KAULI YA CCM KUHUSU UAMUZI WA RAIS MAGUFULI KUFANYA UTUMBUAJI ALIPOKABIDHIWA RIPOTI YA MCHANGA WA MADINI


Chama cha mapinduzi (CCM) leo May 25 2017 Dar es salaam kimezungumza na Waandishi wa habari kupitia kwa Katibu wake wa itikadi na uenezi Humphrey Polepole na kuzungumzia mambo mawili makubwa yanayoendelea.

JAMBO LA KWANZA: ‘Leo nitazungumza mambo mawili ambayo yamekua makubwa na yanaendelea kwenye taifa letu, moja ni swala la ulinzi na usalama wa Wananchi wetu wa Tanzania hasa zaidi katika muendelezo wa matukio kwenye eneo la Mkuranga, Kibiti na Rufiji‘

‘Sisi kama chama tumelifuatilia na kuona ni vyema kusimama na Watanzania wakiwemo Wanachama wa CCM katika maeneo haya kusema tuko pamoja, tunatambua wanapitia wakati mgumu, wapo waliopoteza maisha sio kwasababu ya mapenzi ya Mwenyenzi Mungu… wamepoteza maisha yao kwasababu yamekatizwa’

"Sitaki kusema maneno makubwa kwamba zaidi kwamba ikiendelea tutapenda kuona watu wengine wanawajibishwa.. niseme pia tumesikitishwa sana, sisi tunaamini demokrasia ya vyama vingi ni mshikamano lakini tunahisi kama tumeachwa wenyewe, tumevunjika moyo sana, ukimya wa wenzetu vyama vingine vya siasa umetusikitisha"

“Nimeona wenzangu wametingwa na kufanya siasa za madaraka kuliko siasa za maendeleo na zinazohusika na shida za watu wetu, hakuna namna nyingine nzuri ya kuwahudumia Watanzania kama kushikamana wakati wa matatizo bila kujali tofauti zetu za kiitikadi" – Polepole

JAMBO LA PILI: "Nalisema hili katika namna ambayo mara nyingi watu wamezoea na ni mazoea mabaya kwamba mtu akifanya jambo jema hatakiwi kusifiwa sababu ni wajibu wake, leo napenda niwaambie kivingine… jambo ambalo Rais Magufuli amelifanya jana ninawaomba kwa heshima kubwa Watanzania wote tumuunge mkono"

"Vita zipo za aina nyingi, zipo tunazopigana kwa silaha… mtu na mtu, nchi na nchi… wengi wamezoea hizi…. lakini zipi vita za kiuchumi, ni mbaya zaidi kuliko vita ya kupigana na silaha, inalenga kuturudisha nyuma na kufukia malengo ya sisi kuwa taifa huru na linalojitegemea"

"Nawaomba Watanzania sio tu WanaCCM kwa heshima kubwa tumuunge mkono Rais wetu mpendwa, atakua imara na madhubuti zaidi tukisimama nae sote"

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post