KUHUSU MWANAMKE ALIYEKUTWA JUU YA PAA LA JENGO LA WIZARA YA FEDHA NA KUANZA KUPIGA KELELE

 

Katika hali isiyokuwa ya kawaida, mwanamke mmoja amepanda katika paa la jengo la Wizara ya Fedha na Mipango huku tukio hilo likizua sintofahamu kwa wafanyakazi wa wizara hiyo na wapita njia.




Tukio hilo lilitokea jana Dar es Salaam majira ya asubuhi ambapo mwanamke huyo anayedaiwa kuwa raia wa Kenya alipanda juu ya paa hilo na kuanza kupiga kelele. 


Katika tukio hilo, inadaiwa mwanamke huyo aliwasili katika eneo hilo la wizara akionekana kama mmoja wa wananchi ambao walikwenda kwa ajili ya kupatiwa huduma, lakini baada ya muda alionekana akiwa juu ya paa huku akipiga kelele. 


Mwanamke huyo aliyekuwa amebeba mkoba, ambaye haikufahamika mara moja nia yake ya kupanda juu ya paa hilo, ilimchukua saa kadhaa akiwa juu na pale walinzi wanaolinda ofisi za wizara hiyo walipokwenda katika eneo hilo na kumwomba ateremke aligoma. 


Hata hivyo hali hiyo ilionekana kutowakatisha tamaa walinzi hao wanaolinda majengo ya Wizara ya Fedha na Mipango yaliyopo mita chache kutoka Ikulu ya Dar e Salaam, ambao walikwenda tena wakiwa na ngazi na kuanza kumbembeleza ambapo jaribio hilo lilifanikiwa na mwanamke huyo kuteremka. 


Wakati mwanamke huyo akiwa juu ya paa, wananchi waliokuwa chini walianza kumuuliza maswali, lakini hakusikika majibu yake kutokana na kelele za watu ambao kila mmoja aliimuuliza swali lake.


Hata hivyo mmoja wa askari wa kikosi cha Usalama Barabarani ambaye alisogea kwa karibu kumuuliza mwanamke huyo, alisema kuwa alimwambia amechukua uamuzi huo kutokana na kuteswa na askari nchini Kenya. 


“Tukio hili ni la ajabu na linaibua maswali… hivi inakuwaje kwa jengo kama hili la wizara ambalo lipo jirani na Ikulu mtu anapanda juu na walinzi wapo? 


“Hii inasikitisha sana na ni ajabu kwa kweli, ipo siku tutakuta watu wanaingia Ikulu na kufanya mambo ya ajabu kwa viongozi wetu,” alisema mmoja wa wananchi waliokuwa katika eneo hilo ambaye hakupenda kutajwa jina lake gazetini. 


Alipotafutwa Msemaji wa wizara hiyo, Ingiahedi Mduma ili kuzungumzia suala hilo, alisema kwa sasa yupo mjini Dodoma katika maandalizi ya vikao vya Bunge na hana taarifa ya tukio hilo. 




 

Mwanamke huyo akizungumza na watu waliokusanyika lakini alikuwa hasikiki vizuri maneno aliyokua akiongea kutokana na wananchi waliokusanyika kumuuliza maswali mengi kwa wakati mmoja. 

 

Polisi akiwa pembeni ya uzio wa majengo ya wizara ya fedha na mipango mara baada ya mwanamke huyo kuwa juu ya paa la nyumba hizo. Baada ya muda wafanyakazi wa wizara hiyo walimwekea ngazi na kumshusha ili kumhoji zaidi nini kimemfanya apande juu ya paa la majengo hayo.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527