Na Sumai Salum – Kishapu
Halmashauri ya Wilaya ya Kishapu mkoani Shinyanga imetenga makisio ya bajeti ya Shilingi bilioni 36.849,308,000.00 mwaka wa fedha 2026/2027 kwa ajili ya kuboresha maslahi ya watumishi wa umma na kuongeza ufanisi wa utoaji wa huduma kwa wananchi, hatua inayolenga kujenga ari ya kazi, uwajibikaji na utendaji bora katika ngazi zote za Halmashauri.
Hayo yameelezwa Februari 3, 2026 wakati wa Baraza la Wafanyakazi la Halmashauri ya Wilaya ya Kishapu lililofanyika katika Ukumbi wa Mikutano wa Halmashauri hiyo mkoani Shinyanga, likilenga kupitia utekelezaji wa majukumu ya kiutumishi, kujadili changamoto zilizopo na kuweka mwelekeo wa pamoja wa kuboresha utendaji na maslahi ya watumishi.
Akizungumza, Mwakilishi wa Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Kishapu, Mona Bitakwate, ambaye pia ni Mkuu wa Divisheni ya Utumishi na Rasilimali Watu pamoja na Mwenyekiti wa kikao hicho, amesema Baraza la Wafanyakazi ni chombo muhimu cha kisheria kinachosaidia kuimarisha mshikamano, uwazi na ushirikishwaji wa watumishi katika maamuzi ya maendeleo ya Halmashauri.
Amesisitiza kuwa ufanisi wa Halmashauri unategemea kwa kiasi kikubwa nidhamu, maadili ya kazi, ushirikiano na uwajibikaji wa watumishi wake, huku akibainisha kuwa Menejimenti itaendelea kushughulikia haki, stahiki na madai ya watumishi kwa kuzingatia sheria, kanuni na taratibu za utumishi wa umma.
Kwa upande wake, Katibu wa TALGU mkoani Shinyanga, Ally Bulolelo, amesema Baraza la Wafanyakazi ni jukwaa muhimu linalowapa watumishi fursa ya kutoa maoni, kujadili maslahi yao na kushiriki kikamilifu katika maamuzi yanayolenga kuboresha mazingira ya kazi na huduma kwa wananchi.
Bulolelo amewataka watumishi wa umma kufahamu haki, wajibu na mipaka yao kwa kuzingatia sheria na miongozo ya utumishi wa umma, huku akihimiza nidhamu, uaminifu na maadili ya kazi kama nguzo muhimu za kuongeza ufanisi kazini.
Naye Katibu wa TUGHE mkoani Shinyanga, Ramadhani Pangala, ameipongeza Halmashauri ya Wilaya ya Kishapu kwa kuwashirikisha vyama vya wafanyakazi katika upangaji wa bajeti, akisema hatua hiyo imewezesha kupatikana kwa bajeti inayojitosheleza na inayolenga moja kwa moja kutatua changamoto za watumishi.
“Kuwashirikisha vyama vya wafanyakazi ni jambo la msingi kwa kuwa ni wadau wakuu wa maendeleo mahali pa kazi. Watumishi wanapaswa kuwa na bidii na uzalendo wa kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi, kila mmoja kwa nafasi yake na kwa wakati, huku wakihudumia jamii inayowazunguka,” amesisitiza Pangala.
Kwa upande mwingine, Katibu wa Chama cha Walimu Tanzania (CWT) mkoa wa Shinyanga, Allen Shuhi, amesema bajeti hiyo imejikita katika kuboresha maslahi na mazingira ya kazi ya wafanyakazi wa umma, hali itakayochochea utendaji kazi mzuri na kuongeza tija katika utoaji wa huduma.
Akizungumza katika Baraza hilo, Mwakilishi wa Serikali, Mathias Balele, amesema makisio hayo ya bajeti ya Shilingi bilioni 36,849,308,000,00 zilizotengwa na Halmashauri ya Wilaya ya Kishapu kwa mwaka wa fedha 2026/2027 zimezingatia mahitaji halisi na ya msingi ya watumishi wa umma, akieleza kuwa endapo bajeti hiyo itaidhinishwa na Baraza la Madiwani, itasaidia kwa kiasi kikubwa kuboresha maslahi ya watumishi na kuongeza ufanisi wa kazi.
Balele amepongeza uongozi wa Halmashauri hiyo, akimtaja Mkurugenzi Johnson kuwa kiongozi bora na wa mfano mkoani Shinyanga kwa kuwajali watumishi na kushughulikia stahiki zao, huku akibainisha kuwa kutokana na ukomo wa mapato ya ndani, Serikali Kuu itashauriwa kusaidia Halmashauri kwa kulipa baadhi ya madai ya fedha za kujikimu kwa watumishi wapya kwa wakati ili kuongeza ari ya kazi.
Wajumbe wa Baraza hilo wameipongeza Menejimenti ya Halmashauri kwa kushughulikia masuala mbalimbali ya watumishi ikiwemo kupandishwa vyeo, kuthibitishwa kazini, kulipwa stahiki na madai mbalimbali pamoja na kuendelea kuboresha mazingira ya kazi.
Aidha, Baraza hilo limeipongeza Serikali ya Awamu ya Sita kwa kuendelea kutoa ajira katika kada mbalimbali, hatua inayotarajiwa kupunguza uhaba wa watumishi na kuongeza ufanisi wa utoaji wa huduma kwa wananchi.
Baraza la Wafanyakazi wa Halmashauri ya Wilaya ya Kishapu limehitimishwa kwa wito kwa watumishi kuendelea kufanya kazi kwa bidii, uaminifu na kuzingatia maadili ya utumishi wa umma, huku wakikumbushwa kuwa mshikamano, uwazi na haki kazini ni msingi wa maendeleo endelevu na huduma bora kwa wananchi.
Social Plugin