Picha 36!! MKUTANO WA CHADEMA LEO MJINI SHINYANGA,MAFURIKO YA HATARI,MAELFU WAJITOKEZA



Hapa ni katika viwanja vya Jeshi la zimamoto na uokoaji mjini Shinyanga ambapo leo jioni April 10,2016 kumefanyika mkutano mkubwa wa Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) ukiongozwa na naibu katibu mkuu wa Chadema Salum Mwalimu,mjumbe wa baraza kuu Chadema taifa Joseph Kasambala na mwenyekiti wa baraza la vijana Chadema taifa Patrobas Katambi aliyekuwa mgombea ubunge jimbo la Shinyanga mjini katika uchaguzi mkuu  Oktoba mwaka 2015.

Mkutano huo uliohudhuriwa na maelfu ya wakazi wa Shinyanga ulikuwa na lengo la kuwashukuru wananchi kwa kuchagua wagombea wa Chadema/UKAWA katika uchaguzi mkuu uliopita (2015) na kueleza mwelekeo wa chama hicho katika mambo mbalimbali yanayoendelea nchini Tanzania.Mwandishi mkuu wa Malunde1 blog,ndugu Kadama Malunde alikuwepo eneo la tukio,ametusogezea picha 36 ,fuatilia hapa chini kuanzia mwanzo mpaka mwisho




Baadhi ya viongozi wa Chadema wakiwa jukwaa kuu



Wakazi wa Shinyanga wakiwa katika mkutano huo



Mwenyekiti wa Chadema wilaya ya Shinyanga mjini Titus Jilungu akifungua mkutano huo ambazo umehudhuriwa na maelfu ya wakazi wa Shinyanga kinyume na ilivyotarajiwa na wananchi wengi kwani kumekuwa na mtazamo kuwa chama hicho sasa kimekosa nguvu na hakina tena wafuasi wengi kutokana na kazi ya kutumbua majipu inayofanywa na serikali ya awamu ya tano chini ya rais John Pombe Magufuli



Wakazi wa Shinyanga wakiwa katika mkutano huo



Katibu wa Chadema mkoa wa Shinyanga Zacharia Obadi akizungumza katika mkutano huo ambapo aliwashukuru wakazi wa Shinyanga kujitokeza kwa wingi katika uchaguzi mkuu uliopita kuchagua viongozi wa Chadema na kuongeza kuwa pamoja na kwamba aliyekuwa mgombea urais kupitia chama hicho Edward Lowassa kuibiwa kura kamwe chama hicho hakipo tayari kuona amani ya nchi inatoweka na badala yake Chadema itafika ikulu kwa kura za wananchi siyo kwa kumwaga damu ya watanzania



Wakazi wa Shinyanga wakifurahia jambo katika mkutano huo



Mjumbe wa baraza kuu Chadema taifa Joseph Kasambala akiwahutubia wakazi wa Shinyanga,ambapo aliwaomba watanzania kuendelea kuiamini Chadema kwani ndiyo chama pekee chenye kuleta mabadiliko ya kweli badala ya viongozi wa CCM ambao wanafanya mambo kwa kuiga sera za Chadema.



Kada wa Chadema aliyenyoa kuduku na mtoto wake wakiwa katika mkutano huo



Kasambala aliwataka wakazi wa Shinyanga kubadilika na kuepuka kuchagua viongozi wasiokuwa na msaada kwa wananchi akitolea mfano wa mbunge wa jimbo la Shinyanga mjini Stephen Masele ambaye hajaonekana katika jimbo lake tangu uchaguzi umalizike hata kwa ajili tu ya kuwashukuru wapiga kura wake



Kasambala alisema lengo la mkutano huo ni kuwashukuru wakazi wa Shinyanga kwa kuchagua wagombea wa Chadema katika uchaguzi uliopita na kuwataka madiwani wa Chadema/Ukawa kuchapa kazi kwa kuwatumikia wananchi badala ya kubweteka kama madiwani wa CCM



Tunamsikiliza Kasambala.....



Kasambala Chadema/Ukawa wamejipanga kufanya mikutano kata moja baada ya nyingine kuwafikia wapiga kura wao



Tunamsikiliza Kasambala....



Kasambala alitumia fursa hiyo kumuomba aliyekuwa mgombea ubunge wa jimbo la Shinyanga Patrobas Katambi aliyechakachuliwa matokeo ya ubunge kuwa mvumilivu na kwamba mwaka 2020 lazima Chadema ichukue jimbo la Shinyanga mjini



Wananchi wakionesha alama ya kobra kama walivyoelekezwa na Kasambala



Alama ya kobra....



