LIPUMBA: KUNA MATUKIO YANAPANGWA NJE YA CHAMA CHA CUF ILI KIFUTWE KWA VURUGU

Mwenyekiti wa chama cha wananchi CUF anayetambulika na ofisi ya msajili wa vyama vya siasa nchini Prof. Ibrahim Lipumba amesema ameandika barua maalumu kwa jukwaa la wahariri kuonesha kusikitishwa kwake na vurugu zilizotokea hivi karibuni katika mkutano wa CUF na kusababisha waandishi kufanyiwa fujo.

Prof Lipumba ameliomba jeshi la polisi kufanya uchunguzi juu ya tukio hilo ameyasema hayo katika mahojiano na mwandishi wa habari wa Azam Two na pamoja na mambo mengine amemtaka katibu mkuu wa CUF Maalim Seif wakae wazungumze ili wamalize tofauti zao na wakae wakijenge chama..

“Baada ya kulisikia hilo niliamua kuchukua jukumu la kuwaandikia Jukwaa la wahariri barua ambayo ipo mbioni kwenda kwenye ofisi zao kwamba mimi binafsi kama mwenyekiti wa CUF nalaani kitendo cha kupigwa kwa waandishi wa habari na ni jambo ambalo hatulikubali kabisa, hatuwezi kujenga Demokrasia ikiwa waandishi wa habari hawafanyi kazi yao katika hali ya amani na utulivu”.

“Vile vile kijana wetu amekatwa kisigino kwa panga na anavyo elewa yeye kijana aliyemkata anaitwa Mohamedi Mgonvi na taarifa hii imepelekwa kwenye vyombo vya dola kwa hiyo vyombo vya dola vinalishughulikia na tulitoa wito ambao ulitolewa na Mkurugenzi wetu wa habari na uenezi”

“Mimi toka awali nimeeleza kwamba nataka tumalize tofauti za kisiasa kwa mazungumzo tupate suluhu tuheshimu katika ya chama chetu na nimekuwa nikimuita Maalim Seif aje ofisi bugurudi aweze kuzungumza afanye kazi zake kama katibu mkuu na mimi nimemfahamu Maalim Seif mwaka 1973 tukiwa wanafunzi wa chuo kikuu Dar es Salaam kwahiyo hatuna sababu ya sisi kuwa na mgogoro huu na kuuruhusu kuendelea”

“Hivi sasa kupitia taarifa zetu za kiuchunguzi zinaonesha kwamba kuna mbinu ya kutaka chama hiki kiweze kufutwa kwa hiyo kuna matukio yanapangwa nje ya chama ili paweze kutokea vurugu na zikishatokea waseme chama hiki hakifai kuendelea kuwa chama cha siasa na utakuta kuna vyama vingine vya siasa vinashabikia na kutoa wito ili chama hiki kiweze kufutwa” Prof. Lipumba

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527