MAFUNZO YA KUONGEZA UJUZI WA KUCHAKATA NA KUTENGENEZA BIDHAA ZA NGOZI YAZINDULIWA DIT - MWANZA


Balozi wa Indonesia nchini Mhe. Tri Yogo Jatmiko,  amefungua rasmi mafunzo ya kuongeza ujuzi wa kutengeneza bidhaa za ngozi kwa wajasiriamali kutoka sehemu mbalimbali nchini Tanzania.

Mafunzo hayo yanayoendeshwa kwa ushirikiano baina ya mataifa matatu ambayo ni Indonesia, Ujerumani na Tanzania lengo lake kubwa ni kukuza taaluma ya Ufundi Stadi kupitia teknolojia ya uchakataji na Utengenezaji wa bidhaa za ngozi.

Akifungua Mafunzo hayo Balozi Yogo amesema "Tanzania imejaaliwa kuwa na rasilimali nyingi na malighafi, hivyo kutokana na uhusiano huu wa kidiplomasia kati ya nchini hizi mbili tutasaidiana katika kuwapatia ujuzi wananchi kupitia sekta mbalimbali''. 

Aidha, Balozi Yogo ameongeza kuwa ziara ya hivi karibuni ya mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan nchini Indonesia imefungua milango mbalimbali ya ushirikiano katika nyanja mbalimbali na hii imetokana na mataifa haya kuwa na historia zinazofanana.

Naye mkurugenzi wa kampasi ya Mwanza, Dkt. Albert Mmari akitoa neno la ukaribisho kwa wageni wote, ameshukuru ujumbe wa Indonesia na Ujerumani (GIZ) na kuomba ushirikiano huu uendelee kwa manufaa ya kukuza Stadi ya Ufundi Kwa mataifa yote hayo.

Kwa upande wake Mwl. Marco  Isack, Afisa Elimu, Halmashauri ya Manispaa ya Ilemela akimwakilisha Mkuu wa Wilaya ya Ilemela Mhe. Hassan Masala, ameishukuru serikali ya Indonesia kwa kuleta wataalam wa kufundisha teknolojia mpya ya uchakataji na Utengenezaji wa bidhaa za ngozi huku, Mratibu wa Mafunzo haya upande wa DIT Bwana Ramadani Buthu akibainisha kuwa wajasiliamali waliofika watapata ujuzi na watakuwa chachu ya kukuza teknolojia hii nchini.

Baadhi ya wajasiliamali waliofika katika mafunzo hayo wameahidi kutumia  ujuzi huo wa teknolojia mpya katika kuboresha bidhaa zao.

Mafunzo haya yatakayo dumu kwa muda wa  wiki mbili yamehusisha wajasiliamali kutoka mkoa wa Arusha, Dar es Salaam, Geita, Kagera, Kilimanjaro na Mwanza na lengo kubwa la DIT ni kusimamia mafunzo haya ili kuongeza ubora wa bidhaa za ngozi zinazozalishwa hapa nchini.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post