CCM YAWANYEMELEA WALIOFUKUZWA NA CHADEMA HUKO KAHAMA,KIKAO CHA SIRI KUWANASA CHAFANYIKA


Chama Cha Mapinduzi (CCM) kimeanza mkakati wa kuwachukua waliokuwa viongozi wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) wilayani Kahama waliofukuzwa uanachama hivi karibuni kwa tuhuma mbalimbali ikiwemo kumuunga mkono aliyekuwa Naibu Katibu Mkuu wa Chama hicho Mhe. Zitto Kabwe.
 
Katika mikakati hiyo katibu Mkuu wa Umoja wa Vijana wa CCM Taifa Bw. Sixtus Mapunda ameingia mjini Kahama kimyakimya bila kuripoti sehemu yoyote na kufanya mkutano wa siri na waliokuwa viongozi hao.
 
Kwa mujibu wa chanzo chetu cha habari kimedai kuwa Mapunda baada ya kufika mjini Kahama akitokea Dodoma amefikia hotel mojawapo mjini humo kwa siri na kuwaalika baadhi ya makada wachache wa CCM ambao amewapa masharti ya kutotoa taarifa yoyote juu ya ujio wake.
 
Mmoja wa watu aliowaalika kwenye kikao cha awali kabla ya kukutana na makada hao wa CHADEMA amesema Katibu Mkuu huyo hakutaka kujulikana kama ana mazungumzo na watu hao ingawa amefika kwa kazi hiyo maalumu.
 
Hivi karibuni CHADEMA kiliwafukuza viongozi wake sita wakiwemo watano wa Jimbo la Kahama, miongoni mwao akiwa ni  Diwani wa Kata ya Majengo Bw. Bobson Wambura, kwa madai ya kukiuka Katiba na kuhujumu ya chama wakati wa uchaguzi mdogo wa Udiwani wa Kata ya  Ubagwe uliomalizika hivi karibuni .
 
Wambura ambaye pia alikuwa Katibu Mwenezi wa Jimbo alifukuzwa sambamba na Mwenyekiti wa Jimbo la Kahama Bw. Israel Barakiel, Katibu wa Jimbo hilo Bw. Vicent Kwilukilwa, Mwenyekiti wa BAVICHA Jimbo Bw. Benedicto Shija, Mwenyekiti BAWACHA Jimbo Bw.Kasigwa Adram pamoja na Mratibu wa Vijana wilaya Bw. Vicent Manyambo.
 
Aidha katika kikao hicho cha katibu mkuu wa UVCCM chanzo chetu kimeeleza kuwa waliokuwa makada hao  wa CHADEMA wametakiwa kurudi CCM na katika ziara ya Katibu Mkuu wa CCM Taifa Bw. Abdurahman Kinana na Katibu Mwenezi wake Bw. Nape Nnawiye inayotarajiwa kufanyika hivi karibuni wilayani Kahama watakabidhi kadi za CHADEMA.
 
Hata hivyo mazungumzo hayo ya awali yameonesha kugonga mwamba baada ya kutofikia maelewano ya kimaslahi kati ya Katibu huyo na wana CHADEMA hao waliofukuzwa ambapo mmoja wao aliyeongea kwa niaba yao amesema wameshindwa kuelewana.
 
Mwana CHADEMA huyo aliyefukuzwa Bw. Bobson Wambura kwa niaba ya wenzake amesema wameshindwa kuelewana kutokana na kuwataka wajiunge kwanza na CCM na siku wakikabidhi kadi ndipo watapewa fedha.
 
Pamoja na kuthibitika kuwa Katibu Mkuu huyo wa UVCCM yuko mjini Kahama,lakini alipotakiwa kuthibitisha kwa njia ya simu uwepo wake Bw. Mapunda amegoma akidai hajawahi kufika Kahama kufanya kikao na watu hao,ingawa ameonesha kuwafahamu wengine kwa majina. 
 
Chanzo-Wangsteve blog

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post