BODI YA CAMARTEC YATEMBELEA KIWANDA DARASA CHA KUBANGUA KOROSHO MANYONI


Na Ferdinand shayo ,Singida

Wajumbe wa Bodi ya Kituo cha Zana za Kilimo na Teknolojia Vijijini (CAMARTEC) wametembelea Kiwanda darasa cha Kubangua korosho kilichoanzishwa na kituo hicho Wilayani Manyoni Mkoani Singida kwa lengo la kuwasaidia Wakulima kubangua korosho zao na kuacha kuuza korosho ghafi kwa walanguzi na kushindwa kunufaika ipasavyo na kilimo hicho.

Wakizungumza mara baada ya kutembelea kiwanda hicho Wajumbe hao wakiongozwa na Mwenyekiti wa Bodi ya CAMARTEC Profesa Valerian Silayo amesema kuwa kiwanda hicho kimeanzishwa kwa lengo la kuwasaidia wakulima wasiuze korosho ghafi bali waongeze thamani korosho zao ili kupata manufaa Zaidi yanayotokana na kilimo hicho.


Profesa Silayo amepongeza uongozi wa Halmashauri ya Manyoni kwa kutoa eneo la ujenzi wa kiwanda darasa Pamoja na kulinda miundombinu ya kiwanda hicho ambacho ni mkombozi kwa wakulima wa korosho .

Kaimu Mkurugenzi wa CAMARTEC Mhandisi Paythias Ntella amesema kuwa kiwanda darasa kinatoa ni fursa kwa wakulima kujifunza teknolojia za kubangua korosho pamoja na vijana kujifunza kutumia teknolojia hizo ili kutengeneza kipato kwa kuongeza thamani zao la korosho.

Ntella ameipongeza serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Raisi Dr.Samia Suluhu Hassan kwa kuwezesha ujenzi wa kiwanda darasa Pamoja na Wizara ya Viwanda na Biashara .

Mwakilishi wa Mkuu wa Wilaya ya Manyoni Charles Mchembe amesema kuwa wakulima wa korosho wanapaswa kuchangamkia fursa ya kujipatia teknolojia zilizoko katika kiwanda hicho ili ziwasaidie kubangua korosho zao.

Meneja wa Tawi la Bodi ya Korosho Manyoni Ray Mtangi ameipongeza  CAMARTEC kwa kuanzisha kiwanda hicho kati kati ya Mashamba makubwa ya korosho ili kuwasogezea karibu wakulima huduma za ubanguaji wa korosho ambazo zitasaidia kupunguza uuzaji wa korosho ghafi kwa masoko ya ndani na nje ya nchi.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post