HAYA NDIYO MATUKIO YALIYOTIKISA TANZANIA MWAKA 2014

MWAKA 2014 unafikia tamati leo. Kwa Watanzania, kuna matukio mbalimbali yaliyojitokeza ambayo yameacha kumbukumbu kubwa kwao. Hata hivyo, yafuatayo ndiyo mambo yaliyotia fora zaidi.
Viungo vingi vya binadamu vikiwa vimetupwa katika machimbo ya kokoto yaliyopo Bunju, Dar.

1.VIUNGO VYA BINADAMU VYASHTUA 
Jumatatu ya Julai 21, 2014, nchi ilipatwa na mshtuko mkubwa baada ya kusambaa kwa habari kuwa viungo vingi vya binadamu vilikutwa vikiwa vimetupwa katika machimbo ya kokoto yaliyopo Bunju, Kinondoni jijini Dar es Salaam.

Watu wengi waliamini viungo hivyo vimetokana na mauaji ya halaiki, hasa baada ya kukutwa kwa mabaki ya mikono, miguu, mafuvu, viganja na vingine vingi. Lakini baadaye ikaja kuthibitika kuwa viungo hivyo vilitupwa kimakosa na Chuo Kikuu cha Kimataifa cha Tiba na Teknolojia (IMTU), ambacho pia kinaendesha hospitali.
Viungo hivyo mbalimbali vya binadamu vilikuwa vikitumiwa kimasomo na madaktari wanafunzi, ambavyo vilipaswa kuteketezwa baada ya matumizi. Kitendo hicho kilisababisha serikali kukisimamisha kwa muda chuo hicho kutokana na uzembe huo. Viungo hivyo vya binadamu, hupatikana katika maiti mbalimbali zinazokosa ndugu wa kuwazika na hutolewa na hospitali ya Taifa Muhimbili.
 Kundi lililoitwa Umoja wa Katiba ya Wananchi (UKAWA),wakiongozwa na Mwenyekiti wa CUF, Profesa Ibrahim Lipumba.
2.KUZALIWA KWA UKAWA
Baada ya Rais Jakaya Kikwete kuridhia zoezi la uandikwaji wa Katiba Mpya, Tume ya kukusanya maoni chini ya uenyekiti wa Jaji Joseph Warioba ilifanya kazi yake vizuri na mwaka huu katiba hiyo ilipelekwa Bungeni ambako Bunge Maalum la Katiba lilikutana ili kupitia vifungu vyake kabla ya kuipeleka kwa wananchi kwa ajili ya kuipigia kura ya kuikubali au kuikataa.

Kulitokea malumbano makali kati ya wajumbe wa Bunge hilo juu ya vipengele kadhaa, hasa muundo wa serikali ya Jamhuri ya Muungano. Wajumbe waliotokana na Chama Cha Mapinduzi, walipendezwa na muundo wa serikali mbili kama ilivyo hivi sasa, wakati wapinzani walitaka serikali tatu.
Misimamo hiyo ilileta utengano mkali kiasi kwamba wajumbe wa upinzani wakiongozwa na Mwenyekiti wa CUF, Profesa Ibrahim Lipumba kuamua kususia vikao hivyo, wakipinga kile walichokiita uchakachuaji wa rasimu ya katiba ya Jaji Warioba. Ususiaji huo ulisababisha kuanzishwa kwa kundi lililoitwa Umoja wa Katiba ya Wananchi (UKAWA).
Jaji Warioba
Kuanzishwa kwa umoja huo uliovihusisha vyama vya Chadema, CUF, NCCR-Mageuzi na NLD, kulisababisha kundi hilo kukubaliana kusimamisha mgombea mmoja katika chaguzi zijazo, wakianzia na uchaguzi wa serikali za mitaa uliofanyika katikati ya mwezi huu.
3.JAJI WARIOBA APIGWA
Baada ya wajumbe wa Bunge Maalum la Katiba kumaliza kazi yake na kuikabidhi katiba pendekezwa kwa Rais Jakaya Kikwete tayari kwa ajili ya kuipeleka kwa wananchi ili kupigiwa kura ya maoni, kulikuwa na mkanganyiko miongoni mwa watu juu ya kilichomo ndani ya katiba hiyo, baadhi wakipinga kuondolewa kwa vifungu vingi vilivyokuwa na masilahi kwa nchi.

