WAZIRI MAVUNDE - TANZANIA KUKAA KWENYE RAMANI YA UCHUMI DUNIANI


 Na Mwandishi Maalum. 

Waziri wa Madini, Mhe. Anthony Mavunde amesema Mkutano wa Kimataifa wa Uwekezaji katika Sekta ya Madini unaotarajiwa kufanyika Oktoba 25 na 26 jijini Dar es Salaam utaiweka Tanzania katika ramani ya uchumi duniani. 

Ameyasema hayo, leo Oktoba 23, 2023 jijini Dar es Salaam wakati akizungumza katika kipindi cha runinga cha 360 kinachorushwa na kituo cha Clouds TV.

“Kupitia mkutano huu, tunakwenda kuiweka Tanzania katika ramani ya uchumi duniani, kwa kuwa ni fursa ya kipekee ya sisi kutangaza madini yetu na kuwavutia wawekezaji. Tunataka baada mkutano huu kumalizika Oktoba 26, 2023, dunia nzima iwe inazungumza kuhusu fursa iliyopo katika sekta ya madini Tanzania” amesema Mhe. Mavunde. 

Amesema Mkutano huo utasaidia kubadilishana uzoefu na mataifa yaliyofanikiwa zaidi kiuwekezaji katika rasilimali Madini lengo ni kuhakikisha Sekta ya Madini inaongeza zaidi mchango wake katika Pato la Taifa na uchumi kwa ujumla. 

Aidha, Mhe. Mavunde amesema kuwa Wizara ya Madini kwa kushirikiana na wadau kwa pamoja wamefanya maandalizi ya kutosha kuhakikisha mkutano huo unakuwa wenye hadhi ya kimataifa kwa kusudio la kukutana ana kwa ana na wadau wa sekta kutoka mataifa mbalimbali ili kubadilishana teknolojia na uzoefu katika sekta ya madini. 

Akizungumzia Maono 2030; Madini ni Maisha na Utajiri, Mhe. Mavunde  amesema kuwa ni maelekezo ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kuwasaidia wachimbaji wadogo kupitia utafiti wa kina wa miamba ili kuwe na taarifa za kutosha zinazohusu maeneo yenye rasilimali madini hapa nchini ili wasifanye shughuli za uchimbaji kwa kubahatisha. 

Ameongeza kuwa taarifa hizo za Jiosayansi zitakazokusanywa na Taasisi ya Jiolojia na Utafiti wa Madini Tanzania (GST) pia zitasadia kufungamanisha sekta zingine zikiwemo za Kilimo, Maji, Afya, Biashara pamoja na uchumi kwa ujumla. 


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post