Mgogoro wa Wakulima na Wafugaji!!! MKUU WA MKOA WA SHINYANGA AKUTANA NA WAFUGAJI WILAYANI KISHAPU

Aliyesimama ni Mkuu wa mkoa wa Shinyanga Ally Nassoro Rufunga akizungumza na wananchi wa kijiji cha Magalata wilayani Kishapu kuhusu vurugu zilizotokea wiki iliyopita wakati wa mapigano baina ya Wafugaji na wakulima wa wilaya ya Kishapu mkoani Shinyanga na wilaya ya Igunga mkoani Tabora
Mwenyekiti wa Chama cha wafugaji Kanda ya Ziwa Bwana Mrida Mshota aliwasihi wafugaji wa kijiji cha Magalata kutulia na kusubiri taratibu za serikali
Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga Mheshimiwa  Ally Nassoro Rufunga amewataka wafugaji wanaoishi katika kijiji cha Magalata wilayani Kishapu mkoani Shinyanga kutovuka mto Manonga na kuingia katika wilaya ya Igunga wakati serikali inashughulikia suala la mpaka wa wilaya hizo mbili.

Mheshimiwa Rufunga ametoa agizo hilo jana alipokutana na wafugaji hao katika kijiji cha Magalata wilayani Kishapu, ikiwa ni moja ya makubaliano ya kikao cha Kamati za ulinzi na usalama za mikoa ya Tabora na Shinyanga kilichoketi juzi kuwa kila upande kwa wilaya za Kishapu na Igunga wananchi waelimishwe kutumia ardhi na kuwa watulivu wakati huu serikali inapofanya uchunguzi ili kubaini chanzo cha mgogoro na kufuatilia mpaka halali wa eneo hilo.

Awali wafugaji waliieleza kamati ya Ulinzi na Usalama ambayo Mkuu wa mkoa ni mwenyekiti, kuwa mpaka halisi ni mto Mwanyerere (Manonga) lakini mto huo ulihama kutokana na mvua mwaka 1998 na sehemu kubwa uliingia eneo la Kishapu hivyo eneo lao la kitongoji cha Magogo likabaki upande mwingine na wamekuwa wakichungia huko kwa muda mrefu hadi hapo wakulima wa wilaya ya Igunga walipovamia eneo hilo ndipo vurugu zilianza.

Naye Mwenyekiti wa Chama cha wafugaji Kanda ya Ziwa Bwana Mrida Mshota aliwasihi wafugaji wa kijiji cha Magalata kutulia na kusubiri taratibu za serikali kwani suala hilo limeanza kushughulikiwa muda mrefu tangu serikali ilipopata taarifa za uvamizi huo, chama cha wafugaji pia kinashirikiana kwa karibu na serikali kuhakikisha haki inapatikana.

Mgogoro huo unatokana na kugombea eneo kati ya wakulima wa kijiji cha Isakamaliwa wilayani Igunga mkoani Tabora ambao ni wahitimu wa vyuo vikuu waliopewa eneo hilo na serikali ya mkoa ya Tabora kwa ajili ya kujiajiri kwa njia ya kilimo, wakati huohuo wafugaji wa kijiji cha Magalata wilayani Kishapu mkoa wa Shinyanga wenye asili ya Kitaturu wakidai wamevamiwa eneo hilo  kwani wamelisha mifugo yao kwa miaka mingi hapo.

Serikali ya Mkoa wa Shinyanga na Tabora zinaendelea kushughulikia tatizo hilo lililosababisha vifo vya watu watano na majeruhi mmoja ambapo tume ya watu 18 imeshaundwa na kupewa muda wa wiki nne kufanya uchunguzi wa chanzo hasa cha mgogoro huo na kujua mpaka halali wakati wananchi wakiendelea kuelimishwa kuwa na subira.

Na Magdalena Nkulu -Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Shinyanga

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post