Habari
kutoka mjini Nzega zinasema kuwa Chama Cha Mapinduzi (CCM) wilayani Nzega mkoani
Tabora kinakusudia kumnyang’anya kadi mbunge wake, Dkt Hamisi Kigwangala baada
ya kumtuhumu kwenda kinyume na matakwa ya chama hicho, pamoja na kuwaadhibu madiwani wake wanne baada ya
madiwani hao hivi karibuni kuungana na mbunge huyo kufanya maandamano kupinga maamuzi
ya baraza la madiwani kubadili matumizi ya fedha zilizotolewa na mgodi wa
dhahabu wa Resolute Tanzania Ltd. kiasi cha shilingi bilioni 2.340 ikiwa ni
ushuru wa huduma.
Dkt
Kigwangala pamoja na madiwani hao wanne wanadaiwa kuungana na madiwani wengine
wanaotokana na vyama vya CUF na CHADEMA pamoja na wakazi wa mji wa Nzega
kufanya maandamano makubwa kwenda kwa mkuu wa wilaya ya Nzega kumtaka azuie
kutekelezwa kwa mabadiliko ya matumizi ya fedha hizo.
Imeelezwa
kuwa kitendo cha Dkt. Kigwangala pamoja na madiwani kufanya mkutano wa hadhara
na kisha kuandamana hadi kwa mkuu wa wilaya kiliwakera viongozi wa CCM
wanaodaiwa kuwashinikiza madiwani kubadili matumizi ya fedha hizo na kuagiza
zigawanywe katika kila kata badala ya kununulia mitambo ya kutengenezea
barabara.
Hivi
karibuni wananchi wa Nzega waliungana na mbunge wao na madiwani sita kuandamana
kwenda kwa mkuu wa wilaya hiyo, Bituni Msangi kushinikiza azuie fedha hizo
zisigawanywe katika kila kata kama walivyopendekeza madiwani mpaka muafaka
utakapopatikana na kwamba kitendo cha kutengua bajeti ya awali kinapingana na
utaratibu wa kanuni za halmashauri.
Wananchi hao
walishangazwa na uamuzi wa madiwani kubadili matumizi ya fedha hizo ambazo
tayari katika kikao halali kilichofanyika Aprili 24 na 25 mwaka jana
kilipitisha bajeti ya matumizi yake na kuelekeza zinunulie mitambo ya
kutengenezea barabara na ya kuchimbia visima vya maji na sehemu yake itumike
kuanzishia benki ya watu wa Nzega.
Akiandika
kupitia mtandao wake wa kijamii, mbunge wa Jimbo la Nzega, Dkt. Kigwangala
alithibitisha kupata taarifa hizo ambapo hata hivyo alisema iwapo Chama chake
kitachukua maamuzi hayo yuko radhi kuyapokea kwa vile sasa amechoka kuvutana na
watu wasioitakia maendeleo ya kweli wilaya ya Nzega.
“Nimeshangazwa
sana na kusikitishwa na jinsi Chama kinavyoendeshwa, ninaamini viongozi wakuu
wa Chama wanafuatilia kwa ukaribu na watachukua hatua stahiki. Kwamba kuna watu
wana nguvu kuliko Chama, kwamba wachache wanaweza kuwaonea wengine kwa kuwa
wana vyeo na mamlaka ya kufanya hivyo, na hakuna wa kuingilia kati na kusema
'no',”
“Basi sina
haja ya kuendelea kupambana. Nimechoka, sintokata rufaa wala sintolalamika
tena! Watekeleze hukumu hiyo. Sintojitetea na sintohudhuria kikao chochote kile
kuanzia sasa. Nimechoka kupambana na watu wenye nguvu, nimechoka. Ni bora kuwa
mnyonge lakini ukabaki na uhai, uzima, heshima na furaha yako,” alieleza Dkt.
Kigwangala.
Kwa upande
wao baadhi ya madiwani wanaotuhumiwa kuungana na mbunge huyo kufanya mkutano na
maandamano haramu ambayo pia yaliwahusisha madiwani wa vyama vya upinzani na
viongozi wao wamekiri kupewa adhabu ya onyo kali kutokana na kitendo chao
hicho.
“Ni kweli
kabisa chama kimetuadhibu kwa kutupa adhabu ya onyo kali sisi madiwani wanne,
ambapo hata wale waliokuwa na nyadhifa wamevuliwa nyadhifa zao akiwemo
aliyekuwa katibu wa madiwani wa CCM, tumeonywa vikali sana tukidaiwa kushiriki
maandamano na mkutano haramu, imetushangaza sana,”
“Lakini
chanzo cha hali hii ni baada ya madiwani kuwagomea viongozi wa CCM ambao
waliomba wapatiwe shilingi milioni 200 ili wajengee ukumbi wa mikutano
utakaomilikiwa na chama hicho, lakini ukweli ni kwamba fedha hizo bajeti yake
tuliishaipitisha tangu mwaka jana, tumekata rufaa mkoani kupinga adhabu hii,”
“Kwa kweli
tuliona tukikubali ombi hilo lingeweza kututia matatani zaidi tulikataa kwa
vile fedha hizo ni za wananchi wote wa Nzega na hazikutolewa kwa lengo ya
kukisaidia chama chochote cha siasa, nahisi tulipogoma ndipo
tukashinikizwa tubadili matumizi ili sasa zielekezwe kwenye kata,” alieleza
diwani huyo.
Hata hivyo
kwa upande wake katibu wa CCM wilayani Nzega, Vyolohoka Kajolo akizungumza
kupitia simu yake ya kiganjani hakuweza kukanusha moja kwa moja madai hayo
ambapo aliwaomba waandishi kuwauliza madiwani wanaodai kuadhibiwa iwapo tayari
wameishapatiwa barua zozote juu ya maamuzi hayo.
“Haya ni
mambo ya ndani haturuhusiwi kuyatoa nje, hakuna mtu aliyeadhibiwa na kama ni
kweli basi wawaonesha barua waliozopewa, na hatujamvua madaraka diwani ye yote
yule wala kutishia kumpokonya kadi mbunge wetu, haya mambo hata mimi nimeyasoma
kupitia mitandao ya kijamii na baadhi ya vyombo vya habari, hatujaadhibu mtu,”
alieleza Kajolo.
Post a Comment