MAALIM SEIF ATOA SAA 48 URAIS ZANZIBAR!! "CHAGUZI NNE NIMEIBIWA MATOKEO...SAFARI HII SIKUBALI..SIKUBALI...SIKUBALI..


Mgombea urais wa Zanzibar kupitia Chama cha Wananchi (Cuf), Maalim Seif Sharif Hamad akitoa msimamo wa chama chake baada ya Tume ya Uchaguzi Zanzibar (Zec) kufuta matokeo ya uchaguzi.



Sakata la kufutwa kwa uchaguzi visiwani Zanzibar limechukua sura mpya baada ya mgombea urais kwa tiketi ya Chama cha Wananchi (CUF), Maalim Seif Shariff Hamad, kusema hatakubali kuporwa ushindi wake.

Mgombea huyo ambaye pia ni Makamu wa Kwanza wa Rais katika Serikali ya Umoja wa Kitaifa visiwani humo, pia ameitaka Tume ya Uchaguzi Zanzibar (ZEC) kuendelea na mchakato wa kuhesabu kura katika majimbo yaliyobaki ili kumtangaza mshindi.

Kadhalika, Maalim Seif ameonya kuwa kufikia kesho (Novemba Mosi, 2015), endapo Mwenyekiti wa ZEC, Jecha Salim Jecha, ataendelea na msimamo wake wa kuufuta uchaguzi huo na kupuuza maamuzi ya wananchi kupitia sanduku la kura, yeye na viongozi wenzake wa CUF watajiweka kando katika kuwazuia (wananchi) wasiendelee na hatua ya kudai haki yao ya kidemokrasia kwa njia za amani.

Chaguzi nne nimeibiwa matokeo. Kama Dk. Shein ameamua kung’ang’ania madaraka safari hii... sikubali, sikubali sikubali, alisema Maalim Seif ambaye pia ni Makamu wa Kwanza wa Rais katika Serikali ya Umoja wa Kitaifa iliyotarajiwa kumaliza muda wake baada ya rais mpya kupatikana kutokana na Uchaguzi Mkuu uliofanyika Jumapili iliyopita.

Akizungumza na waandishi wa habari kwenye Makao Makuu ya CUF, Mtendeni mjini Zanzibar jana, Maalim Seif alisema ifikapo Novemba Mosi (kesho Jumapili), wananchi wataanza kudai haki yao ya kidemokrasia kupinga uamuzi wa ZEC kufuta matokeo ya Uchaguzi Mkuu uliofanyika Jumapili.

Aliyasema hayo akiwa na mwenyekiti wake wa kampeni, Nassor Ahmed Mazrui, na pia msaidizi wake, waziri wa zamani wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ), Mansoor Yussuf Himid.
Kwa mujibu wa Katiba ya Zanzibar ya mwaka 1984, kifungu cha 28(2), baada ya tarehe 2 Novemba 2015, Zanzibar haitakuwa na rais wala baraza la wawakilishi na haitakuwa na serikali wala mawaziri, makamu wa kwanza wala makamu wa pili wa rais wa Zanzibar, alisema.

Alisema kimsingi, Zanzibar itakuwa imeingia katika mgogoro mkubwa wa kikatiba na kisheria kutokana na uamuzi wa Mwenyekiti wa Zec, Salim Jecha, wa kufuta matokeo ya uchaguzi bila ya kuwashirikisha viongozi wenzake wa ZEC kinyume cha Katiba.

Alisema kwa mujibu wa katiba, ukomo wa uongozi wa Rais Dk. Ali Mohamed Shein na serikali yake ni Novemba 2, mwaka huu, na anatakiwa kuapishwa rais mpya pamoja na wajumbe wapya wa Baraza la Wawakilishi visiwani humo.

ASHANGAA VIFARU KUJAZWA ZANZIBAR

Alisema tangu kufutwa kwa matokeo, yeye amekuwa akichukua juhudi za kutafuta ufumbuzi kwa kukaribisha mazungumzo na viongozi wenzake wa kitaifa akiwamo Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Jakaya Kikwete na pia Rais wa Zanzibar, Dk. Shein, lakini wamekuwa wakimpiga chenga.
Alisema baada ya uchaguzi kufutwa, alianza kuwatafuta kwa kutumia mawasiliano ya simu na ujumbe kupitia wasaidizi wao, akitaka wakutane lakini hadi sasa ameshindwa kuwapata.
Tumeshatoa nafasi ya kutosha ya kutafuta ufumbuzi wa suala hili kwa njia za mazungumzo lakini viongozi wa CCM wanaonekana hawataki ufumbuzi,î alisema.

“Badala yake tunashuhudia Rais Kikwete akituletea majeshi na vifaru Zanzibar wakati wananchi wa Zanzibar wametulia wakitekeleza wito wetu wa kuwataka watunze amani ili kutupa nafasi viongozi wao kutafuta ufumbuzi, alisema Maalim Seif.
Maalim Seif alisema pamoja na yote, CUF inaendelea na juhudi za kufanya mazungumzo kwa kushirikiana na Jumuiya za Kimataifa ili kuhakikisha viongozi wa Zec wanarudi kazini kumalizia kazi ya kufanya uhakiki na majumuisho katika majimbo 14 yaliyobakia kati ya 54 na kumtangaza mshindi badala ya kuitisha uchaguzi mpya Zanzibar.

