HII HAPA TAARIFA YA CHADEMA KWA VYOMBO VYA HABARI KUHUSU BANGO LA CCM LILILOZUA BALAA





CHAMA CHA DEMOKRASIA NA MAENDELEO (CHADEMA)

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI



Katika hali isiyokuwa ya kawaida ambayo kwa namna yoyote haiwezi isingeachwa imee katika fikra za watu achilia mbali kuachiwa itembezwe hadharani, Chama Cha Mapinduzi (CCM) kupitia katika mojawapo ya mabango yaliyobebwa na wanachama wake kuiadhimisha Sikukuu ya Mapinduzi ya Zanzibar, imedhihirisha kuwa inakumbatia fikra hatari za kikaburu.

Kupitia bango hilo ambalo kwa namna lilivyotengenezwa na lilivyobebwa ni vigumu kuamini kuwa liliibuka ghafla kama vile kitambaa cha mfukoni, mwanachama wa CCM akiwa amesindikizwa na wenzake, waliopita mlangoni mwa Uwanja wa Amani bila kuzuiliwa, kukemewa wala kubugudhiwa, ujumbe hatari wa kibaguzi umeandikwa 'MACHOTARA HIZBU ZANZIBAR NI NCHI YA WAAFRIKA'. Hizi ni fikra za kikaburu. Ni ishara ya mbegu za kibaguzi zilizokomaa na sasa zinachipua.

Kwa wafuatiliaji wa masuala ya kisiasa nchini na kipekee katika muktadha huu, siasa za Zanzibar wataelewa kuwa kauli iliyotolewa katika bango hilo, si ya bahati mbaya. Ni matokeo ya siasa za chuki zinazopaliliwa, kusimamiwa, kuratibiwa na hata kunyamaziwa na uongozi wa juu kabisa wa CCM.

Tutatoa mfano. Moja ya maskani maarufu za masuala ya kisiasa Visiwani Zanzibar inayomilikiwa na CCM iitwayo Kisonge imekuwa na kawaida ya kuandika lugha hatari zinazoashiria ubaguzi ulio wazi kabisa ulio na maudhui sawa sawa na huu uliotolewa leo kwenye Sikukuu ya Mapinduzi.

Mojawapo ya kauli ambazo ziliandikwa katika ubao ulioko katika maskani hiyo hivi karibuni wakati wa joto la Uchaguzi Mkuu uliopita, iliandikwa hivi "Katiba ni ya Unguja na nyinyi Wapemba mwende mkatengeze yenu Pemba."

Lugha hiyo na nyingine za namna hiyo kama ilivyotokea leo, zimekuwa zikitolewa mbele ya viongozi wa CCM au wanaziona lakini kwa sababu wanazozijua wao, pengine zinawasaidia katika kufikia malengo ya siasa hatarishi zinazokiuka misingi yote ya demokrasia, zimekuwa zikifumbiwa macho na kuzidi kumea vichwani mwa wanachama wao na kuleta mpasuko wa ubaguzi wa itikadi za kisiasa, rangi, kanda, kabila na hata dini, si Zanzibar pekee bali nchi nzima.

Kilichotokea leo Zanzibar, ni mwendelezo usiokuwa wa bahati mbaya bali maelekezo ya kimkakati ya kueneza propaganda za chuki miongoni mwa Watanzania ambayo ndiyo imebakia kuwa silaha pekee ya kuibeba CCM ikiwa ni dalili ya wazi ya chama kilichofilisika sera, kuacha misingi yake, kuishiwa ushawishi wa hoja na kukosa uhalali wa kisiasa hivyo kujihalalisha kwa ubaguzi kama huo.

Ni mwendelezo wa kauli za viongozi wakuu wa chama hicho ambazo hutolewa hadharani kwenye majukwaa ya siasa, wakiwabagua wanachama, wapenzi, wafuasi wa vyama vingine kuwa ni wa dini fulani, kanda fulani au kabila fulani. Wakijua kabisa hakuna kikundi chochote cha kisiasa chenye sifa hizo kwa sababu ni kinyume cha sheria na misingi ya taifa letu.

Ni mwendelezo wa kauli iliyowahi kutolewa na viongozi wa chama hicho dhidi ya viongozi wenzao na wala viongozi wakuu wa CCM hawakuthubutu hata kukaripia, tena yakiwa maazimio rasmi ya kikao kwamba "Rais wa Tanzania hawezi kutoka Kaskazini".

Kauli hiyo iliyotolewa baada ya kikao ilikuwa kauli ya kikaburu sawa sawa kabisa na ile iliyotolewa leo huko Zanzibar.

Mwalimu Nyerere, Baba wa Taifa aliwahi kusema ukaburu si rangi, ni fikra.

CHADEMA tunalaani na kupinga kwa nguvu zote mipango, mikakati, tabia na chembechembe za ubaguzi wa aina yoyote, ukiwemo huu wa kisiasa ambao sasa unaanza kusakafiwa kwa ubaguzi wa rangi kwa sababu tunaamini wanaobeba agenda hii hawataishia hapo bali watazidi kutugawa Watanzania pia kwa ubaguzi wa ukanda, ukabila na udini kama ambavyo wamekuwa wakijaribu kuchochea.

CHADEMA kwa kusimamia misingi yake na kuzingatia kikamilifu misingi ya taifa letu hasa haki, uadilifu, utu, umoja na uzalendo, haiko tayari kuona taifa likifikishwa huko na kuhatarisha maisha ya jamii nzima ya Watanzania kwa sababu ya maslahi ya kikundi cha watu wachache.

Tunamkumbusha Mkuu wa Jeshi la Polisi (IGP) Ernest Mangu kuwa kauli za namna hii ambazo zimekuwa zikipaliliwa na viongozi wa CCM na wengine wakitumia nafasi za kiserikali kuchochea ubaguzi ambao ni hatari kwa amani ya nchi na usalama wa raia na mali zao, ni ushahidi wa wazi kwa ajili ya hatua za kisheria badala ya jeshi hilo kujikita katika kubambikia wanachama, wafuasi na wapenzi wa vyama vya upinzani, hususan UKAWA tuhuma na kesi zisizokuwa msingi wowote kwa maslahi tu ya kisiasa kuisaidia CCM.

Wakati tukimtaka Rais John Magufuli kutimiza kwa vitendo kauli yake ya kwamba Serikali yake haitawabagua watu kwa misingi ya kisiasa (huku Waziri Mkuu wake akitoa maagizo kinyume kabisa na kauli hiyo) tunakitaka CCM, kupitia kwa Mwenyekiti wake, Jakaya Kikwete kama hakiko nyuma ya agenda hizo za kibaguzi na fikra hizo za kikaburu, kichukue hatua za haraka mara moja kuwawajibisha viongozi wake waliosimamia na kuachia jambo lililotokea leo huko Zanzibar.

Imetolewa leo Jumanne, Januari 12, 2016 na;

Tumaini Makene

Mkuu wa Idara ya Mawasiliano na Habari
CHADEMA
 *******************************
Hata hivyo taarifa ya Chadema imekuja ikiwa tayari CCM Wakiwa wameomba radhi kutokana na kitendo hicho>>>ANGALIA BANGO HILO NA KAULI YA CCM KUHUSU BANGO HILO

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post