Habari Mpya

6/recent/ticker-posts

WAZIRI SANGU ASISITIZA WAAJIRI KUTEKELEZA AMRI YA KIMA CHA CHINI CHA MISHAHARA


Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu Kazi, Ajira na Mahusiano, Mhe. Deus Sangu amewataka waajiri nchini kuzingatia viwango vya kima cha chini cha mshahara vilivyowekwa na Serikali ili kuhakikisha wafanyakazi katika sekta binafsi wanapata stahiki zao kwa mujibu wa sheria hatua itakayosaidia utekelezaji wa Dira ya Maendeleo ya Taifa 2050.

Mhe. Sangu ametoa wito huo Juni 25, 2026, wakati akifungua Mkutano Mkuu wa 67 wa Chama cha Waajiri Tanzania (ATE) uliofanyika katika Hoteli ya Serena, jijini Dar es Salaam ambapo amesema ulipaji wa mishahara inayokidhi viwango vya chini vilivyowekwa kisheria ni wajibu wa kila mwajiri ambapo inaongeza motisha kwa wafanyakazi na kuimarisha uzalishaji katika maeneo ya kazi.

Waziri Sangu amesema ili sekta ya kazi kuendelea kuwa na mafanikio ni jambo muhimu kutekeleza Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 ili kuhakikisha nguvu kazi ya wafanyakazi inalindwa na wakati huo huo kuhakikisha kuwa mazingira ya biashara yanabaki rafiki, shindani na endelevu.

Amesema Serikali haitasita kuchukua hatua za kisheria dhidi ya waajiri watakaobainika kukiuka masharti ya mishahara kwa kuwalipa wafanyakazi kiwango cha chini ya kile kilichoainishwa katika sheria na kanuni za kazi.

Sambamba na hilo, Waziri Sangu amewataka waajiri wote kuendelea kuzingatia sheria za kazi kwa kuwasilisha kwa wakati michango ya wafanyakazi katika mifuko ya hifadhi ya jamii ikiwemo NSSF, PSSSF pamoja na Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi (WCF) bila kuchelewa au kukiuka taratibu zilizowekwa.

Aidha, amesisitiza umuhimu wa kuendeleza mahusiano mazuri kazini kupitia majadiliano na ushirikiano kati ya waajiri na wafanyakazi ili kuimarisha tija, amani na maendeleo katika maeneo ya kazi.

Katika hatua nyingine, Mhe. Sangu amepongeza Chama cha Waajiri Tanzania (ATE) kwa kuingia makubaliano na NSSF akieleza kuwa hatua hiyo itasaidia kuongeza uelewa na uzingatiaji wa sheria za kazi, hususan katika masuala ya kinga ya jamii, mishahara na utoaji wa ajira zenye staha.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Chama cha Waajiri Tanzania (ATE), Bw. Oscar Mgaya amesema mkakati mpya wa miaka mitano wa chama hicho unalenga kuimarisha uwezo wa waajiri kuboresha huduma kwa wanachama na kuongeza mchango wa sekta binafsi katika maendeleo ya taifa ili kufikia malengo ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

“Waajiri ni nguzo muhimu katika kukuza uchumi, kuongeza ajira zenye staha na kuchangia mapato ya Serikali, hivyo ushirikiano kati ya Serikali, Waajiri na Wafanyakazi utaendelea kuimarishwa kupitia majadiliano ya kijamii yenye tija ili kutatua changamoto za maeneo ya kazi kwa wakati,” amesema Mgaya.

Naye Katibu Mkuu wa Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi Tanzania (TUCTA), Bw. Hery Mkunda amesema TUCTA na ATE zimeendelea kushirikiana katika kutekeleza miradi mbalimbali yenye lengo la kuongeza tija kwa wafanyakazi na waajiri. 

Miongoni mwa miradi hiyo ni programu za ukuzaji ujuzi na uanzishwaji wa kituo kinachotoa taarifa sahihi na huduma kwa Watanzania wanaokwenda kufanya kazi nje ya nchi pamoja na raia wa kigeni wanaokuja kufanya kazi nchini.

Mkunda amewakumbusha  waajiri kuendelea kuimarisha ushirikiano na wafanyakazi kwa kuwashirikisha katika masuala ya maeneo ya kazi na kuondoa dhana kwamba wafanyakazi ni wapinzani wa waajiri. 

Katika hatua nyingine Mkurugenzi wa Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii (NSSF) Bw. Masha Mshomba akizungumza mara baada ya kusaini hati ya makubaliano ya ushirikiano wa taasisi yake na ATE amesema utaongeza wigo mpana wa kufanikisha shughuli za NSSF ikiwa ni mkakati wa kuanza kutekeleza Dira ya 2050 kupitia wigo wa hifadhi ya jamii.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundeblog@gmail.com