Habari Mpya

6/recent/ticker-posts

CHAMA CHA SKAUTI TANZANIA CHAENDESHA MAFUNZO KWA VIONGOZI WA KANDA YA ZIWA



Na Michael Abel, Shinyanga

Chama cha Skauti Tanzania kimeendesha mafunzo maalumu kwa viongozi wa Skauti kutoka mikoa tisa ya Kanda ya Ziwa, ikiwemo Shinyanga, Tabora, Simiyu, Mwanza, Mara, Geita, Kagera, Kigoma na Katavi, kwa lengo la kuwajengea uwezo katika masuala ya utawala bora, uongozi, ukuaji wa wanachama na matumizi ya mfumo wa kidigitali wa kanzi data ya Skauti nchini.

Mafunzo hayo yamefanyika leo, Ijumaa Oktoba 17, 2025, katika Chuo cha Ualimu Shinyanga (SHYCOM), yakihudhuriwa na viongozi mbalimbali wa serikali, Jeshi la Polisi pamoja na Jeshi la Zimamoto na Uokoaji.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa mafunzo hayo, Kamishna wa Skauti Mkoa wa Shinyanga, Mussa Chama, amesema lengo ni kuwajengea viongozi hao misingi imara ya uzalendo, kujituma na uongozi wenye maadili, sambamba na kuhamasisha kila shule nchini kuwa na klabu za Skauti ili kukuza roho ya kujitolea kwa vijana.

“Tunataka kila kijana wa Kitanzania awe na moyo wa uzalendo na kujitolea. Kupitia Skauti, tunawajenga vijana kuwa viongozi bora wa kesho na raia wema wanaotumikia taifa lao kwa heshima na uadilifu,” amesema Chama.

Kwa upande wake, Kamishna Mkuu Msaidizi anayeshughulikia Utawala Bora Makao Makuu ya Skauti, Fredrick Nguma, amesema chama hicho kwa kushirikiana na wakuu wa shule kimeanza mikakati ya kuhakikisha kila shule inakuwa na angalau wanachama 100 wa Skauti, ikilinganishwa na wastani wa sasa wa wanachama 30 hadi 50 kwa shule.

“Tunataka kuona kila shule inakuwa na kikundi imara cha Skauti. Hii itasaidia kukuza nidhamu, ushirikiano na uongozi miongoni mwa wanafunzi,” amesisitiza Nguma.

Akitoa pongezi kwa chama hicho, Afisa kutoka Jeshi la Zimamoto na Uokoaji Mkoa wa Shinyanga, Geofrey Mwambungu, amesema Skauti wamekuwa msaada mkubwa katika matukio ya uokoaji na kutoa huduma za kijamii wakati wa majanga mbalimbali.

Aidha, Mjumbe wa Bodi ya Skauti Mkoa wa Shinyanga, ambaye pia ni askari polisi wa Kata ya Ukenyenge Wilaya ya Kishapu, Insp. Amini Mgata, kwa niaba ya Kamanda wa Polisi Mkoa wa Shinyanga SACP Janeth Magomi, amesema Jeshi la Polisi limeendelea kushirikiana kwa karibu na Skauti katika kuendesha kampeni za kupinga ukatili, kuhamasisha usalama wa jamii na kuzuia uhalifu mashuleni.

Akihitimisha mafunzo hayo kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Afisa Elimu Sekondari wa Mkoa, Samson Hango, ameipongeza Skauti Tanzania kwa kuanzisha mfumo wa kidigitali wa usajili wa wanachama ambao utarahisisha utunzaji wa takwimu na ufuatiliaji wa maendeleo ya vijana.

“Mfumo huu wa kidigitali ni hatua kubwa ya kimaendeleo. Unasaidia kujua idadi halisi ya wanachama, maeneo yao na shughuli wanazofanya. Hii ni njia sahihi ya kujenga uwajibikaji na uongozi bora katika chama,” amesema Hango.

Mafunzo hayo yamehitimishwa kwa washiriki kuahidi kuendeleza elimu waliyopata kwa viongozi na vijana wa Skauti katika mikoa yao, ikiwa ni sehemu ya mpango wa kitaifa wa kuimarisha uongozi na ushiriki wa vijana katika maendeleo ya jamii.

Afisa Elimu Sekondari wa Mkoa, Samson Hango akizungumza na viongozi hao wa skauti.





Kamishna wa Skauti Mkoa wa Shinyanga, Mussa Chama akizungumza mara baada ya mafunzo hayo.

Mjumbe wa Bodi ya Skauti Mkoa wa Shinyanga, ambaye pia ni askari polisi wa Kata ya Ukenyenge Wilaya ya Kishapu, Insp. Amini Mgata akizungumza.










Kaimu Mkuu wa Taasisi ya kuzuia na kupambana na Rushwa (TAKUKURU) Mkoa wa Shinyanga, Mwamba Masanja akizungumza wakati wa mafunzo hayo.

Mafunzo yakiendelea.

Kamishna Mkuu Msaidizi anayeshughulikia Utawala Bora Makao Makuu ya Skauti, Fredrick Nguma akizungumza wakati wa mafunzo hayo.



Afisa kutoka Jeshi la Zimamoto na Uokoaji Mkoa wa ShinyangaGeofrey Mwambungu akizungumza wakati wa mafunzo hayo.



Picha ya pamoja.

Picha ya pamoja.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundeblog@gmail.com