KATAMBI AUNGURUMA KITANGILI, "ENDELEENI KUTUAMINI VIONGOZI WENU"

Mbunge wa jimbo la Shinyanga Mjini Mhe. Patrobas Katambi amefanya mkutano wa hadhara uliowakutanisha wananchi na wakazi wa kata ya Kitangili manispaa ya Shinyanga.
Mkutano huo wa hadhara umefanyika leo Machi 13, 2024 katika ofisi ya mtendaji wa kata ya Kitangili manispaa ya Shinyanga.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa mkutano huo uliolenga  kusikiliza kero za wananchi wa eneo hilo pamoja na kuwafahamisha wananchi juu ya utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo iliyofanyika ndani ya kata yao diwani wa kata ya Kitangili Mariamu Nyangaka amesema katika kipindi cha miaka mitatu wamepokea Shilingi Bilioni 3 kwaajili ya utekelezaji wa shughuli za kimaendeleo hali ikiwemo ujenzi wa madaraja na madarasa.

"Ndani ya Serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Rais Samia Suluhu Hassan tumepokea fedha kwaajili ya ujenzi wa madaraja, barabara na madarasa na kupelekea kata ya kitangili kuondokana na baadhi ya changamoto ikiwemo madaraja mabovu na barabara korofi, haya yote ni kwa sababu ya ushirikiano mzuri wa Mheshimiwa Mbunge wetu Patrobasi Katambi pamoja na upendo wa Rais wetu mama Samia Suluhu Hassani kwa niaba ya wananchi wa kata ya kitangili nipende kumuahidi tutaendelea kuwa naye bega kwa bega na hatuta muangusha", amesema Nyangaka.

Kwa upande wake Mbunge wa Jimbo la Shinyanga Mjini Mheshimiwa Patrobas Katambi amewasihi wananchi kuendelea kuwaamini viongozi kuanzia ngazi ya vijiji hadi Rais ili waweze kukamilisha na kutekeleza miradi iliyopangwa kwenye kata hiyo.

"Miradi tulionayo ni mingi katika kata hii tunataka tupate kilomita za lami za kutosha kwenye barabara za kata hii pamoja na maendeleo mengine na ndiyo maana takribani milioni 61 nilizotoa kwenye kata zote zilizopo manispaa ya Shinyanga ili ziweze kusukuma gurudumu la maendeleo, jukumu langu ni kuleta fedha, na kukagua miradi inavyotekelezwa ili wananchi waweze kupata maendeleo, 

"Hivyo basi ni lazima tuchague viongozi wenye tija na uchu wa maendeleo kwenye kata zetu, endeleeni kutuamini viongozi wenu ili tuweze kufikia malengo tuliyojiwekea, tumeendelea kufanya maboresho kwenye sekta ya afya, elimu, barabara ndani ya Kata hii ya Kitangili na manispaa kwa ujumla", ameongeza Katambi.


Mbunge wa jimbo la Shinyanga Mjini Mheshimiwa Patrobas Katambi akizungumza na wananchi wa kata ya Kitangili wakati wa mkutano huo.

Baadhi ya wananchi waliojitokeza kushiriki mkutano huo.

Diwani kata ya Kitangili Mariamu Nyangaka akizungumza wakati wa mkutano huo.




















Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments