KAMATI YA BUNGE YATEMBELEA MTAMBO WA KUZALISHA MAJI WAMI


Kamati ya Kudumu ya Bunge Uwekezaji na Mitaji ya Umma imeipongeza Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Dar es Salaam (DAWASA) kwa kuendelea kutekeleza miradi ya maji katika maeneo mbalimbali katika Mkoa wa Dar es Salaam na Pwani.

Pongezi hizo zimetolewa Novemba 12, 2023 na Mwenyekiti wa Kamati hiyo Mhe. Deo Sangu (Mb) wakati wa ziara ya kutembelea utekelezaji wa mradi wa maji Chalinze awamu ya tatu unaohusisha upanuzi wa Mtambo wa kuzalisha maji wa Wami.

Mhe.Sangu amesema kuwa DAWASA inafanya kazi kubwa ya kuhakikisha huduma ya majisafi inapatikana kwa wananchi wote, kwa kutumia mapato ya makusanyo ya ndani hivyo basi wataendelea kuisaidia kupata fedha za kusambaza huduma ya majisafi kwa wananchi wa maeneo yote ya Dar es Salaam na Pwani.

Aidha amesema kuwa, mojawapo ya maazimio ambayo Kamati imetoa kwa Serikali kwa ajili ya utekelezaji ni pamoja na kuhakikisha madeni ya Taasisi za Serikali zinadaiwa na DAWASA zinalipwa ili kasi ya maboresho ya huduma za maji iendelee kwa kasi ili kuongeza nguvu katika utoaji wa huduma ya majisafi kwa wananchi wote.

"Madeni ya maji ya taasisi yaweze kulipwa ili kazi ya kusambaza maji kwa wananchi kupitia miradi mikubwa kama huu wa Chalinze awamu ya tatu iweze kuleta tija kwa wananchi, tunaipongeza Menejimenti ya DAWASA kwa jitihada kubwa wanazofanya za kuhakikisha huduma ya maji inawafikia wananchi wote". Amesema

Kwa upande wake Kaimu Afisa Mtendaji Mkuu wa DAWASA Bw. Kiula Kingu amesema awamu hiyo ya tatu ambayo imegharimu Bilioni 83, mradi unahusisha upanuzi wa uwezo wa Mtambo wa Wami kutoka uzalishaji wa lita milioni 7.2 kwa siku hadi lita milioni 21.6 kwa siku.

Pamoja na hayo amesema kuwa , mradi umehusisha ujenzi wa matenki 18 ya kuhifadhi maji pamoja na ujenzi wa vioski 351 vya kuchotea maji ambavyo tayari vimekamilika.

"Mradi umelaza bomba la usamabazaji maji kwa umbali wa kilomita 826, na unalenga kunufaisha wakazi wa vijiji zaidi ya 56". Amesema

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post