Miongoni mwa wanaoongoza harakati za kupinga kuondolewa kwa baadhi ya vifungu vilivyowasilishwa na Tume hiyo, ni Taasisi ya Mwalimu Julius Nyerere ambayo mara kadhaa imeandaa mijadala ya wazi, lakini wakimtumia Jaji Warioba kama msemaji wake mkuu.
Kitendo hicho kimesababisha Warioba kuonekana kama yupo katika mgogoro na chama chake na siku aliyofanyiwa fujo na kupigwa katika ukumbi wa mikutano wa Ubungo Plaza, wanaodaiwa kuwa makada wa CCM wanatajwa kuhusika.
Aliyekuwa mshindi wa miss Tanzania 2014, Sitti Mtemvu kabla ya kuvuliwa taji.
Kitendo hicho pia kilikosolewa na wachambuzi wa habari za kisiasa wakidai ulikuwa ni udhalilishwaji wa mtu aliyewahi kuwa Makamu wa Rais na Waziri Mkuu wa Tanzania na hivyo kuhoji ulinzi wake.

4.MISS TANZANIA YAFUNGIWA MIAKA 2
Shindano la Miss Tanzania limejijengea heshima kwa muda mrefu tokea lilipoanza tena mwaka 1994. Ingawa kumekuwa na malalamiko ya chinichini juu ya kuwepo kwa hila, safari hii lilijikuta likipata aibu kubwa, baada ya mshindi wake wa mwaka huu, Sitti Mtemvu kudaiwa kudanganya umri hivyo kuibua sauti zilizotaka kunyang’anywa kwa taji hilo.

Baada ya skendo hiyo kuchachamaa, Baraza la Sanaa la Taifa liliendelea na uchunguzi wake dhidi ya malalamiko mengi yaliyowahi kuripotiwa na katika tukio ambalo halikutarajiwa, shindano hilo limesimamishwa kwa miaka miwili kutofanyika na sababu nyingine iliyosababisha hatua hiyo, ni kugundulika kuwepo kwa rushwa ya ngono katika hatua mbalimbali za shindano hilo linaloanzia vitongojini.
Aliyekuwa msanii mkongwe katika uchekeshaji maehemu Said Ng’amba ‘Mzee Small’.
5.VIFO VYA WASANII WA MUVI NA MUZIKI
NI mwaka mwingine ambao wasanii wengi, wakiwemo wacheza filamu na wanamuziki walifariki dunia. Mei 27 mwaka huu, msanii wa Bongo Muvi, Rachel Haule alifariki katika hospitali ya Taifa ya Muhimbili. Alikwenda hospitalini kwa ajili ya kujifungua, lakini baada ya kitendo hicho hali yake ilibadilika ghafla ambapo alihamishiwa ICU na hali yake ilizidi kuwa mbaya kabla ya kupoteza maisha.

Recho alifariki wiki moja baada ya muigizaji mwingine maarufu, Adam Kuambiana kufariki ghafla. Baada ya hapo, msururu wa wasanii ulifuata akiwemo prodyuza George Tyson, msanii mkongwe katika uchekeshaji Said Ng’amba ‘Mzee Small’, mwanamuziki wa Twanga Pepeta, Khamis Kayumbu ‘Amigolas’, Side Mnyamwezi, Yesaya Ambilikile ‘YP’ , Maalim Gurumo, Amina Ngaluma, Aisha Madinda na Shem Kalenga.
6. TEGETA ESCROW NA BILIONI 306
DAVID Kafulila, mbunge wa Kigoma Kusini (NCCR-Mageuzi) alianza kama utani, akiwatuhumu vigogo wa serikali kuhusika na wizi wa shilingi bilioni 306, mali ya umma katika akaunti ya Tegeta Escrow. Mwanasheria Mkuu wa serikali wakati huo, Jaji Fredrick Werema akamdhihaki kwa kumuita Tumbili kabla ya kumtishia kumkata kichwa. Dhihaka zikaendelea kwa Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini, Eliakim Maswi, kuziita nyaraka alizokuwa nazo Kafulila kuwa ni makaratasi ya kufungia vitumbua.

