KIKONGWE AUAWA KWA KUKATWA PANGA WAKATI AKIOTA MOTO NYUMBANI KWAKE,ADAIWA KUWAROGA WANAKIJIJI -KATAVI

Siku chache tu baada ya mwanamme aitwaye Mwami Mwanalusi (31) kukatwa sehemu zake za siri  akiwa amelala nyumbani kwa shemeji yake mkoani Katavi , hali imeendelea kuwa mbaya ambapo juzi,mtu  mmoja aliyefahamika kwa jina la Mele  Seni (60)  Mkazi wa Kijiji cha Kapalala Tarafa ya Nsimbo Wilaya ya Mlele Mkoa wa Katavi  ameuawa kwa kukatwa na panga kichwani na mgongoni na watu wasio fahamika wakati akiwa nyumbani kwake akiota moto.


Kwa mujibu wa Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Katavi Dhahiri Kidavashari  tukio hilo la mauaji ya kinyama limetokea juzi majira ya saa moja  na nusu usiku nyumbani kwa marehemu huyo kijijini hapo.

Alisema siku hiyo ya tukio marehemu akiwa nyumbani kwake amejipumzisha akiota moto ghafla  walitokea watu wasiofahamika na kupiga hodi nyumbani kwa marehemu ambae nae aliwakaribisha watu hao kwa kujua ni watu wema.

Alieleza ndipo watu hao walipoanza kumshambulia marehemu kwa kumkata kwa panga kwenye kichwa na mgongoni huku marehemu akiwa anapiga mayowe ya kuomba msaada kwa majirani zake.

Kidavashari alisema licha ya marehemu kupiga moyowe majirani zake hawakuweza kujitokeza mapema kuweza kumpatia  msaada na ndipo watu hao walipoona Mele Seni amefariki dunia huku wauaji wakitokomea  kusiko julikana.

Majirani waliweza kufika nyumbani kwa marehemu baada ya muda mrefu wa kutokea kwa tukio hilo ambapo walimkuta marehemu akiwa ameisha fariki dunia huku mwili wake ukiwa na majeraha ya panga kichwani na mgongoni na kisha walitowa taarifa kwa uongozi wa serikali ya kijiji ambao nao walitowa taarifa kwa jeshi la polisi.

Kamanda Kidavashari alieleza kabla ya tukio hilo  marehemu alikuwa akilalamikiwa  na majirani zake na wanakijiji hicho kuwa amekuwa akijihusisha  na vitendo vya kishirikina kwa kuwaroga watu kijijini hapo.

Hivyo uchunguzi  wa awali uliofanywa na jeshi la Polisi  umebaini kifo hicho kametokana na imani ya ushirikina  ulisababisha wanakijiji hicho kumjengea chuki marehemu huyo.

Mpaka sasa hakuna mtu   au watu waliokamatwa kuhusiana na tukio hili  na jeshi la polisi  linaendelea  na upelelezi ili kuwakamata na kuwafikisha mahakamani  waliohusika katika tukio hili.

Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Katavi  ametowa wito  kwa wananchi kutojichukilia sheria  mkononi  kutokana na kuwahusisha watu na imani za kishirikina na matokeo yake wamekuwa wakiua watu  pasipo sababu
N a Walter Mguluchuma


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post