TEA YAADHIMISHA WIKI YA UTUMISHI KWA UMMA JIJINI DAR ES SALAAM


NA EMMANUEL MBATILO, DAR ES SALAAM

MAMLAKA ya Elimu Tanzania (TEA), katika kuadhimisha Wiki ya Utumishi wa Umma wamekuwa wakipokea maombi kutoka katika taasisi mbalimbali ambazo wanahitaji ufadhili kwa ajili ya kuendelezwa kwa miradi ya elimu nchini.

Ameyasema hayo leo Juni 23,2023 Jijini Dar es Salaam, Kaimu Mkurugenzi Utafutaji Rasilimali na Usimamizi wa Miradi (TEA), Bw. Masozi Nyirenda wakati wakifunga maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma.

Amesema wamekuwa wakipokea watu mbalimbali ambao wamekuja kutaka kupata taarifa kuhusiana na shughuli za Mamlaka ya Elimu Tanzania na kuweza kupewa msaada.

Aidha amesema kupitia Mfuko wa Kuendeleza Ujuzi wanatoa ufadhili wa miradi mbalimbali ya kuendeleza ujuzi ili vijana waweze kupata mafunzo ya kupata ujuzi na kujikumu kimaisha.

"Kuna taasisi ambazo tumekuwa tukifanya nao miradi upande wa Mfuko wa Elimu pamoja na Mfuko wa Kuendeleza Ujuzi ambazo tmekuwa tukifanya vikao nao kwa lengo la kuwapa maelekezo namna gani ya kutekeleza miradi ya pamoja na kutatua changamoto ambazo zinaikabili sekta ya Elimu". Amesema Bw.Nyirenda.

Kwa upande wake Kaimu Meneja Rasilimali Watu na Utawala (TEA), Bw. Kennedy Nsenga amesema katika maadhimisho hayo wamekuwa wakiwaelimisha Watumishi kuhusu maadili ya Utumishi wa Umma ikiwemo kuwahi kazini, kufanya kazi kwa weledi na wakati, nidhamu, mahusiano mema na vilevile kujua haki zao za msingi ambazo wanatakiwa kuzipata katika taasisi.

Nae Katibu Mwendeshaji Ofisi (TEA), Bi. Maria Masanja amesema kupitia maadhimisho hayo wamepokea wateja mbalimbali akiwemo Waziri wa zamani wa Elimu Dkt.Shukuru Kawambwa ambapo alifika katika ofisi za TEA na kutembelea ofisi za Miradi ya elimu.

Amesema Wateja wengine ambao wametembelea Ofisi za TEA Jijini Dar es Salaam katika Maadhimisho hayo ni pamoja na kampuni ya Nissan Tanzania, Kilimanjaro Blinds Trust Africa (KBT), na wadau wengine mbalimbali wa Elimu nchini.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post