DC KONGWA ATOA WITO KWA WADAU KUTUMIA NJIA MBALIMBALI KUSAMBAZA ELIMU KUHUSU SUMUKUVU





MKUU wa Wilaya ya Kongwa Mayeka Simon,akizungumza wakati wa hafla ya kufungua kikao cha mrejesho wa matokeo ya utafiti na mafunzo ya kupunguza sumukuvu katika mazao baada ya kuvuna kilichofanyika wilayani humo.

MAKAMU Mkuu wa Taasisi ya Afrika ya Sayansi na Teknolojia ya Nelson Mandela,Arusha Prof.Maulilio Kipanyula,akizungumza wakati wa hafla ya kufungua kikao cha mrejesho wa matokeo ya utafiti na mafunzo ya kupunguza sumukuvu katika mazao baada ya kuvuna kilichofanyika wilayani Kongwa.


MKURUGENZI Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Kongwa Dkt.Omary Nkullo,akizungumza wakati wa hafla ya kufungua kikao cha mrejesho wa matokeo ya utafiti na mafunzo ya kupunguza sumukuvu katika mazao baada ya kuvuna kilichofanyika wilayani Kongwa.


BAADHI ya washiriki wakimsikiliza Mkuu wa Wilaya ya Kongwa Mayeka Simon (hayupo pichani),akizungumza wakati wa hafla ya kufungua kikao cha mrejesho wa matokeo ya utafiti na mafunzo ya kupunguza sumukuvu katika mazao baada ya kuvuna.


MKUU wa Wilaya ya Kongwa Mayeka Simon,akiwa katika picha ya pamoja mara baada ya kufungua kikao cha mrejesho wa matokeo ya utafiti na mafunzo ya kupunguza sumukuvu katika mazao baada ya kuvuna.

Na.Alex Sonna-KONGWA

MKUU wa Wilaya ya Kongwa Mayeka Simon ametoa wito kwa wadau kutumia njia mbalimbali kusambaza elimu kuhusu sumukuvu kwa wakulima, walaji na wadau wengine katika sekta ya chakula na lishe.

Kauli hiyo ameitoa wilayani Kongwa wakati wa hafla ya kufungua kikao cha mrejesho wa matokeo ya utafiti na mafunzo ya kupunguza sumukuvu katika mazao baada ya kuvuna.

Amesema inaweza kujumuisha uandishi wa machapisho, semina, mikutano ya kikanda, na hata matumizi ya teknolojia kama vile simu za mkononi na mitandao ya kijamii na vyombo mbalimbali vya habari zikiwemo runinga, radio na magazeti ili kufikisha ujumbe kwa haraka na kwa ufanisi zaidi.

kwa upande wa Halmashauri na Wizara ya Kilimo ,amesema uandaliwe mkakati wa maksudi wa kuhakikisha kuwa mapendekezo yote yaliyotokana na tafiti yanafanyiwa kazi kwa ukamilifu.
"Hii inaweza kujumuisha kufanya mabadiliko katika kanuni za kilimo, kuwekeza zaidi katika miundombinu ya kuhifadhi mazao, kuandaa vyakula ili kupunguza hatari ya sumukuvu, na hata kuimarisha mifumo ya udhibiti na ukaguzi ili kuhakikisha viwango vya usalama wa chakula vinazingatiwa,"amesema Mhe.Simon

Hata hivyo amesema kupitia utafiti wa Sumukuvu wameweza kubaini kaya nyingi katika Wilaya ya Kongwa na kwingineko zinategemea nafaka aina ya mahindi na karanga kama sehemu kuu ya uji wa watoto wadogo na ugali ambao ni chakula kikuu cha familia.

Mhe.Simon amesema amefarijika kuona matokeo ya tafiti zilizofanywa katika kipindi cha miaka michache zililenga kuelewa vizuri zaidi madhara ya sumukuvu.

Amesema kupitia tafiti hizo, wameweza kubaini kuwa, kaya nyingi katika Wilaya ya Kongwa na kwingineko zinategemea nafaka aina ya mahindi na karanga kama sehemu kuu ya uji wa watoto wadogo na ugali ambao ni chakula kikuu cha familia.

