NYUMBA 100 ZAWEKWA ALAMA X DAR, WANANCHI WAGOMA,VURUGU YATOKEA




Zoezi la uwekaji alama nyekundu katika zaidi ya nyumba 100 zinazotakiwa kubomolewa kwenye bonde la Mto Msimbazi, Jangwani limemalizika chini ya ulinzi mkali wa polisi baada ya vurugu za wananchi kuigomea serikali katika zoezi hilo.

Zoezi hilo lililoanza leo majira ya saa nne asubuhi likiongozwa na Mwanasheria wa NEMC, Machare Heche lilisababisha vurugu zilizotokana na wananchi kukataa kuwekewa alama hizo huku wakidai kuwa zoezi hilo alikustahili kufanyika kutokana na kusimamishwa kwa zoezi hilo hadi Januari mosi mwakani.

Alipohitajika kuzungumzia zoezi hilo kwakuwa alikuwepo wakati tukio zima hadi kumalizika kwake, Heche aligoma kuzungumzia zoezi hilo kwa kudai kuwa mzungumzaji mkuu ni Waziri anayehusika na Mazingira, January Makamba au Mkurugenzi wa NEMC.

Miongoni mwa malalamiko ya wananchi waishio katika bonde hilo ni kutaka jengo la Stendi ya mabasi yaendayo haraka pia liwekewe alama na hatimaye kubomolewa kwa sababu ya kuwa jengo hilo lipo bondeni sawa na nyumba zao,

Aidha wameiomba serikali kuongeza siku zaidi za maandalizi ili waweze kuhamisha vitu vya majumbani kwani muda uliotolewa hautoshi kufanya maandalizi.

Ikumbukwe kuwa zoezi la kubomoa nyumba zilizopo mabondeni lilianza Desemba 17 mwaka huu na kusitishwa baada ya siku tatu na Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, William Lukuvi hadi Januari 5 kwa kigezo cha kutoa nafasi kwa watu waliojenga katika maeneo hayo kuondoa wenyewe mali zao .

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527