Iwapo hadi tarehe Mosi, Novemba 2015, hatutaona hatua zozote za maana zikichukuliwa kukamilisha uchaguzi huu na kuheshimu maamuzi ya Wazanzibari waliyoyafanya Oktoba 25, 2015, mimi na viongozi wenzangu wa CUF tutaondoa mikono yetu na kuwaachia wananchi wenyewe wa Zanzibar watafute haki yao kwa njia ya amani, alisema Maalim Seif aliyekuwa amefuatana pia na Waziri wa Katiba na Sheria wa Zanzibar, Abubakar Khamis Bakari.
Aidha, alisema CUF inaamini kuwa Watanzania wote na wapenda haki na amani na Jumuiya za Kimataifa, watawaunga mkono Wazanzibari katika kutafuta haki yao ya Kidemokrasia.

Alisema waangalizi wa ndani na wa kimataifa, wakiwamo Umoja wa Ulaya (EU), Jumuiya ya Madola Umoja wa Afrika (AU), Jumuiya ya Maendeleo ya Nchi za Kusini mwa Afrika (SADC), Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC), waangalizi wa Marekani na Uingereza, katika ripoti zao wamesema uchaguzi wa Zanzibar mwaka huu ulikuwa huru na wa haki.
Alisema Mwenyekiti wa ZEC (Jecha) amefanya kitendo cha ubabe kwa kufuta uchaguzi baada ya kuona mwelekeo mbaya wa matokeo ya uchaguzi huo kwa mgombea wa chama tawala -- Chama Cha Mapinduzi (CCM), Dk. Shein.

MSAIDIZI WA MWANASHERIA MKUU

Alipoulizwa kuhusiana na madai ya Maalim Seif kuwa baada ya Novemba 2 Zanzibar haitakuwa na rais, kwa mujibu wa Katiba ya Zanzibar ya mwaka 1984, kifungu cha 28(2) inayoeleza ukomo wa muda wa kuwa madarakani kwa rais na serikali yake, Msaidizi wa Mwanasheria Mkuu wa Zanzibar , Amisa Mmanga hakuwa tayari kutoa ufafanuzi kwa madai kuwa msemaji wa jambo hilo ni Mwanasheria Mkuu ambaye hivi sasa yuko safarini nje ya nchi.

Alisema kwa kuwa mkuu wake (Mwanasheria Mkuu) amesafiri nje ya nchi, hawezi kutoa ufafanuzi kwa jambo lolote kwani ni lazima kwanza apate baraka zake.

Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais, Mohamed Aboud, alipoulizwa kuhusiana na suala hilo, alisema bado ni mapema kwa serikali kutoa msimamo wake kuhusu kauli ya Maalim Seif , hasa ya kuamua kurejesha ajenda ya kufutwa matokeo kwa wananchi wa Zanzibar.

Sina cha kuzungumza serikali itatoa taarifa maalum wakati ukifika kwa kila jambo linalojitokeza sasa baada ya kufutwa kwa matokeo ya uchaguzi, alisema Waziri Aboud ambaye pia ndiye Msemaji Mkuu wa Serikali ya Umoja wa Kitaifa Zanzibar.
Matokeo ya Uchaguzi Mkuu wa Zanzibar yalifutwa na Mwenyekiti wa ZEC, Jecha, baada ya kutangazwa majimbo 31 kati ya 54 kwa madai kulikuwa na kasoro nyingi zinazoufanya usiwe huru na wa haki, ikiwamo kura kuongezeka katika baadhi ya majimbo kisiwani Pemba na pia baadhi ya makamishna wa ZEC kutanguliza itikadi za vyama hadi kuvua mashati ili kupigana.

Kadhalika, Mwenyekiti wa ZEC, alisema katika baadhi ya vituo, masanduku ya kupigia kura yaliporwa na kwenda kuhesabiwa nje ya vituo, kitendo ambacho ni kinyume cha sheria ya uchaguzi na pia, kuna taarifa ya kufukuzwa kwa baadhi ya mawakala wa wagombea na hivyo kushindwa kutekeleza wajibu wao.

Hata hivyo, kwa mujibu wa waangalizi wa kimataifa wakiwamo kutoka SADC, Jumuiya ya Afrika Mashariki, Jumuiya ya Madola, Umoja wa Afrika (AU) na Umoja wa Ulaya (EU), uchaguzi mkuu nchini kote ulifanyika kwa uhuru na haki na hivyo wakaitaka ZEC iendelee na mchakato wa kuhesabu kura na kumtangaza mshindi atokanaye na uamuzi wa Wazanzibari.

Kadhalika, Mwakilishi wa Umoja wa Mataifa (UN) nchini na pia balozi za mataifa mbalimbali zikiwamo za Uingereza, Ireland Kaskazini na Marekani, zimetoa taarifa ya kustushwa na uamuzi wa Mwenyekiti wa ZEC na kutaka tume hiyo iheshimu uamuzi wa Wazanzibar kwa kuendelea na mchakato wa kuhesabu kura, huku wanasiasa wote wakisisitizwa kutanguliza mbele taifa na kuhakikisha kuwa amani na utulivu vinaendelea kustawishwa visiwani humo.

CHANZO: NIPASHE

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527