SWICA YAIINGIZIA SERIKALI DOLA ZA MAREKANI 2,773,000

 

Na. Beatus Maganja, Bungeni Dodoma 

Waziri wa Maliasili na Utalii Mhe. Angellah Jasmin Kairuki (Mb) amesema katika kuongeza mapato yatokanayo na shughuli za utalii, Wizara yake imefanikiwa kuanza utekelezaji wa Uwekezaji Mahiri kwenye Maeneo ya Wanyamapori (Special Wildlife Investment Concession Areas - SWICA) ambapo jumla ya Dola za Marekani 2,773,000 sawa na Shillingi bilioni 7.1 zimepatikana ikiwa ni ada ya vitalu zilizokusanywa tangu kusainiwa kwa mkataba tarehe 3 Januari, 2024.

 Ameyasema hayo leo Mei 31, 2024 Bungeni Dodoma akiwasilisha taarifa ya utekelezaji wa Mpango wa Bajeti ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025.

Mhe Kairuki amesema kupitia Uwekezaji huo Wizara yake inategemea kuongeza mapato kufikia Dola za Marekani millioni 312 sawa na wastani wa Dola za Marekani millioni 15.5 kwa mwaka.

Akizungumzia suala la uvunaji wa wanyamapori na masharti ya Mkataba wa CITES, Mhe. Kairuki amesema Tanzania imefanikiwa kuingia katika kundi la kwanza (Category I) la nchi wanachama zenye Sheria zinazotekeleza Mkataba wa CITES kikamilifu hatua inayotajwa kuiwezesha Tanzania kufanya biashara ya uwindaji wa kitalii na mataifa ambayo masharti ya kupokea nyara kutoka kwenye nchi ambazo Sheria zake ziko katika kundi la kwanza.

Katika kuhakikisha maeneo ya malikale yanaendelea kukidhi vigezo vya kimataifa na kuvutia watalii, Waziri Angellah Kairuki amesema Wizara ya Maliasili na Utalii imefanikiwa kupandisha hadhi Eneo la Magofu ya Kilwa Kisiwani na Songo Mnara, lenye hadhi ya Urithi wa Dunia kuwa miongoni mwa maeneo yenye mahusiano ya kisayansi kati ya binadamu na mazingira (Man and Biosphere Reserve).

Amesema hadhi hiyo imetolewa na UNESCO mwezi Julai, 2023 na hivyo kuongeza idadi ya maeneo yenye sifa hiyo kutoka 5 hadi 6  na hatua inayotajwa kuchochea shughuli za utalii wa malikale kwa kuongeza idadi ya watalii wa Kimataifa katika eneo la Magofu ya Kilwa Kisiwani na Songo Mnara hususani kupitia utalii wa meli.



Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post