EWURA YARIDHIA KWA SEHEMU OMBI LA TANESCO KUPANDISHA BEI YA UMEME 2017


MAMLAKA ya Udhibiti wa huduma za Nishati na Maji, (EWURA), imetangaza ongezeko la bei ya umeme kwa asilimia 8.5%.

Kwa mujibu wa Mkurugenzi Mkuu wa EWURA, Felix Ngamlamgosi, (pichani), ongezeko hilo la bei ni kufuatia maombi ya Shirika la Umeme Nchini, (TANESCO), ambalo liliwasilisha maombi EWURA ya kutaka ongezeko la bei kwa asilimia 18.19, ifikapo Januari mwaka 2017.

Akitangaza bei hizo mpya jijini Dar es Salaam, jana Mkurugenzi Mkuu huyo wa EWURA amesema, baada ya kufanya uchambuzi wa kina, Mamlaka yake imefikia uamuzi wa kuongeza asilimia 8.5 itakayoanza kutumika Januari Mosi, 2017 kutokana na kuongezeka kwa gharama za uzalishaji wake.

Shirika la umeme Zanzibar (ZECO) ambalo linanunua umeme wa jumla kupeleka Zanzibar limeongezewa kwa asilimia 5.7% ya bei ya umeme.

Hata hivyo ongezeko hilo halitaathiri wateja wa majumbani ambao matumizi yao hayazidi uniti 75 kwa mwezi.

Kundi la TIB linalohusisha viwanda vidogo, mabango na minara ya mawasiliano litakua na tozo ya mwezi ya shilingi 5,520.

Shirika la Umeme Tanzania, (TANESCO), linaendelea kufanya maboresho ya miundombinu ya umeme na kutekeleza miradi mipya ya kuunganisha wateja ili kuboresha huduma za umeme nchini.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527