RAIS SHEN AAGIZA SOMO LA UJASIRIAMALI KUFUNDISHWA SHULE ZA SEKONDARI ZANZBAR


Rais wa Zanzibar, Dk Ali Mohamed Shein ameiagiza Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali kuongeza kasi ya kubadili mitaala katika shule za sekondari na kuingiza somo la ujasiriamali kwa lengo la kuwaandaa wanafunzi kwa maisha ya kujiajiri. 
Pia, alisema Serikali itaimarisha vyuo vya amali ili somo la ujasiriamali liweze kuchukua nafasi katika mitaala na kuhakikisha wanafunzi wanapomaliza masomo watoke wakiwa na uelewa mzuri wa namna ya kujiajiri. 
Akizungumza katika kongamano la siku mbili na maonyesho ya wajasiriamali linalofanyika katika ukumbi wa Baraza la Wawakilishi, Kikwajuni mjini Unguja, alisema utaratibu huo utawapa elimu itakayowasaidia kujiajiri watakapokuwa wamemaliza masomo. 
Dk Shein aliwakumbusha vijana kuwa elimu waliyoipata katika vyuo vikuu na taasisi mbalimbali zinazotoa mafunzo ya kazi na ufundi, wachukulie ni mtaji muhimu katika kuendeleza shughuli za ujasiriamali. 
Hivyo, aliwataka wasijenge dhana kuwa ujasiriamali ni kufanya biashara ndogondogo za bidhaa zinazoonekana katika masoko, lakini wajifunze kutokana na uzoefu wa nchi mbalimbali hasa India ambapo vijana wengi waliosoma wamekuwa wakijiajiri baada ya kumaliza masomo yao. 
Alisisitiza kuwa Serikali inatambua umuhimu wa kuwaendeleza wajasiriamali katika kuyafikia malengo ya kupambana na umaskini wa kipato na kupunguza tatizo la ajira, hasa miongoni mwa wanawake na vijana. 
Dk Shein alitumia fursa hiyo kueleza mafanikio ya Mfuko wa Uwezeshaji ambao katika kipindi cha miaka miwili tangu ulipoanza umetoa jumla ya mikopo 998 yenye jumla ya Sh1.6 bilioni, kwa visiwa vyote vya Unguja na Pemba na hadi sasa marejesho ni asilimia 96. 
Alisema taarifa zinaonesha kwamba asilimia 67 ya watu waliopewa mikopo ni vijana wenywe umri kati ya miaka 18 hadi 35, huku akiwataka wanasiasa kutowadanganya vijana kuhusiana suala la ajira kwani vijana hivi sasa hawadanganyiki. 
Waziri wa Kazi, Uwezeshaji, Wazee, Vijana, Wanawake na Watoto, Maudline Castico alisema kuwa kongamano hilo ni la kwanza la aina yake kufanyika visiwani humo na kueleza kuwa mchango wa sekta binafsi kupitia wajasiriamali wakubwa na wadogo ni muhimu ili kufikia lengo la Zanzibar kuwa na uchumi wa kati ifikapo 2020. 
Alisema kuwa kongamano hilo linatarajiwa kuhamasisha na kuwaelimisha wajasiriamali ili kuendeleza shughuli zao kwa ufanisi zaidi.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post