Habari Mpya

6/recent/ticker-posts

TFS SHINYANGA YATOA ELIMU YA UOKOAJI WA UVAMIZI WA NYUKI KWA JESHI LA ZIMAMOTO NA UOKOAJI


Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) kupitia ofisi yake ya Wilaya ya Shinyanga, imetoa mafunzo maalum kwa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji juu ya namna bora ya kukabiliana na matukio ya uvamizi wa nyuki kwa lengo la kulinda maisha ya wananchi na wahanga wa mashambulizi hayo.

Mafunzo hayo yametolewa kufuatia kuongezeka kwa visa vya nyuki kuvamia makazi ya watu na kusababisha madhara mbalimbali ikiwemo majeraha na hata vifo, hali ambayo imeleta hofu kwa baadhi ya wakazi wa maeneo ya vijijini na mijini.

Akizungumza wakati wa kutoa elimu hiyo, Mtaalam wa masuala ya nyuki Barnabas Salun, ameeleza hatua sahihi za kufuata wanapokabiliana na matukio ya watu kushambuliwa na nyuki. na kusisitiza umuhimu wa kutumia vifaa vya kisasa vya kujikinga pamoja na kuchukua tahadhari ili kuokoa maisha bila kuweka maisha yao pia hatarini.

"Katika uokoaji wa tukio la nyuki, usalama wa mtaalamu wa uokoaji ni jambo la kwanza kuzingatia. Tumejifunza mbinu sahihi za kutumia vifaa, namna ya kutambua aina ya nyuki, na hatua za haraka za msaada kwa wahanga," amesema Salun.

Kwa upande wake, Afisa Uelimishaji kutoka TFS, Fanael Sumali, ametoa wito kwa wananchi kuacha tabia ya kufuga nyuki kiholela katika makazi ya watu, akisema kuwa kufanya hivyo ni kuhatarisha maisha ya watu wasiokuwa na uelewa wa masuala ya nyuki.

"Tunahimiza watu wafuge nyuki katika maeneo yaliyotengwa na kufuata taratibu za kitaalamu. Ufugaji holela unachochea migogoro kati ya binadamu na nyuki," alisema Sumali.

Wakizungumza mara baada ya kupatiwa elimu hiyo maafisa na askali wa jeshi la zimamoto na uokoaji Wilayani Shinyanga wakaeleza changamoto wanazokumbana nazo katika uokoaji wa matukio ya nyuki kushambulia watu huku wakiahidi kutumia elimu hiyo waliyoipata kuboresha huduma zao za uokoaji.

Afisa Mhifadhi Mwandamizi kutoka TFS Wilaya ya Shinyanga, Mhifadhi Fabiani Balele, amesema lengo la mafunzo hayo ni kuongeza uelewa na uwezo wa vikosi vya uokoaji katika kukabiliana na matukio ya nyuki, kutokana na ongezeko la matukio hayo katika maeneo mbalimbali.

"Tumeona umuhimu wa kushirikiana na taasisi nyingine kama zimamoto ili kwa pamoja tuweze kuhakikisha usalama wa jamii yetu dhidi ya majanga yanayosababishwa na nyuki, hasa kutokana na mabadiliko ya tabianchi na mwingiliano wa binadamu na maeneo ya asili ya nyuki," amesema Mhifadhi Fabiani Balele.

Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) kuhakikisha jamii inaishi kwa usalama sambamba na uhifadhi endelevu wa misitu na viumbe hai waliopo ndani yake.


Afisa Mhifadhi Mwandamizi kutoka TFS Wilaya ya Shinyanga, Mhifadhi Fabiani Balele akizungumza wakati wa utoaji wa mafunzo hayo.

Afisa Uelimishaji kutoka TFS, Fanael Sumali akizungumza kwenye mafunzo hayo.

Mafunzo yakiendelea.


Mtaalam wa masuala ya nyuki Barnabas Salun akiztoa elimu ya masuala ya nyuki kwa maafisa na askali wa zimamoto na uokoaji.
Baadhi ya maafisa na askali wa zimamoto na uokoaji walishiriki mafunzo hayo.
Picha ya Pamoja.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com