NOMA KWELI--MCHUNGAJI RWAKATARE ATENGWA,APONZWA NA NDOA YA MBUNGE NA KINDA

Na Betty Kangonga

MBUNGE wa Viti Maalumu, Mchungaji Getrude Rwakatare (CCM) wa Kanisa la Tanzania Assemblies of God (TAG), Mikocheni B, jijini Dar es Salaam, ametengwa katika Ushirikiano wa Makanisa baada ya kanisa lake kulalamikiwa kufungisha ndoa inayodaiwa kukiuka taratibu za kikanisa, kisheria na kimaadili, Tanzania Daima Jumatano limejulishwa.
Ndoa inayolalamikiwa kufungishwa na kanisa hilo ni ile iliyoibuliwa na gazeti hili wiki iliyopita ambayo inamhusisha Mbunge  wa Viti Maalumu, Rosweeter Kasikila (CCM) mwenye umri wa miaka 60 na kijana Michael Christian wa miaka  26.
Ndoa hiyo ambayo ilifungwa katika kanisa hilo Septemba Mosi mwaka 2011, imebaki kuwa gumzo na kuwaacha hoi baadhi ya mawaziri, wabunge pamoja na majirani wanaoishi jirani na mbunge huyo mjini Bagamoyo, Pwani.
Akizungumza na gazeti hili jana, Mwenyekiti wa Kamati ya Maadili na Haki za Jamii ya makanisa hayo, Mchungaji William Mwamalanga, alisema uamuzi wa kulitenga kanisa la Mama Rwakatare umetokana na kikao cha Kamati ya Maadili iliyokutana jana jijiji Dar es Salaam.
Alisema Kanisa la Mchungaji Rwakatare halifai kuendelea kuwa katika ushirika huo kutokana na kubariki ndoa hiyo aliyodai kuwa ni batili.
Mchungaji Mwamalanga alisema utaratibu wa ndoa katika makanisa unafahamika, ikiwa ni pamoja na wafungaji wa ndoa kutakiwa kutangaza ndoa hiyo hadharani kwa kipindi cha wiki tatu.
“Ndoa hii haikutangazwa hadharani, kibaya zaidi inasemekana imefungwa ndani ya ofisi na sio kanisani. Hiyo haiwezi kuitwaa ndoa maana haijakidhi vigezo na taratibu za kikanisa, ni lazima Mchungaji Rwakatare awajibike,” alisema.
Alisema lazima nyumba za ibada zikubali kutogeuzwa kichaka cha kusaidia uovu kama ilivyofanywa na kanisa hilo la Mikocheni B kwa kukubali kufanikisha ndoa hiyo kinyume cha taratibu.
“Tunalaani ndoa hiyo kuanzia mawio hadi machweo kwa kuwa hata maandiko ya kitabu kitakatifu cha Biblia kinawathamini yatima kama alivyo huyo kijana Michael anayeonekana kutoafiki ndoa hiyo kwa matakwa yake,” alisema mchungaji huyo.
Alisisitiza kuwa wanamtenga Mchungaji Rwakatare na kanisa lake kwani amewachafua  na kuyatia aibu makanisa mengine yote nchini.
Mchungaji huyo pia alimtaka Mwenyekiti wa CCM taifa, Rais Jakaya Kikwete kuwaengua kwenye chama hicho Mchungaji Rwakatare na Kasikila kuhusiana na ndoa hiyo.
“Rwakatare ni mtunga sheria, anajua wazi kuwa ndoa inatakiwa pia kubandikwa katika ubao wa matangazo. Ni wazi kuwa wameamua kuvunja sheria na kutenda kosa la jinai,” alidai.
Mwamalanga alisema kuwa kwa hatua hiyo ndoa hiyo ni batili na haramu kwa kuwa ni aibu pia kwa mtoto kumuoa mwanamke mwenye umri wa mama yake.
Katika hatua nyingine, mchungaji huyo alisema umoja wao unafanya kila iwezalo kuhakikisha kijana Michael anarudishiwa vyeti vyake ambavyo kwa sasa vimezuiliwa na Mbunge Kasikila.
Pia aliitaka Kamati ya Maadili ya Bunge kuwaita na kuwahoji wabunge hao kwa kitendo chao cha kuhalalisha ndoa hiyo kwani kimeutia doa muhimili huo.
Alisema Bunge ni sehemu tukufu, hivyo Rwakatare na Kasikila hawana hadhi ya kukaa huko, hivyo alishauri waenguliwe.
Alipopigiwa simu kueleza msimamo wake juu ya uamuzi wa umoja wa makanisa hayo kumtenga kwa kuhalalisha ndoa hiyo, Mchungaji Rwakatare aling’aka na kukata simu.
Alipopigiwa tena simu yake ilizimwa na hakuweza kupatikana tena hadi tunaenda mitamboni.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments