Habari Mpya

6/recent/ticker-posts

BALOZI MWAPACHU NAYE AJICHOMOA CCM….KAMA KINGUNGE


Aliyewahi kuwa Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Afrika Mashariki na Kada wa Chama cha Mapinduzi (CCM), Balozi Juma Mwapachu jana ametangaza kujivua uanachama wa chama hicho kutokana na chama kupoteza dira.

Tamko la Balozi Mwapachu linasema kuwa kuanzia leo kada huyo wa CCM hatakuwa tena mwanachama wa chama hicho tawala na kuongeza kuwa bado hajaamua kujiunga na chama kingine.

‘’Kuanzia kesho( leo) mimi si mwana CCM tena. Nitarejesha rasmi kadi yangu kupitia ofisi ya CCM ya kata yangu Mikocheni, Dar es Salaam. Kwa sasa sijaamua kujiunga na chama kingine. Mwenyezi Mungu anilinde,” inasema sehemu ya tamko hilo.

Mwanasiasa huyo ambaye amekuwa ndani ya CCM kwa miaka 48 sasa amesema kuwa katika mchakato wa kumpata mgombea urais wa chama hicho, chama kilidhihirisha kutokuwa chama kinachoendeshwa kwa misingi ya demokrasia kwa kumuengua waziri mkuu wa zamani, Edward Lowassa ambaye anapendwa na wengi ndani ya chama.

Mwapachu amesema kuwa Lowassa na wanachama wengine wa CCM waliojitoa ni sahihi hivyo naye anaungana nao.

‘’Kujitoa kwake uanachama wa CCM hivi karibuni ni sahihi kabisa kwasababu CCM si chama tena cha watu. Kimetekwa, na mimi nakubaliana na msimamo wa Lowassa na hao waliyofuata kutoka ndani ya CCM,’’ alisema Mwapachu.

Mwapachu ameshika nyadhifa mbalimbali ndani ya chama hicho lakini pia amewahi kuwa Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC).

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com