WAZIRI MAVUNDE ASHUHUDIA URUSHWAJI NDEGE NYUKI ANGANI





*Kusini kuchele, Utafiti wa Miamba na Madini wahamia Mtwara

*GST kufanya tafiti madini mkakati Mtwara

Waziri wa Madini Mhe. Anthony Mavunde ameshuhudia jaribio la urushwaji wa Ndege Nyuki (Drone) angani kwa ajili ya utafiti wa miamba na madini hususan madini ya Kinywe, Nikeli, chuma na titanium katika Kijiji cha Utimbe kata ya Lupaso wilayani ya Masasi mkoa wa Mtwara.

Waziri Mavunde ameshudia jaribio hilo leo Februari 23, 2024 baada ya kutembelea eneo linalofanyika utafiti huo kwa lengo la kukagua shughuli za utafiti zinazo endelea katika maeneo mbalimbali nchini ikiwa ni utekelezaji wa Vision 2030 "Madini ni Maisha na Utajiri".

Akizunguza katika eneo la utafiti, Waziri Mavunde amesema mpaka sasa Tanzania ina taarifa za kina za tafiti wa miamba na madini kwa asilimia 16 ambazo zimepelekea uwepo wa migodi mikubwa, ya kati na midogo hivyo amesisitiza kwamba nchi hiyo ikifanyiwa utafiti wa kina wa High Resolution Airborne Geophysical Survey wa angalau asilimia 50 ifikapo 2030  itasaidia ongezeko kubwa la uwekezaji katika Sekta ya Madini.

Aidha, Waziri Mavunde amesema Serikali ya Awamu ya Sita inayo ongozwa na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imedhamiria kwa dhati kuhakikisha inawasaidia wachimbaji wadogo wa madini kwa kuwapatia maeneo yenye taarifa za jiolojia ili wachimbe kwa faida na kuondokana na uchimbaji wa kubahatisha.

Awali, Waziri Mavunde alitembelea ofisi ya Chama cha Mapinduzi (CCM) na ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Mtwara kwa lengo la kupata taarifa za shughuli za madini zinazoendelea mkoani humo.

Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Mtwara Kanali Ahmed Abbas, ameipongeza Wizara ya Madini kwa kurusha Ndege Nyuki kwa ajili ya utafiti katika eneo lake na pia, amemuomba Waziri Mavunde kusaidia upatikanaji wa soko la madini ya Chumvi sambamba na kujengwa  Kiwanda cha kuchakata madini hayo mkoani humo.

Naye, Mtendaji Mkuu wa GST Dkt. Mussa Budeba amemshukuru Waziri Mavunde kwa kukubari kushiriki na kushuhudia jaribio la urushwaji wa Ndege Nyuki kwa lengo la kutafiti miamba na madini kwa kutumia teknolojia ya high resolution airborne geophysical survey katika kijiji cha Utimbe wilayani Masasi mkoa wa Mtwara.

Sambamba na hayo, Dkt. Budeba amesema GST inashirikiana na Kampuni za Tukutech Company Ltd kutoka Tanzania, Zanifi Enterprise Ltd kutoka Zambia na Radai OY kutoka nchini Finland kufanya tafiti za miamba na madini katika maeneo mbalimbali nchini kwa kurusha Ndege Nyuki angani kwa kutumia teknolojia ya High Resolution Airborne Geophysical Survey.

Katika hatua nyingine, Dkt. Budeba amesema Ndege Nyuki inauwezo wa kufanya uchunguzi wa madini na miamba katika eneo kubwa kwa haraka ambapo hupelekea kupungua kwa muda na gharama zinazohitajika katika tafiti ikilinganishwa na njia nyingine za utafiti.

Mpaka sasa majaribio ya utafiti wa high resolution airborne geophysical survey unaoendelea kufanyika mkoani Mtwara tayari umefanyika katika mikoa ya Dodoma, Shinyanga, Geita, Manyara na Lindi kwa lengo la kutekeleza dhana ya Vision 2030.

*#Vision2030MadininiMaishanaUtajir#*

*#UtafitiTanzania#*

*#GeologicalSurveyofTanzania#*


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post