KUHUSU TUKIO LA WANA NDUGU 12 KUPOTEZA MAISHA KATIKA AJALI YA BARABARANI WAKIENDA MSIBANI HUKO KILIMANJARO

Lori la mizigo aina ya Fusso likiwa limegongana na  gari ndogo aina ya Toyota Hilux Pick Up katika eneo la Hedaru, wilayani Same, Kilimanjaro, juzi  na kusababisha vifo vya watu 12.


Mji wa Hedaru uliopo wilayani Same mkoani Kilimanjaro, jana ulizizima kwa vilio na simanzi baada ya waombolezaji 12 wote ndugu, kufariki dunia kwa ajali ya barabarani.
 
Waombolezaji hao wanawake, walipewa lifti ya gari na Diwani wa Kata ya Hedaru, Gerard Mgwena (CCM), kwa ajili ya kuwapeleka msibani eneo la Majengo ambako mtu mmoja alifariki kwa kusombwa na maji.
Kamanda wa Polisi mkoa wa Kilimanjaro (RPC), Robert Boaz alithibitisha ajali hiyo akisema ilitokea juzi saa 2:00 usiku na kwamba ilikuwa mbaya zaidi tangu kuanza kwa mwaka 2014.
“Ni ajali iliyohusisha magari matatu kwa wakati mmoja…; watu 11 walifariki pale pale na mwingine alifariki dunia leo (jana), asubuhi Hospitali ya Rufaa ya KCMC,”alisema Boaz.
Hata hivyo, alisema hakuwa na nafasi nzuri ya kufafanua kwa undani ajali hiyo kwa vile alikuwa nje ya Mkoa wa Kilimanjaro na kuelekeza atafutwe Kamanda wa Kikosi cha Usalama Barabarani Mkoa (RTO), Joseph Mwakabonga.
Akizungumza kwa niaba ya RPC, Mwakabonga alisema, lori aina ya Mitsubish Fusso lililokuwa likitokea Moshi kwenda Dar liligonga kwa nyuma gari aina ya Toyota Hilux Pick-Up.
Alisema kuwa baada ya kuligonga gari hilo lililowabeba waombolezaji hao, nalo lilisukumwa na kwenda kuligonga lori aina ya Scania lililokuwa na tela lake.
Lori hilo aina ya Scania lilikuwa likitokea Dar es Salaam kwenda Moshi likiendeshwa na dereva wake, Gabriel David. Madareva wawili wa Toyota Pick-Up na Toyota Fusso wote hawajulikani waliko.
Taarifa zilizopatikana baadaye, zilisema dereva wa Fusso alikuwa amelazwa katika Hospitali ya KCMC, wakati Kigogo wa CCM aliyekuwa amewabeba waombolezaji akilazwa hospitali moja jijini Arusha.
Mwakabonga aliwataja waliofariki kuwa ni Stella John(45), Salma Kizoka (33), Marry Senzige (49), Neema Daniel (52), Rehema George (29) na Sophia Mbike (51).
Wengine ni Ritha Kalani (55), Mama Kalani Stephano (55), Kolina Mmatha(55), Bahati Daud(25) na Farida Kiondo mwenye umri wa miaka 25.
Majeruhi mmoja, Maria John (33) ambaye ni miongoni mwa watu 10 waliojeruhiwa, alifariki dunia jana asubuhi katika Hospitali ya Rufaa ya KCMC alikolazwa kwa ajili ya kuokoa maisha yake.

Kwa mujibu wa watu walioshuhudia ajali hiyo, watu hao walipata ajali hatua 10 kutoka katika eneo ambalo ndugu yao aliosombwa na maji na kufa, ambapo maiti yake iliokotwa eneo hilo.
Alex Shirima mmoja wa mashuhuda alisimulia kuwa gari la diwani lilikwama kweye tope katikati ya Barabara ya Moshi Dar es Salaam.
Alisema, kabla ya kushuka kuangalia namna ya kulinasua gari lake, likatokea lori gari aina ya Fuso kwa nyuma ambalo liliigonga gari lake iwani na kulisukuma mita kadhaa mbele ambako lilikutana uso kwa uso na lori lingine aina ya Scania lililokuwa likitokea Dar es Salaam.
Alisimulia kuwa kutokana na ukubwa wa ajali hiyo, eneo hilo lilitapakaa viungo vya binadamu na damu.
Shirima ambaye ni dereva aliyefika katika eneo hilo dakika mbili baada ya ajali kutokea, alisema eneo hilo ni hatari kwa madereva kwa kuwa mvua zikinyesha, barabara hujaa maji na matope.
Hali ilivyo kijijini
Mmoja wa watoto ambaye mama yake mzazi amefariki katika ajali hiyo, Sebali Mkwizu alisema kuwa kijiji chao kimekumbwa na ukimya na majonzi, huku wakishindwa kuamini kilichotokea.
Alisema kuwa ajali hiyo imechukua maisha ya ndugu zake wanane na kati ya hao, saba walikuwa wakiishi kijijini hapo kwenye nyumba tofauti zinazofuatana.
“Nimepoteza mama yangu mzazi, mama mdogo, shemeji zangu watatu, mke wa ndugu yangu na watoto wawili. Hapa nyumba saba zina msiba,” alisema Mkwizu.
Alibainisha kwamba mazishi ya wanawake hao yanatarajiwa kufanyika leo katika eneo la pamoja kijijini hapo.
“Tumeambiwa watazikwa eneo moja, lakini bado hatujajua ni sehemu gani, hadi kesho (leo) ndiyo tutapata taarifa kamili,” alisema.
 Na Daniel Mjema na Rehema Matowo

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments