TCRA YAPIGA MARUFUKU UUZWAJI WA SIMU AINA SAMSUNG GALAXY NOTE 7 TANZANIA

MAMLAKA ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) imewataka wafanyabiashara wenye leseni za kuingiza simu nchini, zinazotolewa na mamlaka hiyo, kutekeleza maagizo yaliyotolewa na Kampuni ya Samsung ya kurejesha simu za kisasa za Samsung Galaxy Note 7 baada ya kubainika zina matatizo ya betri.

Akizungumza Dar es Salaam jana, Meneja Mawasiliano wa TCRA, Innocent Mungy, alisema ni vyema mawakala hao wakatekeleza maagizo hayo, kwani simu hizo ni hatari kuendelea kutumika.

Aidha Mungy aliwataka wananchi ambao tayari wanatumia simu hizo kuzizima na kuzirudisha haraka katika maduka walikozinunua ili kuepusha hatari ambayo tayari Sumsung wameshaitoa.

“Simu hiyo tayari Samsung wenyewe wamesema ina matatizo ya betri na mara mbili sasa imelipuka, hakuna faida ya mtu kuendelea kuitumia unaweza ukasababisha hatari kubwa, inapolipuka inaweza kukuondoa mikono, inaweza kulipua nyumba na matatizo mengine tunawataka wenye simu hizo kuziridisha haraka,” alisema Mungy.

Pia alisema simu hiyo haijasambaa hapa nchini, lakini kuna watu wanaweza kuwa wameletewa zawadi au mtu alisafiri na kuamua kuinunua.

“Taarifa tulizonazo haijaingia sana hapa nchini lakini wapo walioletewa kama zawadi kutoka nje ya nchi nawaomba warudishe huko kuepuka matatizo yanayoweza kujitokeza,” aliongeza Mungy.

Hivi karibuni Samsung ilitangaza kwamba haitaunda tena simu aina ya Galaxy Note 7 baada ya kutokea kwa ripoti kwamba simu ambazo kampuni hiyo iliamini ziko salama, zinawaka moto.

Kampuni hiyo ilikuwa tayari imepunguza uundaji wa simu hizo na iliwataka waliokuwa na simu hizo, kuzizima na kuacha kuzitumia huku uchunguzi ukiendelea.

Samsung iliwataka watu waliokuwa wamenunua jumla ya simu milioni 2.5 mwezi Septemba mwaka huu, kuzirejesha madukani baada ya wateja wengi kulalamika kwamba betri za simu hizo zilikuwa zinalipuka. Katika hatua nyingine, wiki iliyopita, Kampuni hiyo ya Samsung ya Korea Kusini ilitangaza kuwa imesitisha utengenezaji wa simu aina ya Galaxy Note 7.

Ilisema imefanya hivyo kutokana na madai kwamba simu mpya zilizotengenezwa hivi karibuni, kuchukua nafasi za mwanzo zilizokuwa na matatizo ya betri, nazo pia zimegundulika zina matatizo. Vyombo vya habari vya Korea Kusini, viliwanukuu maofisa wa serikali, wakisema kuwa kampuni hiyo imesitisha utengezaji wa simu hizo.

Hatua hiyo ya Kampuni ya Samsung, imechukuliwa wiki kadhaa baada ya kampuni mbili za Marekani, kusitisha uuzaji wa simu hizo. Kampuni hiyo pia ilisema itazuia usafirishaji wa simu hizo katika nchi mbalimbali duniani ili kuzifanyia ukaguzi.

Kampuni hiyo ilizirudisha simu hizo mwezi Septemba mwaka huu na kuwahakikishia wateja wake duniani kwamba simu zilizorekebishwa, zingekuwa salama.

Hata hivyo, hali imekuwa kinyume. Mashirika kadhaa ya ndege duniani, yamepiga marufuku abiria kutumia simu hizo kwenye ndege zake kutokana na matatizo kadhaa, ikiwemo kulipuka ghafla. Mathalani, Shirika la Ndege la Singapore lilitangaza wiki hii mwanzoni kuwa ni marufuku kwa abiria kubeba simu hizo na pia marufuku kuichaji kwenye ndege.

Nchi nyingine iliyopiga marufuku abiria kubeba simu hizo kwenye ndege zake ni Rwanda kwenye Shirika lake la Rwanda Air.

Nao Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Hong Kong, ulitangaza katika tovuti yake juzi kuwa kutokana na matukio ya siku za karibuni, ni marufuku kwa abiria kutumia au kuchaji simu za Samsung Galaxy Note 7 wakiwa kwenye ndege, na pia hawatakiwi kuzihifadhi katika mizigo yao.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post