono kampeni ya usafi hapa nchini. “Naomba unifikishie salamu zangu kwa Mfalme wa Kuwait, mwambie tunathamini mchango mkubwa wa Kuwait katika maendeleo ya nchi yetu, hizi fedha za barabara mlizotupatia zitatusaidia kumalizia sehemu hiyo ya barabara ambayo ndio ilikuwa imebaki,” alisema Rais Magufuli.

Rais Magufuli pia aliishukuru Serikali ya Kuwait kwa kuunga mkono juhudi mbalimbali za utoaji wa huduma za kijamii nchini, ikiwemo msaada wa Dola za Marekani 250,000 kwa ajili ya kununulia vifaa katika Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete na visima vya maji safi 27 vilivyochimbwa Jijini Dar es Salaam kwa ajili ya wanafunzi na wananchi wa maeneo jirani na shule.

Aidha, Rais Magufuli aliishukuru Serikali ya Kuwait kwa kutoa Dola za Marekani milioni 50 kwa ajili ya kuikarabati Hospitali ya Rufaa ya Mnazi Mmoja iliyopo Zanzibar. Pia aliiomba Serikali ya Kuwait kuweka alama ya kumbukumbu ya uhusiano wake na Tanzania kwa kusaidia ujenzi wa barabara za makao makuu ya nchi mjini Dodoma.

Alimhakikishia Mfalme wa Kuwait, Sheik Sabah Al-Ahmad Al-Jaber Al-Sabah kuwa Serikali ya Awamu ya Tano itaendeleza na kuimarisha zaidi uhusiano na ushirikiano kati ya Tanzania na Kuwait, hususani katika masuala ya kiuchumi, ikiwemo mafuta na gesi ambayo imevumbuliwa kwa kiasi kikubwa nchini Tanzania.

Kwa upande wake, Balozi wa Kuwait hapa nchini, Jasem Ibrahim Al- Najem alielezea kufurahishwa kwake na uhusiano na ushirikiano mzuri kati ya nchi yake na Tanzania. Alimhakikishia Rais Magufuli kuwa Kuwait ipo tayari wakati wowote, kuunga mkono juhudi za maendeleo kulingana na vipaumbele vya Tanzania.

Wakati huo huo, Rais amefanya mazungumzo na Mjumbe Maalum wa Rais wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC), ambaye ni Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Mambo ya Nje wa Kongo, Leonard She Okitundu na kumhakikishia kuwa Tanzania inaunga mkono juhudi za kumaliza tofauti, kati ya pande zinazopinga nchini Kongo.

Pamoja na kukabidhi barua yenye ujumbe wa Rais wa DRC, Joseph Kabila, Balozi Leonard She Okitundu alimueleza Rais Magufuli kuwa hali ya Kongo ni shwari na kwamba mchakato wa mazungumzo kati ya pande zinazopingana nchini humo unaendelea vizuri.

Katika hatua nyingine, Rais Magufuli amefanya mazungumzo na Mjumbe Maalum wa Rais wa Jamhuri ya Msumbiji ambaye ni Waziri wa Ulinzi wa nchi hiyo, Jenerali Atanasio Salvador Ntumuke.

Baada ya mazungumzo hayo, Jenerali Atanasio Salvador Ntumuke alisema Msumbiji itaendelea kushirikiana na Tanzania kwa mambo mbalimbali kwa kuwa nchi hizo ni ndugu na zimesaidiana kwa mengi tangu harakati za kupigania uhuru, ambapo Tanzania ilitoa mchango mkubwa.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post