ASKARI POLISI WACHAFUA HALI YA HEWA HUKO GEITA,RPC AZIMA HASIRA ZA WAENDESHA BODABODA

Kamanda wa polisi mkoa wa Geita Joseph Konyo akizungumza na waendesha bodaboda mjini Geita
Baadhi ya Askari  polisi Mjini Geita, wamelalamikiwa na waendesha pikipiki maarufu kama bodaboda kwa kukumbatia rushwa jambo ambalo linawaumiza  kiuchumi.

Wakizungumza kwenye Mkutano na kamanda wa polisi Mkoa wa Geita Joseph Konyo, uliofanyika katika ukumbi wa bwalo la  polisi uliopo mjini Geita, baadhi ya waendesha bodaboda walisema  kitendo cha kukamatwa na kuombwa rushwa kimekithiri sana katika mkoa huo.
Mkutano huo ulikuwa na lengo la kujadili  kuhusu kukamatwa kwa watu 16 waendesha bodaboda, waliokuwa katika vurugu ziliz tokea juzi baada ya kumzingira mfanyabishara mmoja Juma Joseph maarufu (Manyama), anayetuhumiwa kuhusika  kupanga mauaji na kupora pikipiki.
“Kamanda tunashukuru kwa kutuita waendesha bodaboda wote katika ukumbi huu, ili tujadili changamoto za kuuawa kwa bodaboda wenzetu, lakini kuna jambo ambalo sisi kama waendesha pikipiki linatukera sana la baadhi ya askari wako wanatuomba rushwa kwa nguvu,”walisema waendesha bodaboda hao.
Waendesha bodaboda hao walieleza kuwa wamekuwa wakiogopa kwenda kituo cha polisi pindi wanapokuwa na shida au wanapowatambua wahalifu wanaowabeba kwa kuogopa kubambikiziwa kesi jambo ambalo baadhi ya waendesha pikipiki wamebambikwa kesi na kuwekwa ndani.

“Sisi tunapenda sana ushirikiano kati yetu na polisi lakini kamanda tumekuwa tukihofia kufika kituoni kutoa ushahidi ama malalamiko yetu kwa sababu wakati mwingine unatoa ushahidi mwisho wa siku unageukwa na kupewa kesi kuwa wewe ni mhalifu,”alisema Joseph Iddi.

Baada ya kupokea malalamiko hayo Kamanda Konyo, alisema atayashughulikia na ikibainika askari wake wanahusika moja kwa moja, sheria za kinidhamu zitachukuliwa dhidi yao bila kujali cheo cha mtu.

“Niwatoe wasiwasi malalamiko yenu nimeyapokea yote na niwaahidi nitafUatilia moja baada ya jingine na yeyote atakayebainika amefanya hayo atashughulikiwa, sisi tupo hapa kwa kushughulikia matatizo yenu, kwanza hakuna askari yeyote katika nchi hii anayeruhusiwa kunyanyasa raia na suala la rushwa ni matakwa ya mtu mwenyewe na jeshi letu tunapinga suala la rushwa,’’alisema Konyo.

Katika hatua nyingine Konyo alimwagiza mpelelezi wa wilaya  ya Geita Kinyunko Marlaw, kuwaachia huru  waendesha bodaboda 16 waliokamatwa na polisi  bila kuwekewa masharti ya aina yeyote lakini akasisitza kuwa iwapo wataachiwa wasifanye fujo wala kuharibu mali za mtuhumiwa bali wawe watulivu wakati wakisuburi mtuhumiwa apandishwe mahakamani.

“Jamani waendesha bodaboda nawaomba tuendelee kushirikiana mnapobaini kuna tatizo ama uharifu tupeane taarifa ili tudhibiti hii hali na suala la kukamatwa kwa wenzenu 16 nimeshatoa maagizo wadhaminiwe bila masharti, lakini chonde chonde hawa watu watakapotoka wasifanye vurugu yeyote wala kuharibu mali za mtuhumiwa hapa haki lazima itendeke hayupo atakayeonewa,”alisema Konyo.
Na Valence Robert-Malunde1 blog Geita 


Bonyeza hapa Tukupe habari zote mara moja zikitoka "HABARI" VITUKO "MAPENZI"MAGAZETI,UDAKU>
Endapo una Habari,Picha,Video,Tangazo au Tatizo Lolote wasiliana nasi kwa namba  +255 688 405 951

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527