Mapenzi hatariii !!! JAMAA AUA MCHUMBA WAKE NA KUMZIKA PORINI,FISI WAFUKUA KABURI,MBWA WALA KICHWA CHA MAREHEMU

Watu wawili wamekufa katika matukio tofauti wilayani Bunda, mkoani Mara, akiwemo mwanamke mmoja aliyeuawa na mchumba wake na kufukia mwili wake porini na kisha fisi kufukua kaburi hilo na kichwa chake kuonekana mitaani kikiliwa na mbwa.

Tukio hilo la kikatili lililothibitishwa na polisi, limetokea Machi 22 mwaka huu, majira ya saa 3:00 asubuhi katika kijiji cha kiroreli wilayani Bunda.

Mwanamke aliyeuawa na mchumba wake ametambuliwa kwa jina la Wambura Magonze, mkazi wa kijiji cha Kiroreli.

Polisi wamesema kuwa baada ya kupata taarifa ya tukio hilo walikwenda katika eneo la tukio wakiongozana na mkuu wa upelelezi wilayani hapa, Munguwajuna, na kukuta mbwa mitaani wakila kichwa cha marehemu huyo.
 
Imeelezwa kuwa mwaume huyo baada ya kumuua mchumba wake kwa kipigo, wakiwa wanatoka shambani aliuzika mwili wake porini katika kaburi lenye urefu wa futi moja.

Aidha, imeelezwa kuwa baadaye wanyama wanaodhaniwa kuwa ni fisi waliufukua mwili huo na kuanza kuula, na kwamba kichwa cha marehemu kilionekana mitaani kikiliwa na mbwa.

Mwanaume huyo Matoka Maroba Isumail (24) mkazi wa kijiji hicho, baada ya tukio hilo alitoroka, lakini baadaye akakamatwa na polisi na amekiri kufanya mauwaji hayo.

Polisi wamesema kuwa awali mwanaume huyo aliandika ujumbe kwenye vipande vya karatasi vipatavyo saba na kuvipeleka nyumbani kwa baba wa mwanamke huyo, ambavyo vilikuwa na vitisho kadhaa.

Katika maelezo yake aliyotoa polisi mwanaume huyo amesema kuwa aliamua kumuua mchumba wake huyo kwa sababu baba yake alikuwa anataka kumuoza kwa mume mwingine kwa mahali nyingi, licha ya yeye kukubaliana kutoa mahali ya ng’ombe saba na laiki sita, pamoja na kutoa kishika uchumba cha sh. 70,000.

Ameongeza kuwa baada ya kumuua mchumba wake yeye pia alikuwa anao mpango wa kujiua na kwamba tayari alikuwa amekwishaandika historia ya maisha yake ambayo ingesomwa wakati wa mazishi yake.

Mtuhumiwa huyo  leo Jumatano amefikishwa kwa mlinzi wa amani na akakiri kufanya mauaji hayo, ambapo kesho asubuhi atafikishwa katika mahakama ya wilaya ya Bunda, kujibu tuhuma hiyo.

Na katika tukio jingine lililotokea usiku wa kuamkia leo Jumatano, mwendesha pikipiki mmoja Kitaboka Maringo Matutu Issa, mkazi wa mjini Bunda, ameuawa na mtu au watu wasiofahamika kwa kupigwa na kitu kizito kichwani, pamoja na kuchomwa shingoni na kitu chenye ncha kali.

Tukio hilo ambalo pia lilithibitishwa na polisi limetokea katika mtaa wa Manyamanyama kata ya Nyasura mjini Bunda.

Afisa mtendaji wa kata ya Nyasura, John Yapanda, amesema kuwa mwendesha pikipiki huyo aliuawa kikatili na watu hao ambao pia walimpora pikipiki yake.

Kamanda wa polisi mkoani Mara, kamishina msaidizi mwandamizi wa polisi, Ferdinand Mtui, leo hakupatikana kuzungumzia matukio hayo, kutokana na pilikapilika  za shughuli za msiba wa mkuu wa mkoa wa Mara, John Gabriel Tupa, aliyefariki dunia ghafla jana akiwa wilayani Tarime, alikokuwa amekwenda kufunga mafunzo ya mgambo.
  Via>>Mara yetu

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments