STAMICO YASHUSHA NEEMA KWA WATU WENYE ULEMAVU

Na Dotto Kwilasa,Dodoma 

SHIRIKA la Madini la Taifa (STAMICO) limemwaga neema kwa watu wenye ulemavu nchini kupitia fursa ya uwakala na uuzaji wa mkaa mbadala wa Rafiki briquettes ambao ni rafiki wa mazingira utakasaidia kuunga mkono juhudi za serikali kukabilina na mabadiliko tabianchi.

Mkurugenzi wa Shirika la Foundation For Disabilities Hope (FDH) Michael Salali, amebainisha hayo leo Septemba 26 Jijini hapa wakati alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari kuhusu fursa hiyo.

Amesema shirika la STAMICO, limeanzisha utengenezaji wa mkaa mbadala ambao unafahamika kwa jina la Rafiki briquettes, ambapo watu wenye ulemavu watapatiwa fursa ya kuwa mawakala na wauzaji wa bidhaa hiyo.

“Tunalishukuru sana shirika la STAMICO kwa fursa hii kwa watu wenye ulemavu ambayo ianakwenda kusaidi kuwakwamua kiuchumi.

“Kama mnavyofahamu watu wenye ulemavu nchini uchumi wao bado ni duni sana hivyo fursa hii itasaidia kuboresha maisha yao na kuwaondolea changamoto ya unyanyapaa wanaokumbana nao katika jamii zao”amesema

Pia, amesema mkaa huo mbadala utasaidia kuendeleza juhudi za serikali na dunia kwa ujumla katika kukabilina na tatizo la mabadiliko tabia ya nchi yatokanayo na uharibifu wa mazingira utokanao na ukataji miti hovyo.

“Kama mnavyofahamu dunia ipo katika mapambano makali ya mabadiliko tabia nchi lakini pia uharibifu mazingira ambao unachangia watu wenye ulemavu wa ngozi kupata saratani ya ngozi kutokana na mionzi ya jua inayosababishwa na ukosefu wa vimvuli kutokana na ukataji miti kiholela unaendelea nchini”amesema

Aidha, ametoa wito kwa watu wenye ulemavu nchini kuchangamkia fursa hiyo adhimu ili kujikwamua kichumi na kuacha kuendelea kuwa tegemezi.


“Tunalishukuru sana shirika la STAMICO lakini pia serikali yetu ya awamu ya sita chini ya Rais Samia Suluhu Hassan kwa namna ambavyo anafungua fursa za kiuchumi kwa makundi mbalimbali ikiwemo kundi letu ka watu wenye ulemavu”amsema Salali


Mwisho

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post