DK NCHIMBI: TUTAWAENZI WAASISI KWA KUENDELEZA UTUMISHI KWA WATU


Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) , Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi amezuru kaburi la Hayati Mzee Constantine Osward Millinga, aliyekuwa mmoja wa waasisi na wapigania uhuru kuanzia wakati wa Tanganyika African Association (TAA), Tanganyika African National Union (TANU), hadi CCM, katika makaburi ya familia yaliyopo, Mtaa wa Mhekela, Mbinga Mjini, mkoani Ruvuma, leo Jumatatu, Aprili 22, 2024.

Katibu Mkuu wa CCM Dk Nchimbi, na viongozi aliombatana nao katika msafara wa ziara yake mkoani humo, mbali ya kuweka shada ya maua, walipata nafasi ya kumsalimia Mjane wa Hayati Millinga, Bi. Maria Orign Mapunda (88), na kushiriki ibada ya kumuombea marehemu iliyoongozwa na Padri Andrea Silimbo.

Hayati Mzee Millinga ambaye alikuwa mmoja wa viongozi waandamizi wa TAA, TANU hadi CCM, akishirikiana na wenzake, wakiwemo viongozi wakuu na wanachama, wakiongozwa na Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, akiwa sehemu ya waasisi wa vyama hivyo vya ukombozi vilivyobeba chimbuko na kuweka misingi ya uhuru na maendeleo ya Tanganyika, baadaye kuipata Tanzania, na kuzaliwa kwa CCM, alifariki dunia Machi 5, 2018.

Akizungumza wakati wa kutoa salaam za pole kwa wanafamilia na wananchi wengine, Dk Nchimbi amesema Chama Cha Mapinduzi kitaendelea kuenzi na kujifunza kupitia mema yote yaliyofanywa na waasisi wake wa vyama vya TANU na ASP, ikiwa ni sehemu ya njia ya kuendelea kulijenga Taifa letu kwa misingi imara ya kisiasa, uchumi na kuimarisha umoja na mshikamano wa kitaifa.

Dk Nchimbi aliambatana na Katibu wa NEC - Oganaizesheni Ndugu Issa Haju Gavu na Katibu wa NEC - Itikadi, Uenezi na Mafunzo wa CCM Taifa Ndugu Amos Makalla.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post