Naibu katibu mkuu wa Chadema Salum Mwalimu akiwa na aliyekuwa mgombea ubunge jimbo la Shinyanga mjini Patrobas Katambi jukwaani



Mwenyekiti wa Baraza la vijana Chadema taifa Patrobas Katambi,aliyekuwa mgombea ubunge katika jimbo la Shinyanga mjini katika uchaguzi uliopita akiwashukuru wananchi wa mkoa wa Shinyanga kwa kumpigia kura katika uchaguzi huo



Katambi amesema pamoja na kuhujumiwa ubunge ataendelea kuwatumikia wakazi wa Shinyanga kwa kufichua maovu yote yanayofanywa na viongozi wa CCM na serikali kwa ujumla kwani nia yake ni kuona watanzania wanaishi mazuri.Katambi amewashukuru wananchi wote waliompigia kura na ambao hawakumpigia kura kwa hayo ndiyo mambo ya demokrasia



Tunamsikiliza Katambi.....



Katambi amesema wakazi wa Shinyanga bado wanaendelea kuishi maisha magumu kutokana na kuongozwa na viongozi wasiokuwa wazalendo,akitolea mfano wa mbunge wa jimbo hilo Stephen Masele ambaye hajafanya jambo lolote tangu uchaguzi umalizike na haonekani hata kwenye jimbo lake kutatua kero na hata kuwashukuru tu wapiga kura wake



Tunamsikiliza Katambi wetu...



Mwenyekiti huyo wa BAVICHA Patrobas Katambi alitumia fursa hiyo kuukosoa uongozi wa wa serikali iliyopo madarakani kwa kupuuza wafadhili kutoka nje ya nchi na kusisitiza kuwa Tanzania bado haijafikia hatua ya kujitegemea kiuchumi hivyo inahitaji ushirikiano zaidi kutoka nje ya nchi.Amesema Tanzania inanyimwa misaada na nchi za nje kutokana na kuminya demokrasia



Viongozi mbalimbali wa Chadema na wananchi wakiwa eneo la mkutano huo


Mkutano unaendelea....



Wakazi wa Shinyanga wakiwa na baiskeli zao kwenye mkutano...



Patrobas Katambi ametumia fursa hiyo kumkaribisha mkuu mpya wa mkoa wa Shinyanga Anne Kilango Malecela na kumtaka kuwatumikiwa wakazi wa Shinyanga bila kuwabagua na kama ataenda kinyume basi Chadema hawatasita kuchukua hatua dhidi yake kwani sasa kinachotakiwa ni kuchapa kazi



Mkutano unaendelea



Naibu katibu mkuu wa Chadema Salum Mwalimu akiwahutubia wakazi wa Shinyanga ambapo pamoja na kuwashukuru kuwapigia kura wagombea wa Chadema/Ukawa amewatahadhalisha watanzania kutoshabikia utumbuaji majipu unaoendelea kwani ni kauli inayolenga kuwaaminisha wananchi kuwa serikali inafanya kazi vizuri watanzania bado wanaendelea kuishi maisha magumu



Wakazi wa Shinyanga wakiwa kwenye mkutano na Kahawa yao...



Mwalimu amewataka watanzania kuendelea kuunga mkono Ukawa/Chadema na kutokatishwa tamaa na matokeo ya uchaguzi kwani dunia nzima inatambua kuwa mgombea urais kupitia Ukawa Edward Lowassa ndiyo mshindi katika uchaguzi huo



Mwalimu ameongeza kuwa Chadema ni mpango wa mungu na wataingia ikulu kwa njia ya amani siyo kumwaga damu na wanaodai kuwa Chadema itakufa wanajidanganya kwani ni chama imara na wanachofanya sasa ni kuisoma serikali ya Magufuli akidai kuwa wanachofanya CCM ni Ngoma ya watoto ambayo siku zote huwa haikeshi



Mkutano unaendelea...



Mwalimu amesema viongozi wa serikali wengi sasa wanakurupuka kila mmoja anataka sifa kuwa mtumbuaji majipu na kuongeza kuwa wakati mwingine ziara hizo za kushtukiza zinakuwa kwa ajili ya kulipiza visasi kwa watu wasio na hatia



Mwalimu amesema mkutano uliofanyika leo Shinyanga ni kama salamu tu na wanajiandaa kufanya mkutano mkubwa zaidi huku akitumia fursa hiyo kupongeza hotuba ya aliyekuwa mgombea urais wa Zanzibar Maalim Seif aliyoitoa leo...isome <<HAPA>>

Picha zote na Kadama Malunde-Malunde1 blog

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post