MABADILIKO YA TABIA NCHI , SHUGHULI ZA KIBINADAMU ZAHATARISHA BWAWA LA NING'HWA

 

Na Mwandishi wetu - Shinyanga

Mkurugenzi Mtendaji wa Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Shinyanga(SHUWASA), Mhandisi Yusuph Katopola, amesema jitihada kubwa zinahitajika katika kutoa elimu juu ya umuhimu wa kutunza chanzo cha maji cha Bwawa la Ning'hwa katika Manispaa ya Shinyanga ambalo lipo hatarini kutoweka kutokana na shughuli za kibinadamu na mabadiliko ya tabia nchi.

Akizungumza wakati wa kutembelea Bwawa hilo linalozungukwa na Kata za Chibe, Pandagichiza na Old Shinyanga, Mhandisi Katopola amesema hali ya bwawa hilo ni mbaya kutokana na kupungua maji kwa kiasi kikubwa.

Amesema endapo hali hiyo itaendelea, basi watalazimika kuzima mitambo ya kusafisha majisafi yanayotumika katika Manispaa ya Shinyanga.

"Na hii inaweza kuwa sababu ya gharama za maji kuwa juu kwasababu tutakuwa tunatumia maji yote ya kununua kutoka KASHWASA tofauti na tunapotumia maji ya chanzo hiki mbadala," amesema Katopola.

Ametoa wito kwa wananchi kutunza chanzo hicho ili kuendelea kunufaika na huduma ya maji inayotolewa na Mamlaka hiyo.

Naye Msimamizi wa Bwawa la Ning'hwa kutoka Ofisi Ndogo za Bonde la Kati, Ninje Kashindye, amesema Bwawa hilo linahatarishwa zaidi na kilimo, uchungaji wa mifugo pamoja na uvuvi.

Amesema hivi sasa kina cha maji yaliyopo ni mita tano ambayo ni kidogo sana ikilinganishwa na uwezo wa Bwawa hilo.

Amesema licha ya jitihada za kutoa elimu na kuzuia shughuli hizo lakini wananchi wamekuwa wakikaidi na kuendelea na shughuli hizo.

Bwawa la Ning'hwa ni chanzo muhimu cha majisafi ambayo huzalishwa na kusambazwa katika Manispaa ya Shinyanga sambamba na vyanzo vingine vya maji kutoka Ziwa Victoria.

Bwawa hilo likiwa limejaa lina ujazo wa mita za ujazo Milioni 10.6 na mtambo wa kusafisha maji una uwezo wa kuzalisha mita za ujazo 10,000 kwa siku.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post