" Kwa bahati mbaya mazao haya yanashambuliwa zaidi na kuvu wazalishao sumukuvu endapo mbinu bora za kilimo, uhifadhi na uandaaji wa chakula zisipozingatiwa kikamilifu,"amesema

Hata hivyo amesema pamoja na changamoto ya mazao kushambuliwa na kuvu, kupitia tafiti hizo watafiti wameainisha kwamba, athari zinazoweza kusababishwa na sumukuvu zinaweza kupunguzwa kwa kuzingatia mbinu bora za kilimo na uhifadhi mazao baada ya kuvuna.

Vile vile mbinu bora za kuandaa nafaka hizi kabla ya kupika zinaweza kupunguza sumukuvu endapo zitafanywa kwa ufanisi.


Kwa upande wake Makamu Mkuu wa Taasisi ya Afrika ya Sayansi na Teknolojia ya Nelson Mandela,Arusha Prof.Maulilio Kipanyula, amesema kuwa uchambuzi wa matokeo ya utafiti kuhusu sumukuvu umebaini mambo manne.

Prof.Kipanyula ameyataja mambo hayo ni kaya nyingi kutegemea mahindi na karanga kama chakula
kikuu cha watoto wadogo na familia ikifuatiwa na mtama, ulezi na uwele.

Pia,Vyakula hivyo vina kiwango cha virutubisho vinavyohitajika kuupa mwili nguvu (energy), proteini na mafuta (lipid); vina nusu ya kiwango kinachohitajika cha madini ya calcium na Vitamini A, na upungufu mkubwa wa madini chuma (iron) na zinc.

Amesema pia matokeo hayo yamebaini mahindi na karanga zinashambuliwa na sumukuvu zaidi kuliko nafaka nyingine.

" Viashiria vya uwepo wa sumukuvu kwenye sampuli za kibaolojia kama vile damu na mkojo, hali hii anaashiria uwezekano wa watoto na jamii kuwa katika hatari ya kupata madhara yanayosababishwanasumukuvu,"amesema Prof Kipanyula.

Amesema maandalizi ya awali ya mradi yalianza mwaka 2015 na kufuatiwa na awamu ya utekelezaji mwaka 2017.

"Mradi huu ulifanikiwa kufikia kaya zipatazo 2,874 katika Halmashauri ya Wilaya ya Kongwa;watoa huduma ya afya ya Baba, Mama na Mtoto wapatao 52 kutoka katika vituo vyote vya kutolea huduma za afya ndani ya Wilaya ya Kongwa,"amesema

Pia umewafikia watoa wahudumu wa Afya ngazi ya jamii 104,ambapo jumla ya kaya zilizofikiwa moja kwa moja na mradi huo kuwa 3,030 sawa na idadi ya watu 14,370.

Amesema Matokeo ya utafiti uliofanywa na mradi MMT yanaendana kwa kiasi kikubwa na yale ya tafiti nyingine zilizofanywa na wanazuoni wengine ambazo pia zilibaini uwepo wa tatizo la sumukuvu kwenye mazao katika maeneo ya Wilaya ya Kongwa.

"Na hivyo kuathiri ubora wake kwa matumizi ya chakula cha binadamu na mifugo. Kama nilivyoanza kusema lengo la mkutano huu ni kuleta mrejesho wa matokeo ya utafiti wetu.

"Sambamba na hilo tumeona ni vyema kuandaa mafunzo ya namna ya kudhibiti kuvu kushambulia nafaka baada ya kuvuna, na jinsi ya kupunguza sumukuvu kwenye nafaka ambazo tayari zimeshaathiriwa.

"Ni matumaini yetu kuwa kupitia mafunzo yatakayotolewa, jamii itapata uelewa wa namna ya kupambana na sumukuvu katika mazao ya chakula na hivyo kupunguza athari zake,"amesema Prof Kipanyula

Naye Msimamizi wa Mradi Prof.Neema Kassim amesema kuwa mradi huo umewafikia watu 3,000 tatu sababu ya washiriki wa mradi wapo 2874 ukijumlisha na wahudumu wa afya wanafikia hiyo idadi ya watu 3000 hawa ndo tulifawakia moja kwa moja kwa kuwafundisha na kuwapa kitendea kazi

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post