TSH. MILIONI 50 KUSHINDANIWA KATIKA SHINDANO LA STORIES OF CHANGE


Mkurugenzi Mtendaji wa JamiiForums, Maxence Melo na Mkurugenzi wa Uchechemuzi wa TWAWEZA, Annastazia Rugaba wakizungumza na Waandishi wa habari jijini Dar es salaam.

                                                        *****

Na Mwandishi wetu

Baada ya mafanikio ya Shindano la Uandishi la "Stories of Change" katika Mwaka 2021, 2022 na 2023, kwa mara nyingine JamiiForums inazindua Msimu mpya wa Shindano hilo kwa Mwaka 2024 kwa kushirikiana na Taasisi ya TWAWEZA.

Akifungua Msimu mpya, Mkurugenzi Mtendaji wa JamiiForums, Maxence Melo amesema Dhima ya Shindano la 'Stories of Change' (SoC) Mwaka 2024 ni "Tanzania Tuitakayo" ikilenga kuhamasisha Wananchi kuibua mawazo mbadala ya nini kifanyike kuipata Tanzania iliyobora zaidi kwa kupendekeza mawazo bunifu.

Amefafanua kuwa Mawazo haya ni lazima yawe yale yanayoweza kutekelezeka ndani ya Miaka 5, 10, 15 hadi 25 ijayo na kuwa Shilingi Milioni 50 imetendwa kwa ajili ya washindi watakaoshiriki katika Shindano hilo linalotarajiwa kuanza Mei Mosi, 2024 hadi Juni 30, 2024.

Misimu iliyopita ya Shindano la 'Stories of Change' (SoC), takribani machapisho 6,000 yaliwasilishwa ndani ya JamiiForums.com kutoka kwa Wananchi.

Ameeleza kuwa Miongoni mwa Maudhui yaliyowasilishwa, yamechangia kuboresha Mifumo ya Utoaji wa Huduma katika Sekta ya Umma na Binafsi

Kwa Upande wa Mkurugenzi wa Uchechemuzi wa TWAWEZA, Annastazia Rugaba amesema moja kati ya kazi zao ni kuhakikisha Wananchi wanapaza sauti zao na zinatiwa maanani na Serikali kuanzia Serikali za Mtaa mpaka Serikali Kuu.

Ameongeza "Lakini pia kiu yetu kubwa ni kuona Serikali inatumikia Umma ambao ndo wamewaweka Madarakani. Na JamiiForums ni wadau wetu mkubwa wa muda mrefu ikiwemo hili la Stories of Change".

Ameeleza kuwa sehemu ya masharti ni kuwa andiko liwe na maneno kuanzia 700 na yasiyozidi 1,000 kwa lugha ya Kiswahili au Kiingereza.


Mkurugenzi wa Uchechemuzi wa TWAWEZA, Annastazia Rugaba akisisitiza jambo kwenye mkutano na waandishi wa habari jijini Dar es salaam juu ya Msimu mpya wa shindano la  'Stories of Change' (SoC) Mwaka 2024.


 
Mkurugenzi Mtendaji wa JamiiForums, Maxence Melo akisisitiza jambo kwenye mkutano na waandishi wa habari jijini Dar es salaam juu ya Msimu mpya wa shindano la  'Stories of Change' (SoC) Mwaka 2024.


Baadhi ya waandishi wa habari wakifuatilia mkutano kati ya   Mkurugenzi Mtendaji wa JamiiForums, Maxence Melo Mkurugenzi wa Uchechemuzi wa TWAWEZA, Annastazia Rugaba  juu ya Msimu mpya wa shindano la  'Stories of Change' (SoC) Mwaka 2024.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post