BARAZA HURU LA USULUHISHI LATOA MAFUNZO KWA WAANDISHI WA HABARI KUHUSU SHUGHULI ZA KUSHUGHULIKIA MALALAMIKO YA UKIUKWAJI WA HAKI ZA BINADAMU MGODI WA ALMASI MWADUI

 


Mtaalamu wa Jopo huru ambaye ni Mwanasheria katika Baraza huru la usuluhishi (IGM) Natujwa Mvungi akitoa mafunzo ya Baraza hilo.

Na Marco Maduhu, SHINYANGA

BARAZA huru la usuluhishi( Independent Grievance Mechanism IGM) limetoa mafunzo kwa Waandishi wa Habari Mkoani Shinyanga, kufahamu shughuli zao ambazo wanazifanya za kushugulikia malalamiko ya ukiukwaji wa haki za binadamu katika Mgodi wa Almasi Mwadui.

Mafunzo hayo yametolewa leo Novemba 22, 2023 kwa kuelezewa Shughuli za Baraza hilo na Mafanikio ambayo wamefikia na Changamoto zake.
Mtaalamu wa Jopo huru ambaye ni Mwanasheria katika Baraza huru la usuluhishi (IGM) Natujwa Mvungi, amesema baraza hilo ni chombo huru kisicho cha kimahakama, ambacho kilianzishwa kwa ajili ya kushughulikia malalamiko ya ukiukwaji mkubwa wa haki za binadamu unaodaiwa kufanyika katika Mgodi wa Almasi Mwadui.

Amesema Baraza hilo liliamza rasmi kufanya kazi Novemba 2022 kufuatia makubaliano yaliyofikiwa kati ya Kampuni ya Petra Diamond Limited na Kampuni ya Kiwakili ya Leigh Day, kwamba pamoja na mambo mengine makubaliano hayo yalihusu kuanzishwa na kutekelezwa kwa mfumo huru usio wa Kimahakama kushughulikia malalamiko yanayohusu uvunjifu mkubwa wa haki za binadamu ambao unahusishwa na utendaji wa Makampuni ya ulinzi ya Mgodi wa Mwadui.
“Baraza huru limeundwa kufuatia miongozo ya msingi wa Umoja wa Mataifa juu ya Biashara ya Haki za Binadamu (UN Guiding Principles On Bussiness and Human Right UNGP) kwa kuzingatia vigezo na ufanisi(Effectives Criteria), na kuhakikisha linatekeleza majukumu yake kikamilifu bila ya kuathiriwa na Mgodi,”amesema Mvungi.

Amesema Malalamiko ya ukiukwaji wa haki za binadamu ambayo wanayashughulikia ni kuanzia kipindi cha mwaka 2009 hadi 2021, na kwamba Baraza hilo litafanya kazi kwa kipindi cha miezi 24 tangu kuanziswa kwake mwaka jana na baada ya hapo litavunjwa.

Aidha, ametaja idadi ya Malalamiko ya ukiukwaji wa haki za binadamu ambayo wameyapokea tangu kuanzishwa kwa baraza hilo Novemba mwaka jana, kuwa ni 5,573 ambayo yanatoka kwa Wananchi katika vijiji 12 vinayozungumza Mgodi wa Mwadui.
Amesema Malalamiko hayo yanahusu kupigwa, kuumwa na Mbwa, Kubakwa,Vifo, watu kupotea, na Uharibifu wa mali, na kwamba hadi kufikia Novemba mwaka huu wamesajili malalamiko 840, na Kati ya hayo 296 yalishapatiwa maamuzi, 375 bado yanaendelea kufanyiwa uchunguzi, 127 yalikuwa nje ya wigo na 108 yalikidhi kizingiti huku 188 hayakukidhi kigezo cha ushahidi.

Katika hatua nyingine ametaja Changamoto ambazo wanakumbana nazo, kuwa ni Uelewa hafifu wa walalamikaji, ukosefu wa ushahidi na ukweli kwa malalamiko yaliyowasilishwa, na udanganyifu wa taarifa sahihi wa malalamiko yanayoletwa kwenye Baraza.
Paul Mikongoti kutoka Baraza hilo huru la usuluhishi, amesema wamekutana na Waandishi wa habari ili kufahamu shughuli zao, na wanapokuwa wakiandika habara waandike habari kwa usahihi na kuelimisha umma na kusaidia kupata haki zao.

Mwenyekiti wa Klabu ya Waandishi wa habari Mkoani Shinyanga Greyson Kakuru, akizungumza kwa niaba ya Waandishi wa habari mkoani humo, ameshukuru kupewa elimu ya kufahamu majukumu ya baraza hilo huru la usuluhishi.
Mtaalamu wa Jopo huru ambaye ni Mwanasheria katika Baraza huru la usuluhishi (IGM) Natujwa Mvungi akitoa mafunzo ya Baraza hilo.
Paul Mikongoti kutoka Baraza huru la usuluhishi akizungumza kwenye mafunzo hayo.
Mwenyekiti wa Klabu ya Waandishi wa Habari Mkoa wa Shinyanga Greyson Kakuru akizungumza kwenye mafunzo hayo.
Waandishi wa habari wakiwa kwenye mafunzo ya Baraza huru za usuluhishi.
Mafunzo yakiendelea.
Mafunzo yakiendelea.
Mafunzo yakiendelea.
Mafunzo yakiendelea.
Mafunzo yakiendelea.
Mafunzo yakiendelea.
Waandishi wa habari wakiwa kwenye mafunzo ya Baraza huru la usuluhishi.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post