Mbunge wa Kigoma Kusini (NCCR-Mageuzi), David Kafulila.
Kadiri muda ulivyokuwa unakwenda, ikaja kuthibitika kuwa ni kweli kulikuwa na uchotwaji wa fedha hizo isivyo halali, kitu kilichosababisha nchi kuingia katika kashfa nyingine ya mabilioni ya fedha, ukiacha EPA, Richmond, Rada na Ndege ya Rais.
Mshindo wa skendo hiyo umeondoka na vigogo watatu, waliotanguliwa na Jaji Fredrick Werema aliyejiuzulu, Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Profesa Anna Tibaijuka aliyeondolewa na Katibu Mkuu Maswi, aliyesimamishwa ili kupisha uchunguzi dhidi yake.
7.HOMA YA DENGUE
Ni ugonjwa mpya ambao uliingia na kumshtua kila Mtanzania, kufuatia kasi yake ya kuua na utata wa tiba yake. Uliwafanya watu kuogopa na kuitaka serikali kuhakikisha tiba yake inapatikana mara moja ili kuondoa hofu miongoni mwa wananchi.

8. UCHAGUZI SERIKALI ZA MITAA 
INGAWA umekuwa ukifanyika kila baada ya miaka mitano, lakini uchaguzi wa serikali za mitaa mwaka huu ulipata hamasa kubwa na kufuatiliwa kwa karibu na watu wengi. Ingawa kama ilivyotegemewa, Chama Cha Mapinduzi kuibuka na ushindi, lakini hata hivyo, matokeo yake yalionyesha dalili za kuimarika kwa vyama vya upinzani baada ya kushinda viti takribani 3000 vya uenyekiti wa serikali za mitaa.

‘Diamond platnumz’.
Uchaguzi huo ambao ulisimamiwa na Tawala za Mikoa (TAMISEMI) iliyo chini ya ofisi ya Waziri Mkuu, ulikuwa na dosari kadhaa zilizomlazimisha Waziri wake, Hawa Ghasia, kuwasimamisha kazi Wakurugenzi, kuwafukuza na wengine kupewa onyo, kufuatia uzembe wao katika kusimamia zoezi hilo muhimu nchini.
DIAMOND, IDRIS WANG’ARA
Msanii wa Bongo Fleva, Nasibu Abdul ‘Diamond’ mwaka 2014 aliwaongoza wenzake kuing’arisha Tanzania kimataifa baada ya kufanikiwa kutwaa tuzo tano barani Afrika. Hizo ni pamoja na tatu kutoka kituo cha televisheni cha Channel O, jijini Johannesburg na  The Future Awards Africa iliyofanyika Lagos, Nigeria.

Ushindi wake huo ulimfanya kupata mapokezi makubwa ya aina yake alipowasili Uwanja wa ndege wa kimataifa wa Julius Nyerere na mashabiki walimsindikiza hadi ukumbi wa Escape One kwa mi guu, umbali wa zaidi ya km 20.
Aidha kijana Idris Sultani alikuwa Mtanzania wa pili kushinda shindano la Big Brother, baada ya Richard Bezuidenhout  kuibuka kinara mwaka 2011. Idris, aliyeshinda Big Brother Hotshots alijinyakulia kitita cha dola 300,000 baada ya kumbwaga Tayo Faniran wa Nigeria.


Bonyeza hapa Tukupe habari zote mara moja zikitoka "HABARI" VITUKO "MAPENZI"MAGAZETI,UDAKU>
Endapo una Habari,Picha,Video,Tangazo au Tatizo Lolote wasiliana nasi kwa namba  +255 688 405 951

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527