MBUNGE MTATURU : HATUNA DENI NA RAIS SAMIA


MBUNGE wa Singida Mashariki Miraji Mtaturu amekagua ujenzi wa daraja litakalounganisha vijiji vya Lighwa na Ujare vilivyopo kata ya Lighwa ambalo kukamilika kwake kutaondoa changamoto ya kukatika kwa mawasiliano kipindi cha mvua.

Daraja hilo pamoja na barabara za maingilio linajengwa kwa thamani ya Shilingi Milioni 222.9.

Akikagua daraja hilo Januari 4,2024,Mtaturu amemshukuru Rais Samia Suluhu Hassan kwa kuridhia fedha za miradi mingi jimboni humo ikiwemo ujenzi wa daraja hilo na mnara wa simu unaoendelea kujengwa katika Kijiji cha Lighwa.

"Mto huu ulikuwa changamoto kipindi cha masika kutokana na kukatika kwa mawasiliano na hivyo kupelekea wananchi kukosa huduma ndani ya Kata ikiwemo wanafunzi wanaosoma Shule ya Sekondari ya Lighwa,

"Namshukuru Rais wetu kwa kutuona kwa jicho la pekee,hapa Singida Mashariki tumepokea fedha nyingi za miradi mbalimbali,kwa niaba ya wananchi wa Singida Mashariki wamenituma nipeleke salaam na shukrani kwa Rais Dkt Samia Suluhu Hassan kwa kuridhia fedha za miradi mingi,"amesema Mtaturu.

Kwa upande wake Diwani wa Kata ya Lighwa Gabriel Mukhandi amemshukuru Mbunge Mtaturu kwa kuendelea kuwapigania bungeni na hatimaye serikali kuwatengea fedha.

"Tunathamini sana jitihada zako mbunge wetu,na ndio maana serikali inaendelea kutuletea fedha kwenye miradi mingi ya maendeleo jimboni kwetu,sisi wananchi tunajivunia sana uwakilishi wako,"amesema diwani huyo.

#SingidaMashariki#SSH2025#

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post