MAHAKAMA KUU KANDA YA SHINYANGA KUIBUKA NA KOMPYUTA KWA KILA HAKIMU ACHAPE NAKALA ZA HUKUMU MWENYEWE


Jaji mfawidhi wa mahakama kuu ya Tanzania kanda ya Shinyanga Richard Kibela akizungumza wakati wa maadhimisho ya siku ya sheria nchini-picha na Kadama Malunde-Malunde1 blog
******

Katika kuendana na kasi ya ulimwengu wa sayansi na teknolojia Mahakama kuu ya Tanzania kanda ya Shinyanga inatarajia kuanzisha mpango wa kuhakikisha kila hakimu anakuwa na komputa mpakato ili kila hakimu achape hukumu yake mwenyewe.

Hayo yamesemwa mwishoni mwa wiki iliyopita na Jaji Mfawidhi wa Mahakama kuu ya Tanzania kanda ya Shinyanga Richard Kibela wakati wa maadhimisho ya siku ya sheria nchini iliyofanyika katika viwanja vya mahakama hiyo mjini Shinyanga.

Jaji Kibela alisema katika kuendana na kasi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) mahakama hiyo inataka kuhakikisha kuwa wananchi wanapata huduma zinazotolewa na mahakama hiyo kwa wakati ili wapate muda wa kufanya shughuli zingine za maendeleo ili kukuza uchumi wa nchi.

“Katika matumizi ya TEHAMA mahakama yetu ina mpango wa kila hakimu awe na kompyuta mpakato ili kila hakimu aweze kuchapa hukumu yake mwenyewe ili kuongeza kasi ya nakala za hukumu kutolewa ndani ya siku 21.

Katika hatua nyingine Jaji Kibela alisema katika kipindi cha mwaka 2016 mahakama hiyo iliamua jumla ya mashauri 392 yakiwa ni kati ya mashauri yaliyokuwa yamefunguliwa na yake yaliyobaki mwaka 2015 ambayo kwa ujumla yalikuwa mashauri 1087.

“Kesi nyingi zimerithiwa kutoka mahakama kuu ya Tanzania kanda ya Tabora kabla ya kuanzisha kanda hii mwaka 2015 na pia baadhi ya majaji wamekuwa na majukumu mengine ya kikazi nje ya kanda.

Naye Kaimu mwenyekiti wa Chama cha Mawakili wa Kujitegemea mkoa wa Shinyanga Paul Kaunda alisema nakala za hukumu hazichapwi kwa wakati n ahata zikichapwa mahakimu wamekuwa wakitumia muda mrefu kuzifanyia uhakiki hivyo kuchelewesha azma na haki yam kata rufaa katika mahakama za juu.

Aidha alisema pia ucheleweshaji wa utoaji haki kwa wakati unasababishwa na mahakama kuwa na mahakimu wachache kukabiliana na mashuri yanayofunguliwa kila siku.

Kaunda alilitupia lawama jeshi la polisi kwa kuwashikilia watuhumiwa kituoni kwa zaidi ya saa 24 tangu mtuhumiwa akamatwe.

“Kifungu cha 32 na 33 cha sharia ya mwenendo wa makosa ya jinai kinawataka polisi wawe wamemfikisha mahakamani mtuhumiwa wa makosa ya jinai ndani ya masaa 24 lakini cha ajabu mamlaka ya jeshi la polisi imekuwa ikifanya kinyume na matakwa ya sheeria kwa sababu wanazozijua wenyewe”,alisema.

Naye mgeni rasmi katika maadhimisho hayo mkuu wa wilaya ya Kahama Fadhili Nkurlu aliyemwakilisha mkuu wa mkoa wa Shinyanga aliwataka baadhi ya watu wanaosema mahakama inaingiliwa na katika majukumu wapuuzwe.

“Mahakama zetu ziko huru,naombeni muwapuuze watu wanaosema kwamba mahakama zinaingiliwa,nawaomba pia majaji na mahakimu mtoe haki kwa wakati kwani tunataka Tanzania mpya yenye haki,sisi tunaposema hapa kazi tu,basi nyie semeni hapa haki tu”,alisema Nkurlu.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527