Rais Magufuli Amlilia Mke wa Rais Mstaafu wa Kenya Mama Lucy Kibaki


Marehemu Lucy Kibaki akiwa na Mumewe Rais Mstaafu wa Kenya Mzee Mwai Kibaki siku ya ndoa yao mwaka 1962. 

********


 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt John Pombe Magufuli amemtumia salamu za rambirambi Rais wa Jamhuri ya Kenya mheshimiwa Uhuru Kenyatta,kufuatia kifo cha mke wa Rais Mstaafu wa Kenya mama Lucy Kibaki aliyefariki dunia leo tarehe 26 April 2016



Mama Lucy Kibaki ambaye ni mke wa Rais Mstaafu wa Kenya Mheshimiwa Mwai Kibaki amefariki dunia jijini London nchini uingereza ambako alikuwa akipatiwa matibabu.


Katika salamu hizo,Rais Magufuli ameeleza kushtushwa na kifo hicho na kuongeza kuwa Kenya imempoteza mtu mhimu aliyetoa mchango mkubwa katika maendeleo ya nchi yake.


"Kupitia kwako Rais wa Jamhuri ya Kenya mheshimiwa Uhuru Kenyatta napenda kumpa pole nyingi Rais Mstaafu wa Kenya Mheshimiwa Mwai Kibaki,Familia yake,ndugu,jamaa na marafiki wote walioguswa na msiba huu mkubwa." Amesema Rais Magufuli.


Dkt John Pombe Magufuli pia amemuombea marehemu Lucy Kibaki apumzishwe mahali pema peponi,Amina.


Gerson Msigwa
Kaimu Mkurugenzi wa Mawasiliano,IKULU
Dar es salaam
April 26,2016

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527