MUUGUZI MATATANI TUHUMA ZA KUMBAKA MAMA MJAMZITO BAADA YA KUMCHOMA SINDANO YA USINGIZI WODINI


Na Mwandishi wa JamhuriMedia, Tabora

Jeshi la Polisi Mkoa wa Tabora linamshikilia muuguzi wa hospitali ya Wilaya ya Sikonge kwa tuhuma za kubaka mama mjamzito aliyekuwa amelazwa hospitalini hapo.

Kamanda wa Polisi mkoani humo, Kamishna Msaidizi wa Polisi (ACP) Richard Abwao, amesema kuwa tukio hilo limetokewa wakati mtuhumiwa ambaye ni Afisa Muuguzi Msaidizi (ANO) Rayson Agnelus Duwe akiwa zamu usiku.

Kamanda amesema kuwa mama mjamzito huyo alifikishwa hospitalini hapo Juni 9, mwaka huu, majira ya saa 2, usiku, akiwa anasumbuliwa na malaria ambapo alilazwa hospitalini hapo kwa ajili ya matibabu zaidi.

Amesema kuwa uchunguzi wa awali unaonesha mtumishi huyo alikuwa eneo la mapokezi ya wagonjwa wa nje (OPD) na aliingia kazini akiwa amelewa.

Kamanda amefafanua kuwa mtuhumiwa akiwa na jukumu la kupokea wagonjwa (mapokezi) alitoka na kwenda chumba cha mgonjwa huyo na kumfanyia kitendo hicho.

Ameongeza kuwa mtuhumiwa alikutwa na wenzake akiwa chumbani humo na pembeni yake kulikuwa na vifaa vilivyotumika kumchoma mhanga dawa ya usingizi ijulikanayo kwa jina la Diazepam injection ambayo ilimfanya mama huyo kupata usingizi hivyo kumbaka.

Aliongeza kuwa uchunguzi wa tukio hilo tayari umekamilika na mtuhumiwa amepandishwa kizimbani ili kujibu tuhuma zinazomkabili.

Akizungumzia tukio hilo mkuu wa wilaya hiyo ambaye ndiye Mwenyekiti wa Kamati ya Ulinzi na Usalama ya wilaya Simon Chacha amesema hatua ya awali waliyochukua ni kumsimamisha kazi huku Jeshi la Polisi likiendelea na kazi yake.

Chanzo - JamhuriMedia

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post