Habari Mpya

6/recent/ticker-posts

KATAMBI AKABIDHI MILIONI 5 KWA STAND UNITED, ATOA AHADI NYINGINE YA MILIONI 10 KWA MECHI YA MARUDIANO

 

Naibu Waziri wa Kazi, Ajira, Vijana na Wenye Ulemavu ambaye pia ni Mbunge wa Jimbo la Shinyanga Mjini, Mhe. Patrobas Katambi, ametimiza ahadi yake kwa kuikabidhi timu ya Stand United kiasi cha shilingi milioni tano (5,000,000/=), alizokuwa ameahidi iwapo timu hiyo ingeshinda mchezo wake wa awali dhidi ya Fountain Gate FC.

Licha ya Stand United kupoteza mchezo huo uliochezwa juzi, katika uwanja wa CCM Kambarage Mhe. Katambi ameonesha mfano wa kuigwa kwa kutimiza ahadi yake, ambapo amekabidhi fedha hizo kwa mlezi wa timu hiyo ambaye pia ni Mkuu wa Wilaya ya Shinyanga, Wakili Julius Mtatiro.

Akizungumza wakati wa kukabidhi fedha hizo, leo Julai 7, 2025 Mhe. Katambi amesema alitoa ahadi hiyo kama sehemu ya kuwahamasisha vijana kupambana na kuonesha ushindani, lakini pia kutambua juhudi na nia njema ya timu hiyo katika kuinua tasnia ya michezo mkoani Shinyanga.

Katika hatua nyingine, Mhe. Katambi ametangaza ahadi mpya ya kutoa shilingi Milioni Kumi (10,000,000/=) endapo Stand United itaibuka na ushindi katika mchezo wa marudiano dhidi ya Fountain Gate FC na kufanikisha kupanda Ligi Kuu ya NBC msimu ujao, huku akiwataka mashabiki wa soka mkoani humo kuendelea kuipa sapoti timu yao.

“Ninawaamini vijana wetu, naamini morali iko juu na watapambana kwenye mchezo wa marudiano, nipo hapa kama mbunge wa jimbo la Shinyanga Mjini kuwahamasisha na kuhakikisha ndoto ya kurejea Ligi Kuu inatimia,” amesema Mhe. Katambi.

Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Shinyanga na mlezi wa Stand United, Wakili Julius Mtatiro, amemshukuru Mhe. Patrobas Katambi kwa kuendelea kuwa bega kwa bega na timu hiyo, akisema mchango wake ni chachu ya maendeleo ya michezo mkoani humo, huku akiahidi kufanya vizuri katika mchezo unaofuata na kuhakikisha furaha ya wana Shinyanga inarejea kwa kurudi kushiriki kwenye ligi kuu Tanzania Bara. 


Naibu Waziri wa Kazi, Ajira, Vijana na Wenye Ulemavu ambaye pia ni Mbunge wa Jimbo la Shinyanga Mjini, Mhe. Patrobas Katambi akizungumza wakati wa makabidhiano hayo.



Mkuu wa Wilaya ya Shinyanga na mlezi wa Stand United, Wakili Julius Mtatiro akizungumza wakati wa makabidhiano hayo.

Naibu Waziri wa Kazi, Ajira, Vijana na Wenye Ulemavu ambaye pia ni Mbunge wa Jimbo la Shinyanga Mjini, Mhe. Patrobas Katambi akimkabidhi fedha taslimu Shilingi Milioni 5 Mkuu wa Wilaya ya Shinyanga na mlezi wa Stand United, Wakili Julius Mtatiro.




Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundeblog@gmail.com