Hatari hii!! MAAFISA USALAMA FEKI WATEKA WAFANYABIASHARA MUME NA MKE HUKO SINGIDA


DSC001791
WAFANYABIASHARA wa Manyoni mjini mkoani Singida mume na mke,wametekwa na watu watatu waliojifanya kuwa ni maafisa usalama wa taifa makao makuu jijini Dar-es-salaam.
Waathirika wa utekaji huo ni Methew Dominik Cheupe (46) na mke wake Selina Methew (42).

Kamanda wa Jeshi la Polisi mkoani Singida, SACP Geofrey Kamwela amesema tukio hilo limetokea juzi saa tisa alasiri Manyoni mjini.

Amesema Faraja George (35) mfanyabiashara wa Dodoma mjini,mganga wa tiba asilia na mkazi wa mkoa wa Tanga,Saidi Mgolola @Pesa mbili (49) Michael Peter  na Michael Peter (26) mkazi wa Moshi mjini na dereva wa gari lililotumika katika utekaji huo.

Amesema siku ya tukio watuhumiwa wakiwa na gari T.242 CBM aina ya toyota prado,walifika dukani kwa Methew baada ya kudai kuwa wao ni maafisa usalama taifa,walimwamuru mwenye duka kuwa wanamhitaji Singida mjini kwa ajili ya mahojiano.

“Methew aliwaomba maafisa hao bandia kuwa aambatane na mke wake huko kwenye mahojiano hayo.Baada ya waathirika hao kuingia ndani ya gari,gari hilo badala ya kuelekea Singida mjini,lilibadili na kuelekea Dodoma”,amesema.

Kamwela amesema bahati nzuri polisi Manyoni mjini walipata taarifa ya tukio hilo mapema na wakawasiliana na wenzao wa Bahi mkoani Dodoma ambao walifanikiwa kuwanasa watuhumiwa hapo kwenye kizuizi.

Amesema uchunguzi wa awali umebaini kuwa chanzo cha tukio hilo,ni watuhumiwa kutaka kumwibia mali mfanyabiashara hiyo Methew.Uchunguzi zaidi bado unaendelea.

Kamwela amesema kuwa mara upelelezi utakapokamilika,watuhumiwa watafikishwa mahakamani kujibu tuhuma inayowakabili.
 Na Nathaniel Limu, Singida

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments