BABU TALE,ORYX WAGAWA MITUNGI YA GESI 800 KWA WANANCHI


Na Mwandishi Wetu,Ngengere

MBUNGE wa Jimbo la Morogoro Kusini Mashariki Hamis Taletale kwa kushirikiana na Kampuni ya Oryx Gas wamekabidhi mitungi ya gesi na majiko yake zaidi ya 800 kwa wananchi wa jimbo hilo.

Lengo la kukagawa mitungi hiyo ni sehemu ya muuendelezo wa kuunga mkono jitihada za Rais Dk.Samia Suluhu Hassan za kuhamasisha matumizi ya nishati safi ya kupikia.

Akizungumza wakati wa kukabidhiwa kwa mitungi hiyo kwa wananchi uliokwenda sambamba na utolewaji wa taarifa ya utekelezaji wa Ilani ya CCM katika Jimbo hilo,Makamu Mwenyekiti wa CCM Abdulurahman Kinana amesema kugawiwa kwa mitungi hiyo ni matokeo ya sera na ubunifu wa Rais Dk .Samia.

Amefafanua Rais Samia mwaka jana alianzisha mchakato wa kuwatua akina mama mzigo wa kuni kichwani kwa kuanzia kampeni ya nishati safi na salama.

"Kuna maelfu ya kinamama wamefariki kwasababu ya matumizi ya kuni na mkaa , Karibu watu 50000 kwa mwaka walikufa kwasababu ya matumizi ya nishati isiyo salama.

"Rais ameamua kwamba ianze kampeni ya kuhakikisha kila nyumba inatumia gesi na kinachofanyika leo ni sehemu ya kuunga mkono jitihada za Rais."

Ameongeza kuwa nchi yetu inaumri wa miaka 60 tangu ipate uhuru na katika miaka yote hiyo hakuna aliyefikiria kuwatua akina mama kuni kichwani lakini kwa Rais Samia hilo kimewezekana kutokana na jitihada zake za kuwapenda na kuwajali Watanzania na hasa wanawake.

Amesema katika harakati za nishati safi hivi karibuni Rais Samia alikuwa Mwenyekiti Mwenza katika Kongamano la kidunia la Nishati Safi ambalo lilifanyika nchini Ufaransa na kupitia Kongamano hilo Rais akitoa muelekeo kwa Bara la Afrika kuhusu nishati safi na kuunga mkono.

"Hivyo katika kufanikisha kampeni hii fedha nyingi zinahitajika na Serikali haitaweza kufanikisha kampeni hii peke yake ndio maana unaona wadau mbalimbali kama hawa wanashiriki katika kufanikisha kampeni ya nishati safi nchini,"amesema Kinana.

Kwa upande wake Meneja Masoko wa Oryx Gas Peter Ndomba amesema katika tukio hilo wameungana na Mbunge Taletale kugawa mitungi zaidi ya 800 kwa wananchi wa Ngerengere na Kata nyingine za jirani katika Jimbo hilo.

"Huu ni muendelezo wa shughuli zetu za kila siku tunazofanya katika kusaidia mitungi ya gesi katika maeneo mbalimbali na makundi mbalimbali na leo tumekuja hapa kuendeleza jitihada za kuunga mkono matumizi ya nishati safi yaliyopewa msukumo mkubwa na Rais Dk.Samia Suluhu Hassan,"amesema.

Pia amesema mbali ya kutoa mitungi hiyo,wametoa elimu ya sahihi kuhusu matumizi ya gesi na elimu hiyo wanaamini itakuwa ni muendelezo kwa familia zao na jamii nyingine yoyote na wanawasihi wafuate yote ili waendelee kutumia nishati hii kwa usalama.

Awali Mbunge wa Jimbo la Morogoro Kusini Mashariki Babu Tale amesema wanaishukuru Oryx Gas kwa kutoa mitungi hiyo ya gesi kwa wananchi ikiwa ni sehemu ya kufuata maelekezo ya Rais Samia ya kuhamasisha matumizi ya nishati safi

"Kwetu sisi jambo hili ni kubwa ,Wana Morogoro Kusini Mashariki tunatokea vijijini , tunaweza kukata mkaa wenyewe lakini kama leo hii tunaamua kukimbilia katika gesi hiki ni kitu.Nishauri huu ni wakati wa kutumia Oryx Gas ambayo ni gesi ya uhakika na ndio ambayo sisi tumeamua kuitumia.

Akifafanua amesema kilichomsukuma kushirikiana na Oryx Gas kugawa mitungi hiyo ni kuendelea kusimamia yale ambayo Rais Samia ameelekeza ya kutaka wasimamie nishati safi na hivyo anayofuraha kukabidhi mitungi ya oryx kwa wananchi 880."

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post