OFISI YA WAZIRI MKUU YAKABIDHI MISAADA YA KIBINADAMU MKOANI KAGERA.


Mkuu wa Mkoa wa Kagera Fatma Mwasa ( katikati) akikabidhi misaada ya kibinadamu kwa baadhi ya wananchi  Wilaya ya Bukoba vilivyotolewa na Idara ya Menejimeti ya Maafa Ofisi ya Waziri Mkuu baada ya bweni la shule hiyo kuungua moto Tarehe 22 Oktoba 2023.
Mkurugenzi Msaidizi Afya oja kupitia Idara ya Menejimenti ya Maafa Ofisi ya Waziri Mkuu, Dkt. Salum  Manyatta akizungumza na Wakazi wa Halmashauri ya Manispaa ya  Muleba mkoani Kagera wakati wa kukabidhi misaada ya kibinadamu baada ya kupata maafa yaliyotokana na mvua zinazoendelea kunyesha mkoani humo.

Baadhi ya Wakazi wa Halmashauri ya  Manispaa ya  Muleba mkoani Kagera wakisikiliza kikao  wakati wa kukabidhiwa misaada ya kibinadamu  iliyotolewa na Ofisi ya Waziri Mkuu baada ya kupata maafa yaliyotokana na mvua zinazoendelea kunyesha mkoani humo.

Mkuu wa Mkoa wa Kagera Mhe. Fatma Mwasa akizungumza na Wanafunzi wa Shule ya Sekondari ya Wasichana ya Omumwani  na wanafunzi waya Sekondari ya wavulana ya Ikungo alipofika shuleni hapo wakati wa kukabidhi misaada ya kibinadamu iliyotolewa na Idara ya Menejimeti ya Maafa Ofisi ya Waziri Mkuu baada ya bweni la shule hiyo kuungua moto Tarehe 22 Oktoba 2023.


Na Devotha Songorwa, Kagera

Ofisi ya Waziri Mkuu kupitia Idara ya Menejimenti ya Maafa imekabidhi misaada ya kibinadamu  kwa shule ya wasichana ya kidato cha tano na sita Omumwani  waliopata janga la kuunguliwa na mabweni tarehe 22 Octoba,2023 pamoja na wakazi wa Kata ya Karimbi ambao nyumba zao ziliezuliwa na upepo na mazao kuharibiwa kutokana na mvua zinazoendelea kunyesha mkoani Kagera.

Akizungumza wakati  wa kukabidhi vifaa hivyo kwa Mkuu wa Mkoa huo Mhe. Fatma, Mkurugenzi  Msaidizi Afya Moja kupitia Idara ya Menejimenti ya Maafa Ofisi ya Waziri Mkuu, Dkt. Salum  Manyatta alisema wamekabidhi Magodoro 60, Blanketi 60, jumla ya Ndoo lita 10, 120, vyandarua 60, sahani 60, vikombe 60 na sabuni vipande 553 kwa shule hiyo iliyopo Halmasahuri ya Manispaa ya Bukoba.

Ameongeza kuwa vifaa hivyo vya msaada wa kibinadamu vimetolewa pia kwa wakazi  wa Halmashauri ya Wilaya ya Muleba ambavyo ni  Mahindi tani 23.16, magodoro 150, Blanketi 150, Mikeka 150, Vyandarua 150, Sahani 150, Madumu ya maji ya 150 na  sabuni maboksi 5.

“Timu yetu ya Ofisi ya Waziri Mkuu ilishirikiana na wataalam kutoka ofisi ya Wilaya na Mkoa tumefanya tathmini pamoja na wataalam wengine kutoka Kata hii ya Karimbini kazi kubwa imefanyika kuhakikisha wananchi wanarudi katika hali ya kawaida hivyo nitumie nafasi hiyo kuwapa pole kwa maafa yaliyowapata tutaendeela kuwa nanyi wakati wote,”Amesema.

Pia ameeleza kuwa msaada huo wa kibinadamu ni jitihada ya kuunga mkono Serikali ya Mkoa wa Kagera kwa hatua za haraka zilizochukuliwa mara tu baada ya janga hilo kutokea.

Awali Mkurugenzi wa Halmashauri ya  Manispaa ya Bukoba Bw.  Hamid Njovu, alisema mabweni yaliyoathirika ni matatu ambapo bweni moja kati ya hayo lenye wanafunzi 62 liliteketea lote na mali zote za wanafunzi ziliteketea.

“Mabweni mengine mawili ya jirani yalipata nyufa kubwa zinazohitaji ukarabati mkubwa zenye wanafunzi 248 ambao kwa sasa wamechanganywa kwenye mabweni mengine ambayo hayakuathirika nitumie fursa hii kumshukuru Mhe. Kassim Majaliwa  Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muugano wa Tazania kupitia Idara ya Maafa kwa kufika na kutoa faraja kwa wanafunzi waliopatwa na janga la moto,” Alieleza Bw. Njovu.

Naye Mkuu wa Wilaya ya Muleba  Mhe. Dkt. Abel Nyamuhanga alibainisha kwamba msaada huo utagawiwa kwa kuzingatia tathmini iliyofanyika bila upendeleo kama sehemu ya kurejesha hali bila kusahau watu wenye ulemavu, wazee na kaya masikini.

Aidha Mkuu wa Mkoa wa Kagera Mhe.  Hajath  Fatma  Mwasa alisema Serikali itaendelea kutoa fedha kuhakikisha miundombinu mizuri ya shule inajengwa ili wanafunzi waweze kusoma katika mazingira mazuri na kutimiza ndoto zao huku akiwahimiza wakazi wa Muleba kutumia vizuri msaada huo katika wakati huu ambapo wanaendelea kurejesha hali zao.

 

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post