Habari Mpya

6/recent/ticker-posts

DC MASINDI ABARIKI UMOJA WA MAAFISA USAFIRISHAJI MCHONGOMANI KISHAPU


Mkuu wa Wilaya ya Kishapu mkoani Shinyanga, Mhe. Peter Masindi,akizungumza na maafisa usafirishaji wa kijiwe cha Mchongamani Wilayani humo walipokuwa kwenye hafla ya kula na kunywa ikiwa ni sehemu ya kuimarishana kiuchumi na kijamii Novemba 23,2025 katika viwanja vya Storm palace hotel

Na Sumai Salum – Kishapu

Mkuu wa Wilaya ya Kishapu mkoani Shinyanga, Mhe. Peter Masindi, amepongeza Umoja wa maafisa usafirishaji (Bodaboda)wa Kijiwe cha Mchongomani kwa kufanikisha mkutano wa pamoja wa kijamii uliolenga kujenga mshikamano, kusikilizana na kujadili changamoto zinazowakabili katika kazi zao za kila siku.

Tukio hilo limefanyika Novemba 23, 2025 katika uwanja wa Hoteli ya Storm Palace, iliyoko mtaa wa Mhunze ya Juu, ambapo waendesha bodaboda wamekutana kula, kunywa na kufurahi pamoja kama sehemu ya kuimarisha umoja na afya ya kijamii ndani ya kundi hilo.

Akizungumza katika hafla hiyo, Mhe. Masindi ameuita mkutano huo kuwa ni hatua yenye afya na chachu ya maendeleo kwa vijana hao, akisema kuwa umoja huo unajenga nidhamu, ushirikiano na hamasa ya kufanya kazi kwa uadilifu.

Amesema vijana hao wamekuwa mfano bora wa kuigwa kwani mbali na kujumuika kwa furaha, wameonesha uzalendo kwa kulitakia Taifa amani, wakitambua kuwa sekta ya usafirishaji ndiyo mhimili wanaoutegemea katika kujikwamua kiuchumi.

Katika hatua nyingine, hafla hiyo imewakutanisha wadau mbalimbali wa maendeleo pamoja na wafanyabiashara kutoka maeneo tofauti wilayani Kishapu, jambo lililowapa fursa za kujadiliana namna ya kuboresha huduma za usafirishaji na kuongeza tija katika shughuli zao, huku akishiriki kuwachangia Tsh.600,000 kwa kushirikiana na wadau wengine kwa lengo la kukuza mfuko wao.

Kauli ya Mwenyekiti wa Maafisa Usafirishaji

Akizungumza kwa niaba ya maafisa usafirishaji wa Mchongomani Mwenyekiti wa Umoja huo, Paul Sandu, amesema lengo la kukutana na kushiriki chakula pamoja ni kuimarisha undugu, kujenga heshima na kuongeza upendo baina yao.

“Tuliamua kukaa pamoja, kula na kufurahi kama familia moja kwa sababu tunatambua nguvu ya umoja. Hii ni nafasi ya kujengeana, kusikilizana na kutiana moyo katika kazi zetu. Tumefurahi kuwa pamoja, na tutafanya hivi mara kwa mara kwa ajili ya maendeleo yetu,” amesema.

Ameongeza kuwa kundi hilo linaendelea kujiimarisha katika mafunzo ya usalama barabani na kufuata Sheria bila shurti hivyo maafisa wa usalama Barabarani wanapaswa kuwaona kama wateja wao wa karibu na kufanya kazi pamoja kwa Upendo na kupeana elimu zaidi kwa lugha nzuri.










Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundeblog@gmail.com